202002LGBT_Tanzania_main

“Tusipopata Huduma, Tutakufa”

Kuandamwa kwa LGBT na Kunyimwa Haki ya Afya Tanzania

Mwanaume anayefanya mapenzi na mwanaume mwenye VVU akiwa katika zahanati jijini Dar es Salaam, Tanzania, Novemba 16, 2016. Kutokana na msako wa serikali kwa jamii ya wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume, mtu huyu amekuwa akiogopa kwenda kuchukua dawa zake kwa wiki mbili pamoja na hatari juu ya afya yake. © 2016 Kevin Sieff / Getty Images

Muhtasari

“Kwasababu ya serikali, watu wa LGBT hawana mahali pa kupata mafunzo [juu ya afya ya ngono]. Watu hawapati vilainishi, hawapati kondomu, hawapati huduma. Kwa kifupi, tunakufa.”


—Victor, mwanaume anayevutiwa kimapenzi na mwanaume, mwenye miaka 25, Dar es Salaam, aliyehojiwa na Human Rights Watch tarehe 28 Septemba 2018

Tanzania iligonga vichwa vya habari mwezi Oktoba 2018 wakati Mkuu wa Mkoa Paul Makonda, alipodai kwamba ameunda kikosi kazi kuwakamata wanaume wote wanaodhaniwa kuwa ni wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wengine katika jiji la pwani la Dares Salaam, “wapimwe” kwa vitendo vyao vya kufanya mapenzi na wanaume wengine, na kuwafunga maisha. Akawataka Watanzania kumtumia jumbe za simu kumtaarifu yeyote anayeaminika kuwa mwanaume anayevutiwa kimapenzi na wanaume, na kudai kuwa amekwisha pokea mamia ya jumbe za namna hiyo.

Shinikizo la kimataifa lilisababisha serikali ya Tanzania kukana matamshi ya ofisa huyo. Katika hatua isiyotarajiwa hasa kutokana na hulka ya Rais wa Tanzania John Magufuli ya kutotaka kuyumbishwa na mitazamo ya kimataifa na mazingira ya chuki dhidi ya watu wa LGBT ambayo ameirasimisha, Magufuli aliahidi katika mkutano na maofisa wa Benki ya Dunia kwamba serikali ingekomesha “vitendo vya kibaguzi vinavyohusiana na udhalilishaji na/au ukamataji” kwa misingi ya mwelekeo wa hisia za kimapenzi.

Vitisho vya Makonda havikutimia, lakini chuki rasmi ya kitaasisi bado imeendelea kushamiri. Mwezi Aprili 2019, bila kujali uhuru wa kufanya mkutano na haki ya afya, na udhihirishwaji wa wazi wa chuki rasmi ya Tanzania dhidi ya LGBT, serikali ililifutia rasmi usajili shirika liitwalo Community Health Education and Advocacy Services (CHESA), moja ya mashirika thabiti yanayofanya kazi ya kuimarisha afya na haki za watu wa LGBT. Inaarifiwa kwamba serikali iliishutumu CHESA kwa “kuhamasisha vitendo visivyokuwa na maadili.” Mwezi Septemba 2019, naibu waziri wa mambo ya ndani alitaka watu wa LGBT kukamatwa, akipingana na ahadi ya serikali.

Kati ya maeneo yaliyoathirika zaidi na uhasama wa wazi wa serikali dhidi ya watu wa LGBT ni haki ya kupata huduma bora ya afya, inayohakikishwa chini ya mikataba ya kimataifa ambayo Tanzania imesaini. Hata ikilinganishwa na nchi zingine zilizoharamisha mapenzi ya jinsia moja, Tanzania imekuwa ya kipekee katika jitihada za kuhakikisha huduma rafiki za afya kwa watu wa LGBT hazipatikani.

Hadi kufikia mwaka 2016, ambapo vitendo vya mapenzi ya jinsia moja vilikuwa bado vimeharamishwa, sekta ya afya nchini Tanzania ilikuwa imetambua na kufanya jitihada kadhaa kushughulikia hatari fulani za kiafya zinazowakabili wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wengine na makundi mengine yanayochukuliwa kama “makundi maalum”, kwa maana kwamba jitihada za kiafya za umma ziwe na juhudi ya kuyashughulikia mahitaji ya makundi haya kama sehemu ya mkakati wa kitaifa wa kujikinga na kutibu VVU. Vyombo mbalimbali vya serikali viliwajumlisha wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume katika mijadala juu ya kujikinga na kujitibu VVU. Kwa ujumla, mbinu ya Tanzania katika kukabiliana na VVU na UKIMWI ilionekana kuwa yenye mafanikio, kutokana na ukweli kwamba ilitokana na mafanikio yenye Ushahidi na iliyojumuisha makundi mengi ya watu kwa kiasi fulani.

Kinyume na mategemeo, tangu mwaka 2016, Wizara ya Afya imezuia mashirika yaliyopo katika jamii kufanya warsha juu ya kujikinga na VVU kwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume na makundi mengine maalum, kwa dhana potofu kwamba mashirika hayo “yanahamasisha ushoga.” Wizara ilifunga vituo vya msaada wa afya kwa makundi maalum(vituo vya msaada)  ambavyo vilitoa huduma za upimaji VVU na huduma zingine kwa makundi maalum, vilivyokuwa vikiendeshwa mara nyingi na mashirika ya kimataifa, ikidaiwa kwamba vituo hivi, pia, vilikuwa vinajihusisha na “shughuli za kuhamasisha ushoga.” Ilipiga marufuku usambazwaji wa vilainishi, nyenzo muhimu ya kujikinga na VVU kwa makundi maalum na kwa jamii nzima kwa ujumla, ikiwa ni pamoja na wanawake waliojifungua.

Wizara ya Afya inadai kwamba vituo vya afya vya umma nchini Tanzania vinatoa huduma bila kuwabagua watu wa LGBT na makundi maalum na kwamba hakuna haja ya kuwa na huduma maalum ambazo zinafanywa na taasisi za kiraia. Lakini Human Rights Watch imegundua kwamba uwepo wa unyanyasaji na ubaguzi kwa misingi ya mwelekeo wa hisia za kimapenzi na jinsia ya mtu katika vituo vya afya vya serikali ni jambo la kawaida.

Mamlaka pia imekandamiza haki ya afya kupitia matukio mengi ya uvamizi wa polisi katika mikutano na vikao vilivyokuwa vimeandaliwa na wanaharakati wa afya na haki na washirika wao, huku wakiwakamata washiriki, ikiwa ni pamoja na wanasheria wa kigeni, katika jitihada za kunyamazisha na kuitia hofu jamii ya wanaharakati pamoja na makundi yanayotoa huduma pamoja na wanaufaika wa huduma hizo. Miongoni mwa shughuli zilizofungwa na polisi ni pamoja na mafunzo juu ya elimu ya VVU, viongozi wa watu wa LGBT kuhofia kuhudhuria warsha hizi ambazo zinaweza hata kuokoa maisha.

Polisi wameendelea kufanya ukamataji holela kwa misingi ya mwelekeo wa kimapenzi na utambulisho wa jinsia. Wakati mwingine, polisi wamewataka watoa huduma kufanya vipimo vya lazima vya njia ya haja kubwa ili kupata uthibitisho wa ufanyaji mapenzi wa kishoga. Upimaji huu si sahihi na ni ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu unaoweza kuwa ni utesaji. Ukamatwaji na unyanyaswaji wa watu wa LGBT si tu unakiuka haki yao ya faragha, kutokubaguliwa na kutokuteswa, lakini unafanya makundi nyonge kujificha na kwenda mbali na huduma za afya, na kuhatarisha zaidi haki yao ya afya.

Human Rights Watch inaitaka Wizara ya Afya ya Tanzania kuachana mara moja na sera zake za afya zinazokiuka haki za watu, ikiwa ni pamoja na katazo la usambazaji wa vilainishi na utolewaji warsha za jinsi ya kujikinga na VVU na uendeshwaji wa vituo vya msaada uliokuwa ukifanywa na mashirika ya kijamii yanayowahudumia watu wa LGBT na makundi maalum. Mamlaka za Tanzania zinapaswa kuacha ukamataji kwa misingi ya mwelekeo wa hisia za kimapenzi na utambulisho wa kijinsia, na kuacha upimwaji wa nguvu wa njia ya haja kubwa, kurekebisha sheria na sera ambazo zinabagua katika misingi ya mwelekeo wa hisia za kimapenzi na utambulsiho wa kijinsia na kuhakikisha uhuru wa kukutana wa makundi yanayofanya kazi ya kulinda upatikanaji wa huduma za afya na haki zingine za watu wa LGBT.

 

Mapendekezo

Kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Zanzibar

  • Jiepushe na  kutoa kauli za chuki dhidi ya watu wa LGBT na wawajibishe maofisa wa serikali kwa kauli na vitendo vya chuki dhidi ya watu wa LGBT.
  • Timiza ahadi ya kutokomeza unyanyasaji na ukamataji kwa misingi ya mwelekeo wa hisia za kimapenzi

Kwa Ofisi ya Waziri Mkuu

  • Hakikisha kwamba sera ya afya na nyaraka za mbinu za utekelezaji zinazochapishwa chini ya uangalizi wa Ofisi ya Waziri Mkuu, ikiwa ni pamoja na Mkakati wa Taifa wa Kudhibiti VVU na Ukimwi na utekelezaji mwingine wowote kutoka Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS), zinatokana na Ushahidi na zinaendana na utendaji kazi unaotambulika kimataifa, ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa vilainishi na warsha za kijamii.

Kwa Wizara ya Mambo ya Ndani

  • Waelekeze polisi Tanzania bara na Zanzibar kuacha ukamataji kwa misingi ya mwelekeo wa hisia za kimapenzi, utambulisho wa kijinsia, na kuacha uvamiaji wa vikao na warsha zinazoandaliwa na watetezi wa makundi ya LGBT na afya.
  • Toa tamko la kukataza polisi kutumia vipimo vya njia ya haja kubwa kama namna ya kutafuta uthibitisho katika mashitaka ya vitendo vya mapenzi ya jinsia moja.

Kwa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto (Tanzania Bara)

  • Toa agizo la kuondoa katazo la usambazaji wa vilainishi.
  • Ruhusu mashirika yasiyo ya kiserikali kufungua tena vituo vya misaada vinavyotoa huduma za afya kwa watu wa LGBT na makundi mengine maalum.​
  • Ondoa katazo kwa mashirika ya kijamii kutoa elimu ya VVU na warsha zinazowalenga wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wenzao na makundi maalum.
  • Acha matamko yanayoshutumu mashirika yanayofanya kazi ya kutoa huduma za afya kwa makundi maalum kuwa “yahamasisha ushoga.”

Kwa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto (Tanzania Bara) na Wizara ya Afya Zanzibar

  • Toa ilani kali ambazo zinapiga marufuku kwa wahudumu wa afya kutotekeleza au kusaidia katika upimaji wa njia ya haja kubwa kama namna ya kutafuta Ushahidi wa vitendo vya mapenzi ya jinsia moja, misingi ya kwamba kushiriki katika uchunguzi kama huo ni ukiukaji wa maadili ya kitabibu na kwamba uchunguzi kama huo si wa kisayansi na hauna manufaa yoyote ya kitabibu.
  • Hakikisha ya kwamba sera za afya na hati za mikakati ambazo zimechapishwa chini ya uangalizi wa Wizara ya Afya, ikiwa ni pamoja na Mpango Mkakati wa Kitaifa wa Kupambana na VVU na UKIMWI, na mchango mwingine wowote kutoka Tume ya UKIMWI ya Tanzania (TACAIDS), zinategemea ushaidi na kuendana na taratibu bora zinazotambulika kimataifa, ikiwemo kuzingatia upatikanaji wa vilainishi na ufikiaji wa huduma katika jamii.
  • Chukua hatua za kuhakikisha kondumu na vilainishi vya maji na silika vinapatikana kwa wingi, kupitia mashirika yasiyo ya kiserikali na mashirika ya kijamii pamoja na hospitali na kliniki za serikali.
  • Wafundishe watumishi wa afya wa serikali kutowabagua wagonjwa kwa misingi ya mwelekeo wao wa hisia za kimapenzi na utambulisho wa kijinsia. Shirikiana na mashirika ya LGBT ya Kitanzania au ya kikanda katika kupanga na kutekeleza mafunzo yote.
  • Wawajibishe wahudumu wa afya kupitia mfumo wa kutoa malalamiko kwa siri unaowawezesha wagonjwa kutoa malalamiko yao kuhusiana na unyanyaswaji na ubaguzi, na utakaopelekea uchunguzi na hatua za kinidhamu dhidi ya wahudumu wote wa afya watakaopatikana kuwabagua wagonjwa kwa misingi ya mwelekeo wa hisia zao za kimapenzi, utambulisho na muonekano wao wa kijinsia.
  • Idhinisha jumbe maalum za afya zilizohakikiwa na jamii husika kuwafikia wana-LGBT na kutoa taarifa za maamuzi mazuri kiafya yahusuyo kujamiiana
  • Unga mkono hadharani na tetea uondoaji jinai wa mahusiano ya hiyari ya kimapenzi ya jinsia moja.

Kwa TACAIDS, Programu ya Taifa ya Kudhibiti UKIMWI, Tume ya UKIMWI ya Zanzibar,na Mpango Jumuishi wa Zanzibar wa VVU, Homa ya Ini, Kifua Kikuu na Ukoma (awali ilijulikana kama Programu ya Kudhibiti UKIMWI Zanzibar)

  • Hakikisha ya kwamba hati zote za sera na mikakati ya afya zilizotungwa zinategemea ushahidi na zinawiana na taratibu bora zinazotambulika kimataifa
  • Tumieni vyema utaalamu wenu wa afya kwa manufaa ya kutetea kwa kushirikiana na serikali ya Tanzania kwa ujumla kuhusu taratibu bora za VVU na UKIMWI, ikiwa ni pamoja na kurahisisha upatikanaji wa vilainishi vya maji na vile vya silika, na umuhimu wa ufikiaji wenye lengo na utoaji wa huduma rafiki za VVU kwa wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume na makundi mengine maalum.

Kwa Bodi ya Uratibu wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali na Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali

  • Batilisha ufutwaji usajili wa mashirika yanayofanya kazi ya kupigia chepuo afya na haki za binadamu za wana-LGBT na makundi mengine ya wanyonge, ikiwa ni pamoja na wafanyabiashara ya ngono, na kuruhusu mashirika hayo kusajiliwa siku za usoni.
  • Kujizuia kutumia hatua kali zinazoruhusiwa chini ya Sheria mpya (Miscellaneous Amendments) Na. 3 ya 2019, ikiwa ni pamoja na uchunguzi na tathmini ya mashirika yasiyo ya kiserikali.

Kwa Jeshi la Polisi la Tanzania na Jeshi la Polisi la Zanzibar

  • Acha ukamataji holela kwa misingi ya mwelekeo wa hisia za kimapenzi, utambulisho na muonekano wa kijinsia.
  • Acha kuvamia mikutano na warsha zinazoandaliwa na watetezi wa haki za wana-LGBT na afya.
  • Tokomeza matumizi ya nguvu ya upimaji wa njia ya haja kubwa kama namna ya kutafuta ushahidi wa vitendo vya mapenzi ya jinsia moja.

Kwa Bunge la Tanzania bara na Zanzibar

  • Kupitia kamati ya kudumu ya VVU/UKIMWI (Tanzania), fanya uchunguzi wa athari za sera zinazotekelezwa na Wizara ya Afya tangu mwaka 2016, ikiwa ni pamoja na marufuku ya usambazwaji wa vilainishi, marufuku ya warsha za VVU kwa wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume, na kufungwa kwa vituo vya msaada, pamoja na matukio yoyote ya kunyimwa kwa huduma na kubaguliwa kwa wana-LGBT na makundi maalum katika kupata huduma za VVU/UKIMWI.
  • Kutekeleza majukumu ya uangalizi ya Kamati Maalum ya Bunge ya Maswala ya Kigeni, Ulinzi na Usalama (Tanzania) na ile Kamati ya Katiba, Haki na Uongozi  (Zanzibar) kwa kuchunguza unyanyasaji wa polisi kwa wana-LGBT, ikiwa ni pamoja na uvamizi wa mikutano, ukamataji holela, na matumizi ya nguvu ya vipimo vya njia ya haja kubwa.
  • Rekebisha Sheria ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ya 2002, mkiondoa vipengele vilivyoongezwa kwa kupitia Sheria mpya (Written Laws (Miscellaneous Amendments) Na. 3 ya 2019 inayomruhusu Msajili wa NGO kuingilia shughuli za usajili za mashirika yasiyo ya kiserikali, ikiwa ni pamoja na kupepeleza na kutathmini shughuli zao.
  • Fanya marekebisho ya sheria kuondoa jinai mapenzi ya jinsia moja ya hiyari kati ya watu wazima kwa kuondoa vifungu 138A, 154, 155, na 157 kutoka kwenye Sheria ya makosa ya jinai ya Tanzania, na vifungu 150, 151, 153, 154, na 158 kutoka Sheria ya Makosa ya Jinai ya Zanzibar.

Kwa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

  • Timiza ahadi ya Oktoba 2018 ya “kuheshimu makubaliano yote ya kimataifa kuhusu haki za binadamu yaliyotiwa sahihi na kuridhiwa” kwa kutetea ndani ya serikali kurudishwa kwa huduma za afya zinazohitajika kutimiza haki ya afya kwa wana-LGBT na kukomeshwa kwa unyanyasaji wa polisi, ukamatwaji holela, na matumizi ya vipimo vya nguvu vya njia ya haja kubwa.

Kwa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania

  • Acha kuviadhibu vyombo vya habari vinavyotoa sauti kwa wana-LGBT au kujadili haki za wana-LGBT kwa namna chanya au isiyo na upendeleo.

Kwa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB)

  • Kama lilivyo jukumu lenu la kufuatilia kikamilifu ukiukwaji wa haki za binadamu, kunakili na kuripoti ukiukwaji wa haki za binadamu zinazoathiri wana-LGBT wa
  • Tanzania, ikiwa ni pamoja na ukiukwaji wa haki ya afya na haki ya uhuru wa kujieleza na uhuru wa kukutana, pamoja na ukamatwaji holela na upimwaji wa nguvu wa sehemu ya njia ya haja kubwa.
  • Kwa mujibu wa jukumu lenu la kusimamia utekelezaji wa serikali wa mikataba ya kimataifa na kupendekeza mabadiliko ya sheria ili kuhakikisha utekelezaji huo, simamia kuondoa ujinai katika vitendo vya hiari vya mapenzi ya jinsia moja

Kwa Ofisi ya Mratibu wa Ukimwi wa Marekani Ulimwenguni, na Mwakilishi Maalum wa Afya ya Kidiplomasia Ulimwenguni (OGAC), mwenye wajibu wa Mfuko wa Dharura wa Rais wa Msaada wa UKIMWI (PEPFAR), na Shirika la Marekani la Maendeleo la Kimataifa (USAID)

  • Itake Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ya Tanzania kutimiza ahadi iliyotoa katika mchakato wa PEPFAR wa 2019  wa kuidhinisha msaada mpya, ikiwa ni pamoja na kufanya mabadiliko katika sera ya afya na kupiga marufuku upimwaji wa lazima wa sehemu ya njia ya haja kubwa.
  • Hakikisha ya kwamba Mfuko wa Uwekezaji ya Makundi Maalum (Key Population Investment Fund) unatoa ruzuku ambayo inayalenga mashirika yanayoongozwa na wana-LGBT, na kwamba asasi kama hizo zinapata ruzuku za kutosha na ufadhili kupitia mikondo yote ya ufadhili wa PEPFAR.

Kwa Programu ya Pamoja ya Umoja wa Mataifa ya VVU/UKIMWI (UNAIDS)

  • Kutafuta kila fursa kutumia mamlaka yake ya kuhimiza majadiliano kati ya maofisa wa serikali na wana-LGBT.
  • Hakikisha uzingatiaji na utoaji wa ujuzi kwenye miongozo ya kikanuni katika kukabiliana na VVU miongoni mwa makundi maalum.
  • Fanya ziara ya viongozi wa juu kukutana na mamlaka za Tanzania ya kuwataka kuheshimu haki, na kuchukua jitihada za kukinga na kutibu VVU kwa mujibu wa ushahidi.

Kwa Mfuko wa Kimataifa wa Kupambana na UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria

  • Kwa kuzingatia sera ya Mfuko Endelevu wa Ulimwengu , Sera ya Mpito na Ufadhili wa Pamoja, hakikisha kwamba serikali ya Tanzania inachukua hatua za muhimu kushughulikia haki za binadamu na vikwazo vinavyozuia ufanisi katika kupambana na VVU na kwamba inaboresha mazingira ya sheria na sera kwa wana-LGBT, na kufanya tathmini ya mara kwa mara, pamoja na makundi maalum na ushiriki wa wana-LGBT ya programu za haki za binadamu inayoongozwa na serikali na kufadhiliwa na Mfuko wa Kimataifa (Global Fund).
  • Kuhakikisha kwamba Mfumo wa Uratibu wa Nchi (MUN) Tanzania bara na Zanzibar unashughulikia masuala ya afya na haki ya wana-LGBT na unaacha nafasi kwa wana-LGBT, na kwamba wana-LGBT wana nafasi ya kutosha kutoa maoni yao ndani ya MUN.

Kwa Benki ya Dunia

  • Kumuwajibisha Rais Magufuli kwa ahadi aliyoitoa kukomesha unyanyasaji na ukamatwaji holela kwa misingi ya mwelekeo wa hisia za kimapenzi, ikiwa ni pamoja na kufuatilia ukiukwaji wa haki, kufanya majadiliano ya mara kwa mara na asasi za kirai zinazoshughulika na maswala ya LGBT, na kuitaka serikali kuchukua hatua zote za muhimu kukomesha ukiukwaji wa haki.
  • Kufanya uhakiki wa vihatarishi kuhakikisha kwamba hakuna mkopo wowote utakaotolewa kwa Tanzania utachangia katika unyanyasaji kwa misingi ya mielekeo ya hisia za kimapenzi au utambulisho wa kijinsia, na kwamba hakuna mradi wowote unaofadhiliwa na Benki ya Dunia utatekelezwa kibaguzi.

Kwa Wafadhili Wengine wa Tanzania

  • Unga mkono asasi za kiraia zinazoongozwa na wana-LGBT, kupitia fedha, msaada wa kitaalamu, na kuwezesha majadiliano na mamlaka za serikali.
  • Hakikisha kwamba fedha zinazotolewa kwa ajili ya VVU/UKIMWI nchini Tanzania ziwe na fedha maalum zinazolenga mahitaji ya kiafya ya wana-LGBT, na zisimamiwe kwa ukaribu kujua kiasi gani hasa cha fedha kinatumika.
  • Pawepo na “fedha za dharura” kusaidia wanaharakati wa LGBT wanaoathirika na kuandamwa, kunyanyaswa na kukamatwa holela.
  • Shirikianeni na wafadhali wengine kuhakikisha kwamba kunakuwepo na msaada wa kutosha na endelevu kuwasaidia wanaharakati wa LGBT wanaofanya kazi zao.
  • Zungumzeni na serikali ya Tanzania hadharani na faragha, kuwasukuma maofisa kuheshimu haki za wana-LGBT chini ya sheria ya kimataifa.
 

Mbinu ya Utafiti

Ripoti hii imesheheni zaidi mahojiano yaliyofanywa na Watanzania 35 wanaojitambulisha kama wana-LGBT kati ya Mei 2018 na Juni 2019. Kwasababu ya jitihada za serikali ya Tanzania kuzuia uchunguzi huru wa ukiukwaji wa haki za binaadamu, Human Rights Watch ilifanya mahojiano mengi kwa mbali kupitia mbinu mbalimbali za simu na video.

Human Rights Watch pia ilifanya kazi na mtaalamu nchini Tanzania ambaye ana uzoefu wa mbinu ambazo shirika huzitumia, ambaye alifanya mahojiano ya ana kwa ana jijini Dar es Salaam na Zanzibar na kwa kutumia simu kwa wahojiwa wengine waliopo Tanga, Arusha, na Morogoro, ambaye pia alisaidia Human Rights Watch kuunganishwa na waliohojiwa kwa njia ya simu wakiwa mbali. Mahojiano yalikuwa nusu rasmi yalifanyika kwa lugha ya Kiingereza na Kiswahili kutegemea maswali yaliyojikita zaidi na upatikanaji wa afya, lakini yalikuwepo pia maswali kuhusiana na ukamatwaji na unyanyasaji kwa misingi ya mwelekeo wa hisia za kimapenzi au utambuisho wa kijinsia.

Waliohojiwa wote walijulishwa kwamba mahojiano yalikuwa ya hiari na kwamba wangeweza kukataa kujibu swali lolote na kusimamisha mahojiano muda wowote. Hakuna aliyelipwa kwa kushiriki mahojiano. Wahojiwa wengi wana-LGBT wa Kitanzania wamepewa majina bandia katika ripoti hii kuhakikisha faragha na usalama wao; pale majina bandia yalipotumika, hilo limeonyeshwa katika rejea ya chini ya ukurasa.

Human Rights Watch waliwatafuta hasa wahojiwa ambao wamewahi kukutwa na unyanyasaji katika kupata huduma ya afya, hasa inayohusiana na kuzuia na kutibu VVU na huduma nzima kwa ujumla. Kwasababu wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume na wanawake wasio na jinsia ya asili wanakabiliwa na hatari kubwa zaidi ya kupata VVU na ndio walikuwa katika hatari kubwa zaidi ya kuathiriwa na marufuku ya Wizara ya Afya ya vilainishi na kuondolewa kwa huduma rafiki kutoka katika jamii, hao ndio walifanya sehemu kubwa ya wahojiwa wetu. Lakini kwasababu tulitaka kujua namna gani msako wa wana-LGBT umewayaathiri makundi yote ya wana-LGBT, tuliwahoji pia wanaume wasio na jinsia ya asili na wanawake wanaovutiwa na wanawake wenzao. Kwa ujumla, wahojiwa ishirini na tatu walikuwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume ambao walijitambulisha kwa majina tofauti tofauti kama vile shoga, wanovutiwa kimapenzi na jinsia zote mbili, na kuchu (neno la jumla lililotengenezwa na wanaharakati wa wana-LGBT wa Uganda). Wahojiwa watano walikuwa ni wanawake wenye jinsia tofauti na asili, wanne walikuwa ni wanaume wenye jinsia tofauti na asili, wawili walikuwa ni wanawake wanaofanya mapenzi na wanawake, na mmoja alijitambulisha kutokufungamana na upande wowote. Kwasababu tuliwapata wahojiwa hawa kupitia asasi za kiraia na kwa kujuana na mtu, wengi wa wahojiwa walikuwa wakitokea maeneo ya mjini na wenye uwezo wa kupata huduma za LGBT. Baadhi ya sauti za watu wa hali ya chini kupindukia wa Tanzania na wana-LGBT waliotengwa, ikiwa ni pamoja na wale wanaoishi vijijini na wale ambao bado wanajificha sana, hazijajumuishwa katika ripoti hii.

Ripoti hii pia imetokana na mahojiano rasmi na mazungumzo yasiyo rasmi na wanaharakati wa haki za LGBT wa Tanzania, wanaharakati wa haki za binadamu, na wanasheria kati ya mwaka 2014 na 2019 na kupitia safari fupi fupi za utafiti nchini Tanzania mwaka 2014 na 2017, na katika mahojiano na wawakilishi wa mashirika ya Kitanzania, kikanda na kimataifa ya haki za binadamu na wataalamu, wafadhili na mashirika ya Umoja wa Mataifa.

Ripoti hii ni muendelezo wa utafiti uliofanywa na Human Rights Watch mwaka 2012 na 2013 na shirika la Wake Up Step Forward Coalition (WASO), ambalo kwa wakati huo lilikuwa mtandao wa mashirika manne ya Kitanzania yaliyojikita katika afya na haki za wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wengine (tofauti na shirika lingine ambalo linafanya kazi Tanzania hivi sasa ambalo linaitwa WASO). Katika utafiti huo, ambao ulitoa ripoti “Tuchukulie Kama Binadamu”: Ubaguzi dhidi ya Wafanyabiashara ya Ngono, Walio wachache Kijinsia na Wanaotumia Dawa za Kulevya nchini Tanzania” tuligundua kwamba ubaguzi na unyanyasaji viliwazuia wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume, wafanya biashara ya ngono, na watumiaji wa madawa ya kulevya kupata huduma za serikali. Tangu mwaka 2014 hadi katikati ya 2016, watafiti wa Human Rights Watch waliendelea kuwasiliana mara kwa mara na wanaharakati wa LGBT na makundi maalum nchini Tanzania na wadau wengine pia ili kuchangia katika jitihada za kutetea. Baadhi ya taarifa zilizokusanywa wakati ule zimetumika pia katika ripoti hii.

Tofauti na katika utafiti wetu wa mwaka 2013, kwa ripoti hii hatukuwahoji wafanyabiashara ya ngono na watumia madawa ya kulevya labda ikiwa walijitambulisha pia kuwa ni wana-LGBT. Hata kama wafanyabiashara ya ngono na watumia madawa ya kulevya wameathirika na kutolewa kwa huduma muhimu za afya na kwa kuongezeka kwa unyanyasaji wa serikali ya Magufuli, tuliamua kujikita zaidi katika chembechembe za chuki na msako dhidi ya wana-LGBT. Kazi ya muhimu zaidi bado inahitajika kufanywa juu ya namna gani wafanyabiashara ya ngono na watumia madawa ya kulevya wameathirika

Human Rights Watch iliwasiliana na Wizara ya Afya katika siku za awali za chuki na msako dhidi ya wana-LGBT, mwezi Agosti 2016, kuelezea wasiwasi wao kuhusiana na marufuku ya vilainishi na kutaka ufafanuzi zaidi juu ya msimamo wa serikali. Hatukupokea majibu yoyote ya barua iliyotumwa. Mwezi Disemba 2019, Human Rights Watch ilituma barua kwa Wizara ya Afya na Wizara ya Katiba na Sheria ikitoa muhtasari wa matokeo ya ripoti hii na kuomba ufafanuzi wa msimamo wa serikali, lakini haikupata majibu.

 

Mtiririko wa Matukio: Mashambulizi ya Serikali ya Tanzania Dhidi ya Afya na Haki za LGBT, 2016-2019

2016

Aprili 2016: Tanzania inafanya Mapitio ya Ulimwengu ya Msimu (Universal Periodic Review – UPR) katika baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa, ni mapitio yake ya pili ya namna hiyo kwa ujumla na ya kwanza tangu kuapishwa kwa Rais John Pombe Magufuli mwezi Novemba 2015. Kikundi Kazi cha Tanzania cha Makundi Maalum na Walio wachache kiulekeo wa Mapenzi, linalojumuisha mashirika 19 ya Kitanzania, liliwasilisha ripoti mbadala iliyosheheni visa vya unyanyasaji wa polisi, ubaguzi na ukatili.[1] Nchi sita zilitoa mapendekezo ya kuondoa jinai katika vitendo vya mapenzi ya jinsia moja na kulaani hadharani ubaguzi wa chuki kwa wana-LGBT.[2]

Mei 20, 2016: Baraza la Haki za Binadamu lilichapisha ripoti ya Kikundi Kazi cha Mapitio ya Ulimwengu ya Msimu (UPR), ikionyesha kwamba Tanzania ilikataa mapendekezo yote yaliyohusiana na mwelekeo wa kihisia za kimapenzi na utambulisho wa kijinsia.[3]

Juni 28, 2016: Kaoge Mavuto, mwanamke asiye na jinsia ya asili, alifanya mahojiano na luninga ya Clouds ambapo alizungumzia huduma za afya zinazotokana na jamii, ikiwa ni pamoja na kondomu na vilainishi.[4]

Juni 29, 2016: Mbunge anaeleza bungeni kutokufurahishwa kwake na kituo cha Clouds “kuhamasisha mapenzi ya jinsia moja,” na kusababisha mjadala bungeni.[5]

Julai 2, 2016: Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda, anatoa hotuba ya uchochezi ambapo anatishia kuwakamata wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume pamoja na yeyote “anayewafuata” katika mitandao ya kijamii watu wanaojihusisha na mapenzi ya jinsia moja, na kuyafuta mashirika yote “yanayohamasisha mapenzi ya jinsia moja”[6]

Julai 8, 2016: Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania inaitaka Clouds TV kuomba msamaha kwa kurusha mahojiano na mwanamke asiye na jinsia ya asili.[7]

Julai 15, 2016: Katika mkutano wa hadhara, waziri wa afya wa Tanzania bara, Ummy Mwalimu, anatangaza marufuku ya usambazaji wa vilainishi katika hospitali na vituo vya afya vya serikali.[8] (Tanzania bara na Zanzibar wana mawaziri tofauti wa afya, sehemu ya Zanzibar kujitegemea. Labda katika mahali ambapo imesemwa vinginevyo, wizara ya afya au waziri wa afya anayezungumziwa katika ripoti hii ni wa bara; Wizara ya Afya Zanzibar, kwa kadiri ya uelewa wa Human Rights Watch, haijachukua hatua dhahiri za kuzuia upatikanaji wa haki ya afya kwa wana-LGBT.)

Julai 19, 2016: Wizara ya Afya ya bara inachapisha tamko kupinga usambazwaji wa vilainishi na “uhamasishaji wa mapenzi ya jinsia moja.”[9]

Julai 23, 2016: Naibu waziri wa afya wa bara Khamis (Hamisi) Kigwangalla, ana-tweet kwamba vilainishi bado vitaendelea kupatikana katika hospitali za serikali, lakini serikali itayazuia maduka ya dawa kuuza au mashirika yasiyo ya kiserikali kugawa.[10]

Julai 29, 2016: Waziri wa Sheria Harrison Mwakyembe anatishia kuzishitaki asasi zote za kiraia kwa “kuhamasisha” mapenzi ya jinsia moja, ikiwa ni pomoja na kusambaza vilainishi.[11]

Agosti 1, 2016: CHESA inapokea barua kutoka msajili wa NGO ikiwajulisha nia yake ya kufutia usajili shirika kwa shutuma kwamba linahamasisha ushoga.[12]

Agosti 11, 2016: Naibu Waziri Kigwangalla anatoa tamko katika gazeti na mitandao ya jamii, akiwaita LGBT Voice, kikundi ambacho kimekuwa kikikemea chuki dhidi ya wana-LGBT inayoungwa mkono na serikali, kwenda ofisini kwake siku inayofuata. LGBT Voice hawatii amri wito kama huo.[13]

Agosti 15, 2016: Naibu Waziri Kigwangalla, akiwa na polisi na maafisa usalama, wanavamia ofisi za CHESA, wanawahoji wanaharakati, wanapekua ofisi wakitafuta vilainishi, na kuwanyang’anya mafaili. Siku inayofuata, polisi wanamuhoji mkurugenzi wa CHESA John Kashiha kwa takribani saa nane.[14]

Agosti 30, 2016: CHESA wanafungua kesi Mahakama Kuu ya Tanzania kupinga taarifa ya Msajili wa NGO kutaka kuzifutia usajili, na upekuzi na uchukuaji wa vitu uliofanywa na Wizara ya Afya katika ofisi za CHESA, kuwa ni kinyume na katiba.[15]

Oktoba 27, 2016: Wizara ya Afya inasimamisha shughuli zote za “elimu ya afya kwa wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume na vituo vya msaada” kusubiri maandalizi ya miongozo mipya juu ya programu ya VVU kwa makundi maalum na yale yaliyo katika hatari zaidi.[16]

Disemba 14, 2016: Polisi wanavamia mkutano wa afya na haki za binadamu katika hoteli Dar es Salaam, na kuwakamata washiriki nane na kuwahoji ikiwa mkutano huo ulikuwa wa “mashoga.” Wanasheria wanafanikiwa kuachiwa siku hiyo hiyo, lakini polisi wanashikilia vitambulisho vyao kwa siku kadhaa.[17]

Disemba 15 na 16, 2016: Polisi wanavamia baa mbili Zanzibar, wanawakamata wanaume wanaowatuhumu kwa kuvutiwa kimapenzi na wanaume wengine.[18] 

2017

Januari 2017: Polisi wanawakamata wanaume wengi zaidi kwa tuhuma za kuvutiwa kimapenzi na wanaume wengine Zanzibar na kuwapeleka hospitali ya Mnazi Mmoja, ambapo madaktari wanawalazimisha kuwapima kwa nguvu kipimo cha njia ya haja kubwa.[19]

Februari 16, 2017: Wizara ya Afya inaamuru kufungwa kwa vituo vya msaada vipatavyo 40 vinavyotoa huduma za VVU kwa makundi maalum, karibu 30 kati ya hivyo vilikuwa vikiendeshwa na JHPIEGO. Wizara inasema kwamba makundi maalum yanapaswa kwenda kliniki za serikali kupata huduma.

Februari 2017: Polisi wanawakamata wanaharakati wawili kwa kuongoza mafunzo mjini Songea juu ya utambulisho na haki za LGBT.[20]

Februari 2017: Kupitia Twitter, Naibu Waziri Kigwangalla aamuru ukamatwaji wa watu watatu maarufu katika mitandao ya kijamii, ikiwa ni pamoja na Kaoge Mvuto (mwanamke mbadili jinsia aliyefanya mahojiano na Clouds TV mwaka 2016, mara nyingi huitwa kimakosa na taarifa za vyombo vya habari kuwa “mwanaume anayevutiwa kimapenzi na wanaume wengine”), kwa shutuma za “kuhamasisha mapenzi ya jinsia moja.”[21] Mtu mmoja kati yao  anakamatwa, anawekwa kizuizini kwa siku nne, na kupimwa kwa nguvu njia ya haja kubwa, wakati wengine hawakamatwi.[22]

Machi 2017: Polisi Zanzibar wanawakamata wanaume saba kwa makosa ya mapenzi ya jinsia moja.[23]

Machi 2017: Kisiwani Zanzibar, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi wa wakati ule, Ayoub Mohammed, anatishia kufuta usajili wa mashirika yote “yanayohamasisha” vitendo vya mapenzi ya jinsia moja, akiyashutumu mashirika hayo kwa “kuharibu watoto wetu.”[24]

Aprili 2017: Waziri wa Afya anachapisha Miongozo kwa Makundi Maalum na Yaliyo Hatarini ambayo ni mipya ambayo haitaji vilainishi na kutaka shughuli zote za jamii za elimu ya kujikinga na VVU ziwe chini ya serikali.[25]

Juni 22, 2017: Rais Magufuli anashutumu wageni kwa kuleta mapenzi ya jinsia moja nchini Tanzania, akisema “hata ng’ombe, hata mbuzi” hawana mahusiano ya jinsia moja: kauli yake ya kwanza hadharani juu ya masuala ya LGBT.[26]

Juni 25, 2017: Waziri wa Mambo ya Ndani Nchemba anatishia kuyafutia usajili mashirika yoyote na kuwafukuza nchini wanaharakati yeyote “anayehamasisha” mapenzi ya jinsia moja nchini Tanzania.[27]

Septemba 15, 2017: Polisi Zanzibar wanavamia warsha iliyoandaliwa na shirika la kijamii kwa wazazi wa watoto walio sehemu ya kundi la watu maalum juu ya tiba na kujikinga na VVU, wakiwakamata washiriki 20, wanaojitolea na wafanyakazi kwa misingi ya “kuhamasisha ushoga.” Kumi na nane kati yao waliachiwa bila kushtakiwa siku hiyo hiyo, wakati wengine wawili wabaki kizuizini kwa siku mbili.[28] Kamanda wa Polisi wa Mkoa Hassan Ali Nasri alitishia “kuwawinda na kuwashitaki” wana-LGBT.[29]

Oktoba 17, 2017: Polisi wanavamia warsha ya masuala ya kisheria (strategic litigation) katika hoteli ya Peacock Dar es Salaam, na kuwakamata watu 13, ikiwa ni pamoja na mwanasheria na wanaharakati wa Afrika Kusini na Uganda wakiwakilisha shirika la Initiative for Strategic Litigation in Africa (ISLA), wawakilishi wa shirika la Kitanzania la afya na haki CHESA, na wanaharakati wengine wa Kitanzania. Wanashutumiwa kwa “kuhamasisha ushoga.”[30]

Oktoba 20, 2017: Ofisi ya Msajili wa NGO, chini ya maelekezo ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Watoto na Wazee, wanatoa tamko la kusimamisha kazi za CHESA, kwa shutuma kwamba “linahamasisha ndoa za jinsia moja.”[31]

Disemba 2017: Polisi Geita wanawakamata wanawake wawili kwa makosa ya “vitendo vichafu” baada ya video iliyosambaa ikidai kuwaonyesha wakibusiana wakiwa baa. Mmiliki wa baa hiyo na mwanaume anayeshutumiwa kuisambaza video hiyo pia wanashitakiwa. Upande wa mashitaka unafuta mashitaka Mei 2019, lakini polisi wanawakamata tena wanne hao wakiwashutumu kwa makossa yale yale. Hadi Novemba 2019 kesi yao ilikuwa bado inaendelea.[32]

2018

Oktoba 29, 2018: Paul Makonda, mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, anazungumza na waandishi wa habari akiwataka Watanzania kumtumia majina ya yeyote anayeshukiwa kuwa ni mwanaume anayevutiwa kimapenzi na mwanaume mwingine pamoja na watu wanaotumia mtandao kufanya biashara ya ngono, na kutishia kuanzisha “msako” kwa watu hao wiki inayofuata.[33]

Oktoba 31: Makonda anafanya mkutano mwingine na waandishi wa habari na kusema ameunda kikosi kazi kuwasaka wanaume wote wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wengine ambacho kitaanza kazi Novemba 5. Anasema watuhumiwa “watapimwa” juu ya vitendo vya mapenzi ya jinsia moja, kupewa ushauri ikiwa “wanataka kubadilika”, au vinginevyo kupelekwa gerezani.[34]

Novemba 3, 2018: Polisi wanawakamata wanaume 10 ufukweni Zanzibar, wakiwashutumu kwa kufanya “ndoa ya kishoga.”[35] Wanaachiwa kwa dhamana, lakini wanatakiwa kuendelea kuripoti polisi kila wiki hadi Januari 2019.

Novemba 4, 2018: Wizara ya Mambo ya Nje ya Tanzania inakana matamko ya Makonda, ikitoa tamko kusema “mawazo hayo ni ya kwake mwenyewe na si msimamo wa serikali” na kwamba Tanzania “itaendelea kuheshimu mikataba ya kimataifa kuhusu haki za binadamu iliyosainiwa na kuingizwa katika sheria za nchi.”[36] Kauli hiyo ilifuatia taarifa kutoka wahisani wa kidiplomasia kadhaa wakionyesha wasiwasi wao juu ya makakati wa Makonda wa kuwatafuta wana-LGBT. [37]

Novemba 7, 2018: Benki ya Dunia, mfadhili mkubwa wa Tanzania, wanasitisha ziara za Tanzania, wakisema ni kutokana na “kunyanyaswa na kubaguliwa kwa wana-LGBT, ziara zote za Tanzania zimesimamishwa mara moja hadi pale tutakapo hakikishiwa ulinzi na usalama wa wafanyakazi wote.”[38]

Novemba 14, 2018: Waziri wa Mambo ya Nje wa Denmark anatangaza kwamba Denmark haitatoa msaada wake wa $10 milioni kwa Tanzania kwasababu ya ukiukwaji wa haki za binadamu, ikiwa ni pamoja na ubaguaji wa watu kwa misingi ya mwelekeo wa kiijinsia.[39] Wiki chache baadae, Denmark inautoa msaada huo.[40]

Novemba 17, 2018: Maofisa wa ngazi za juu wa Benki ya Dunia wanakutana na Rais Magufuli kujadili sera za Tanzania za kuwatenga wasichana wajawazito na kina mama watoto kutoka shule za sekondari, sheria yake ya kuzuia uchapishaji wa takwimu zinazokinzana na zile za serikali, na mazingira ya chuki dhidi ya LGBT. Baada ya mkutano, Benki ya Dunia inarudisha tena ziara zake, ikisema katika waraka wake kwamba Rais Magufuli “ameihakikishia Benki kwamba Tanzania haitatekeleza vitendo vyovyote vya kibaguzi vinavyohusiana na kuwanyanyasa na/au kuwakamata watu kwa misingi ya mwelekeo wao wa kijinsia.”[41]

2019

Januari 2019: Maofisa wa eneo wanaamrisha kukamatwa kwa wanaume 13 katika mji mdogo kwa misingi ya kushukiwa kwa muonekano wao wa kijinsia. Polisi wanawalazimisha kuwapima kipimo cha njia ya haja kubwa. Kufuatia kuingilia kati kwa balozi za kidiplomasia, wanaachiwa kwa dhamana. Lakini watatu kati yao wanakamatwa tena baadae jijini Dar es Salaam na kushikiliwa kwa wiki mbili kabla ya kuachiwa.[42]

Machi 2019: Katika mkutano Johannesburg, Afrika Kusini, Mfuko Maalum wa rais wa Marekani wa UKIMWI (PEPFAR) unaitaka serikali ya Tanzania kupiga marufuku upimwaji wa nguvu wa njia ya haja kubwa. Wizara ya Afya ya Tanzania inasambaza waraka uliotolewa Januari 2019, ambao haukuwa unajulikana na wanaharakati wa asasi za kiraia waliohudhuria mkutano huo, ambao unaelekeza hospitali kufanya kipimo cha njia ya haja kubwa pale ambapo kuna amri halali ya mahakama. Wanaharakati wanasisitiza kwamba waraka huu pekee hautoshi, na PEPFAR inaungana nao kutaka kupigwa marufuku kabisa kwa upimaji wa nguvu wa njia ya haja kubwa.[43]

Aprili 2019: Msajili wa NGO Neema Mwanga anatangaza kwamba Bodi ya Uratibu ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, chombo cha serikali kinachofanya kazi kwa kuungwa mkono na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Watoto na Wazee, imefuta usajili wa mashirika sita ikiwa ni pamoja na CHESA. CHESA na mashirika mengine yanatuhumiwa kwa “kuhamasisha vitendo visivyo na maadili.”[44]

Aprili 2019: Asasi za kiraia zinaanzisha wito kuitaka Wizara ya Afya kutekeleza ahadi yake ya kuzuia upimwaji wa nguvu wa njia ya haja kubwa.[45]

Septemba 2019: Akiwa Zanzibar, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani Hamad Masauni anaagiza kukamatwa kwa yeyote “anayehamasisha” mapenzi ya jinsia moja.[46]

 

I. Historia

“Sisi ni kama sisimizi tunapigana na tembo.”


—Toni (jina bandia), mwanaharakati wa wasio na jinsia za asili Tanzania, Oktoba 9, 2018

Sheria ya Tanzania imeharamisha kitendo cha ngono ya hiari ya jinsia moja tangu wakati wa utawala wa kikoloni wa Kiingereza (1919-1961).[47] Kwa miongo mingi, unyanyapaa wa kijamii ukijumlishwa na ukandamizaji wa kisheria vimesababisha wana-LGBT wengi kubaki sirini, na kwa wale wanaojulikana au kuhisiwa kuwa LGBT, wamekumbana na ubaguzi wa hali ya juu.[48] Lakini tangu Rais John Magufuli aingie madarakani mwaka 2015, wana-LGBT Watanzania wamekumbana na ukiukwaji wa haki zao kutoka wa kimfumo na kwa kiwango ambacho hakijawahi kutokea kutoka serikalini. Serikali wala haioni haya katika kuwanyima haki za msingi wana-LGBT: katika mchakato wa Mapitio ya Msimu ya Ulimwengu kabla ya Baraza la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu mwaka 2016, serikai si tu ilikataa mapendekezo kuondoa jinai katika kitendo cha ngono ya jinsia moja, lakini ilikataa pia “kupambana na uhalifu wa wazi unaofanywa dhidi ya waliowachache kijinsia/kingono, kuhakikisha kwamba haki yao ya kukusanyika na kufanya mikutano inazingatiwa na kuhakikisha haki ya kuhudumiwa sawa na wengine katika kupata huduma za afya na haki.”[49]

Mazingira ya Kisiasa

Chama cha Rais Magufuli, Chama Cha Mapinduzi, kimetawala Tanzania tangu uhuru. Magufuli alichaguliwa kwa kuahidi katika kampeni kwamba angeinua uchumi haraka na kukomesha rushwa. Katika wadhifa wake kabla ya urais, waziri wa ujenzi, Magufuli alipewa jina la utani “Tingatinga” kwa miradi yake ya ujenzi, jina lililojulikana sana zaidi kwasababu ya aina yake ya uongozi, mbali na utengenezaji wa barabara.[50] Tangu kuchukua madaraka, Magufuli amekuwa akipambana na rushwa na matumizi mabaya ya fedha za serikali. Hata hivyo, usemi wake wa “kusafisha” umeiingia hadi kwa wale anaowaona hawakubaliki katika jamii, ikiwa ni pamoja wafanyabiashara ya ngono na watumiaji dawa za kulevya. [51] Kama mtu aliyetoka kijijini na muumini wa Katoliki, Magufuli amekuwa akijielezea kwamba anatenda mambo yake kufuatana na “mapenzi ya Mungu.”[52]

Kutingatinga Haki

Utawala wa Magufuli umegubikwa na jitihada za kuwanyamazisha wakosoaji, ikiwa ni pamoja na kufungia vyombo vya habari na kuwakamata wanaharakati na wapinzani wa kisiasa.

Juni 2019, Magufuli alitia saini mabadiliko ya sheria (The Written Laws (Miscellaneous Amendments No. 3 of 2019), yaliyorekebisha sheria ya NGO na kumpa Msajili wa NGO mamlaka makubwa ya kuchunguza na kutathmini NGO na kusitisha shughuli zake.[53] Hii ilifuatia mapitio mapya ya mwaka 2018 ya taratibu za NGO zinazotaka NGO kuweka hadharani vyanzo vyao vya mapato, pamoja na matumizi na shughuli zinazokusudia kufanya, ndani ya siku 14 tangu kupokea fedha hizo, au la kufutiwa usajili.[54] Mamlaka zimekuwa pia zikitisha NGO moja kwa moja na kutaka kunyamazisha makundi ya asasi za kiraia. Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kilipofanya mkutano na waandishi wa habari Januari 2018 vikishutumu udhalilishwaji wa vyombo vya dola katika uchaguzi, Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA) ilivipiga faini vituo vitano vya televisheni kwa kutangaza tukio hilo, ikidai kwamba maudhui ya mkutano huo wa waandishi wa habari yalikuwa ni ya “kichochezi.”[55] Polisi wamewashikilia wanaharakati wanaoshughulikia masuala ya utawala bora katika serikali za mitaa katika maeneo ya uchimbaji madini.[56]

Vyombo vya habari huru vimekuwa vikishambuliwa pia. Chini ya Sheria ya Makosa ya Mtandao (2015), takribani waandishi watano wameshitakiwa mwaka 2018 kwa kilichodaiwa kuwa ni makosa ya kuchapisha taarifa za uongo. Magazeti manne yalifungiwa mwaka 2017 kwa kuchapisha maudhui yaliyochukuliwa kama ya kuikosoa serikali, wakati mengine yalisimamishwa kwa muda.[57] Polisi wamewapiga na kuwashikilia waandishi bila kuwashitaki.[58]

Mwaka 2016, Magufuli alitoa amri kwamba shughuli zote za kisiasa zisimame hadi mwaka 2020, akitafuta kuudhoofisha upinzani. Polisi wamekuwa wakiitekeleza amri hiyo kwa bidi, wakiwakamata wabunge wa upinzani ambao walikuwa wakitembelea majimbo yao au kufanya mikutano ya hadhara katika majimbo yao na kuwashitaki kwa makosa ya jinai.[59] Mwaka 2019, Bunge lilirekebisha Sheria ya Vyama vya Siasa, na kumpa msajili wa vyama vya siasa mamlaka mapana ya kufuta usajili wa vyama na kutoa hukumu ya kifungo kwa yeyote atakayetoa elimu ya uraia bila kibali.[60] Maofisa wengi kutoka chama cha upinzani cha Chadema wamekabiliwa na mashtaka ya jinai kwa kufanya shughuli za kisiasa. Watu wasiojulikana wamewauwa na kuwajeruhi maofisa wa Chadema katika mashambulio yaliyoonekana kuwa ni ya kisiasa.[61]

Kurudisha Nyuma Mafanikio

Kufuatia ushambuliaji wa Magufuli wa uhuru wa kiraia, haishangazi kwamba wana-LGBT pia, wanashambuliwa.

Mijadala ya wazi ya maswala ya ngono/kujamiiana kwa kiasi kikubwa ni kinyume na utamaduni nchini Tanzania,[62] na kabla ya kuchaguliwa kwa Magufuli, mijadala ya umma juu ya utambulisho na mwelekeo wa kijinsia na kingono ni kama vile haikuwepo kabisa mbali na kauli za chuki kwa wana-LGBT za mara chache chache kutoka kwa baadhi ya wanasiasa.[63] Rais aliyepita Jakaya Kikwete, alipoulizwa juu ya kuondoa jinai kwa vitendo vya kujamiana kwa jinsia moja mwaka 2014, alijibu kwa kukwepa na kusema kwamba “itachukua muda kwa watu kukubali tamaduni ambazo watu/nchi za Magharibi zinazikubali.”[64] Hata hivyo, kati ya mwaka 2007 na 2015, Tanzania ilipiga hatua juu ya masuala ya haki za wana-LGBT katika mkakati wa kupambana na maambukizi ya VVU kwa kuwajumuisha makundi maalum, ikiwa ni pamoja na wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume, watu walio na jinsia tofauti na asili, wafanyabiashara ya ngono na wanaotumia madawa ya kulevya katika mpango wa sera ya afya.[65]

Mashirika ya LGBT hayakufanya kazi kwa uhuru kabisa chini ya utawala wa Kikwete. Mwaka 2014 Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, ambayo wakati huo iliangalia usajili wa NGO, ilifungia iliyokuwa moja ya mashirika makubwa ya LGBT Tanzania, Tanzania Sisi Kwa Sisi Foundation (TSSF), kwa misingi kwamba ilikuwa ikihamasisha vitendo vilivyo kinyume na sheria.[66] Kufutiwa usajili kwa TSSF, ambako kulitengeneza njia kwa kile kilichokuja kutokea mwaka 2016, kulikuja baada ya chapisho katika ukurasa wa Facebook wa shirika hilo ukikosoa kutokuwa na utayari kwa serikali katika kuruhusu mashirika yasiyo ya kiserikali kuingiza vilainishi nchini kama bidhaa ya kusaidia kujikinga na VVU.[67] Mashirika mengine yalifanikiwa kuendelea kufanya kazi zao, hasa kama yaliweza kunyamaza kimya.

Lakini chini ya Magufuli, maafisa wa serikali wameanzisha unyanyasaji kwa asasi za kiraia zinazofanya kazi na jamii za LGBT. Waziri wa Katiba na Sheria Harrison Mwakyembe alitangaza Julai 2016 kwamba angeyashitaki mashirika “yanayohamasisha” mapenzi ya jinsia moja.[68] Kauli hii iliambatana na udhibiti mkali wa mashirika yanayoshughulikia masuala ya LGBT na hata yale yanayoshughulika na afya ya umma na VVU kwa upana zaidi, pamoja na wimbi kubwa la uvamizi, ukamataji, vitisho vya kufutia usajili, na hatimaye ufutiaji usajili wa kweli wa mashirika kadhaa, ikiwa ni pamoja na shirika lijulikanalo kama Community Health Education and Advocacy Services (CHESA) mwezi Aprili 2019. Wakati huo huo, Wizara ya Afya ikaendelea kupunguza huduma kwa wana-LGBT na makundi maalum, kama zilivyonakiliwa katika sehemu ya II ya ripoti hii.

Mwanzoni Rais Magufuli alikuwa kimya juu ya mada ya haki za LGBT. Alivunja ukimya Juni 2017 na kauli kwamba wageni walileta mapenzi ya jinsia moja nchini Tanzania, pamoja na dawa za kulevya na ubakaji. Alisema, “Wanaume kwa wanaume, wanawake kwa wanawake – hata ng’ombe, au mbuzi hawajawahi kufanya hivyo.”[69]

Jitihada za Magufuli kujilimbikizia mamlaka, huku akiwatesa wanyonge, zinafanana na mbinu zinazotumiwa na tawala za kimabavu ulimwenguni kote.[70] Wanaharakati wa haki za binadamu wanaoshughulikia mambo mbalimbali wanashutumiwa kwa kuwakilisha matakwa ya “kigeni” na kuharibu mila na tamaduni za “Kitanzania”, hoja zile zile zinazoelekezwa dhidi ya wana-LGBT. Mwanaharakati mwanamke anayevutiwa kimapenzi na wanawake aliiambia Human Rights Watch mwishoni mwa 2016, “Sijawahi kuona kitu kama hiki kabisa nchini Tanzania. Watu walikuwa wameanza kuwazoea watu wa makundi maalum na wana-LGBT, lakini baada ya kauli za serikali, watu wanadhani LGBT wameletwa kutoka nje ya nchi. Kila mtu anaogopa.”[71]

Moja ya madhara ya ushambuliaji mkubwa wa Magufuli kwa asasi za kiraia ni kwamba mashirika makubwa ya haki za binadamu nchini Tanzania – ambayo, isipokuwa machache tu, yameshindwa kutoa utetezi wa wazi kwa haki za wana-LGBT – wamekuwa wakisita zaidi kuendeleza jitihada zao, kwa kuhofia kwamba zitawaondolea uhalali/kuaminika au, nyakati zingine kwa misingi ya chuki yao ya kibaguzi iliyojificha dhidi ya wana-LGBT.[72]

Muktadha wa Kisheria

Sheria za Tanzania zinazozuia mapenzi ya hiari baina ya watu wa jinsia moja ni kati ya sheria kali ulimwenguni. Tanzania bara, kifungu 154 cha Kanuni ya Adhabu, ambacho kilianzia wakati wa utawala wa kikoloni wa Kiingereza, unatoa adhabu ya “makosa kinyume na maumbile.” Sheria hiyo mwanzoni ilitoa adhabu ya miaka 14 jela, lakini baada ya uhuru, katika mfululizo wa mabadiliko ya sheria, serikali ya Tanzania iliongeza hukumu hiyo kwa kifungo cha miaka 30 hadi Maisha jela. Kifungu cha 155 kinatoa adhabu ya “kujaribu” kwa namna yoyote ile kufanya vitendo kama hivyo kwa hadi miaka 20 jela.[73]

Zaidi, kipengele cha 157 kinatoa adhabu ya “vitendo vichafu kati ya wanaume.” Katika hali ya kutaka kuweka sawa matokeo ya sheria hizi zinazoingilia faragha, mwaka 1998 serikali ya Tanzania ilipitisha Sheria ya Makosa Maalum ya Kingono (Sexual Offenses Special Provisions Act), na kuongeza katika Sheria ya Makosa ya Jinai kipengele kipya cha 138A, ambacho kinaadhibu “vitendo vichafu kati ya wanaume na wanawake kwa hadi miaka mitano jela.”[74]

Visiwani Zanzibar, sharia zinazoadhibu mapenzi ya jinsi moja zimepanuliwa wigo katika miaka ya hivi karibuni. Sheria ya Makosa ya Jinai ya Zanzibar inaadhibu “vitendo vya kingono kinyume na maumbile” (kifungu cha 150) na “vitendo vichafu” (kifungu cha 154) kwa miaka 14 jela kwa kosa la kwanza na 5 kwa kosa la pili, lakini Zanzibar pia inafanya jinai moja kwa moja mahusiano ya kimapenzi kati ya wanawake wawili baada ya kuongeza katika sheria yake ya makosa ya jinai swala la “vitendo vya kuingiliana kinyume na maumbile” (kifungu cha 158) mwaka 2004. Zanzibar pia inaadhibu “muungano” wa jinsia moja (kifungu cha 158).[75]

Sheria haizuii “ushoga” wenyewe, na hakuna sheria inayozuia “kuhamasisha ushoga”, hata kama mashitaka haya yasiyo na maana yametumika nyakati zingine na polisi wa Tazania kuhalalisha ukamataji.

Wakati sheria ya Tanzania inakataza “aina zote” za ubaguzi, na kueleza wazi maeneo yaliyolindwa, ikiwa ni pamoja na “utaifa, kabila, mahali pa kuzaliwa, rangi, dini, jinsia au kituo katika Maisha,” hakuna katazo la wazi katika sheria ya Tanzania juu ya ubaguzi kwa misingi ya utambulisho au mwelekeo wa kijinsia au kingono.[76]

II. Mashambulizi dhidi ya Haki ya Afya

“Serikali ya Tanzania inapaswa kuwaelimisha watumishi wake wa afya jinsi ya kutuhudumia sisi makuchu [wana-LGBT] bila ya kututukana au kutunyanyapaa wakati sisi ni watu kama watu wengine.”


—Mahojiano ya simu ya Human Rights Watch na King, mwanaume anayevutiwa kimapenzi na wanaume wenzao, Mei 21, 2018

Msako wa Tanzania dhidi ya wana-LGBT ulianza na kipindi cha televisheni. Akihojiwa mwezi Juni 2016 katika runinga maarufu, mwanamke asiye na jinsia ya asili, Kaoge Mavuto, alizungumzia uhusiano wake na asasi za kirai zinazotoa mipira ya kiume na vilainishi kama sehemu ya jitihada zao za kujikinga na VVU.[77]

Siku iliyofuata, mbunge aliishutumu runinga hiyo, Clouds TV, kwa “kutukuza ushoga.”[78] Siku kadhaa baadae, tarehe 2 Julai, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, akatoa hotuba ya kuchochea akiahidi kuwakamata wanaume wote wanaovutiwa kimapenzi na wanaume na mtu yeyote yule “anayewafuata” wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume katika mitandao ya kijamii. Makonda, ambaye ni afisa mteule anayedai kuwa na baraka za Rais Magufuli kwa kauli zake, aliahidi pia kufungia mashirika yote ambayo “yanahamasisha ushoga.”[79] Wiki iliyofuata Mamlaka ya Mawasiliano ya Tanzania iliiamuru Clouds TV iombe radhi.[80]

Vilainishi, nyenzo muhimu ya kuzuia VVU, ilikuwa ni moja ya mhanga wa wasiwasi wa kimaadili. Tarehe 15 Julai, katika uzinduzi wa hospitali iliyofadhiliwa na USAID, Waziri wa Afya Ummy Mwalimu alitangaza kupinga usambazaji wa vilainishi katika hospitali za serikali na vituo vya afya. “Hatukubaliani na kuhamasisha ushoga na vitendo vya kishoga,” alisema kwa msisitizo. “Tufanye hizo shughuli za HIV AIDS lakini jamani kugawa vilainishi kwa wanaume wanaoshiriki mapenzi na wanaume wenzao marufuku ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania…. Kwa kweli Mimi nalipiga marufuku nchi nzima.” [81]

Kushtushwa kwa Mwalimu juu ya usambazaji wa vilainishi kunapingana na ukweli kwamba tangu mwaka 2014, Wizara ya Afya yenyewe ilikumbatia swala la usambazaji wa vilainishi kama njia ya kuzuia VVU. (Tanzania bara na Zanzibar zina wizara za afya tofauti. Isipokuwa mahali ilipoelezwa wazi, sehemu nyingine yoyote iliyotajwa wizara ya afya katika ripoti hii inamaanisha ile ya bara.) Chini ya Rais Kikwete, mbinu ya Tanzania dhidi ya VVU/UKIMWI ilikuwa inachukuliwa kuwa yenye mafanikio kwa kiwango fulani: iliyojikita katika ushahidi na kwa kiasi fulani jumuishi kwa makundi maalum.[82] Kati ya mwaka 2010 na 2015, Tanzania iliongeza upatikanaji wa dawa za kufubaza virusi vya UKIMWI (anti-retroviral treatment), ikaanzisha majaribio ya programu za sindano, na kusisitiza ushirikiano na mashrika kutoka katika jamii. Maambukizi mapya ya VVU na vifo vitokanavyo na UKIMWI vilipungua.[83]

Maambukizi ya VVU miongoni mwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wengine ilikadiriwa kuwa ya asilimia 25 maeneo ya mjini Tanzania bara mwaka 2014,[84] ukilinganisha na asilimia 4.7 miongoni mwa idadi nzima ya watu (umri kati ya miaka 15-49) mwaka 2018,[85] iliyoshuka kutoka asilimia 5.1 mwaka 2012.[86] Hakuna takwimu rasmi zilizopo juu ya idadi kamili ya maambukizi ya VVU miongoni mwa wasio na jinsia za asili nchini Tanzania – au katika nchi nyingi barani Afrika[87]— lakini tafiti katika kanda nyingine zinaonyesha kwamba wanawake wasio na jinsi za asili wapo katika hatari kubwa ya kuambukizwa VVU.[88]

Takwimu zimeweka wazi kwamba mwanya wa kuwafikia wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wengine na makundi mengine maalum zilikuwa zikikwamisha jitihada za jumla katika kupambana na maambukizi ya VVU nchini Tanzania: asilimia 14 pekee ya wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wengine ndio waliokuwa wakinufaika na jitihada za kupambana na maambukizi ya VVU ambazo zilikuwa zikilenga mahitaji yao moja kwa moja, kwa mujibu wa dokezo la mwaka 2014 la Mfuko wa Kimataifa[89], wakati serikali ikikadiria kwamba mwaka 2013 ni asilimia 25 pekee ya wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wengine ndio waliofikiwa na programu yoyote ile inayopambana na maambukizi ya VVU.[90] Lakini ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara ya Afya ilitoa mlolongo wa nyaraka za mkakati wa kupambana na VVU kati ya mwaka 2008 na 2014 ikitafuta kuziba mwanya huo, wakipanua mbinu mbalimbali kukabiliana na maambukizi hayo miongoni mwa makundi maalum, ikiwa ni pamoja na kudhibiti unyanyapaa na ubaguzi. Moja ya nyaraka ya mbinu hizo hata ikataka kuondolewa kwa jinai dhidi ya vitendo vya mapenzi ya jinsia moja.[91] Vyombo vya serikali kama vile Tume ya Ukimwi Tanzania (TACAIDS) na Programu ya Taifa ya Kudhibiti UKIMWI Tanzania bara na Tume ya UKIMWI ya Zanzibar ya Zanzibar mara nyingi viliwakaribisha wawakilishi wa makundi maalum mezani kuhakikisha programu za afya jumuishi.

Kufuatia utetezi uliofanywa na mashirika yasiyo ya kiserikali, Mfuko wa Kimataifa wa Kupambana na VVU, Malaria na Kifua Kikuu, na baadae hata Wizara ya Afya yenyewe, Waziri Mkuu alijumuisha kifungu cha vilainishi katika Mkakati wa Tatu wa Taifa wa Kupambana na VVU na UKIMWI, uliochapishwa mwaka 2013. Shirika lisilo la kiserikali la PSI liliingiza mzigo wa kwanza nchini wa vilainishi kwa programu ya kuzuia VVU iliyowalenga wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume mwaka 2015, wakiwa na baraka za Wizara ya Afya.[92]

Mwezi Juni 2016, Tanzania iliunga mkono hadharani azimio la Baraza la Umoja wa Mataifa lililokuwa na kichwa cha habari “Tamko la Kisiasa juu ya VVU na UKIMWI: Mpango wa Haraka wa Kuharakisha Vita dhidi ya VVU na Kumaliza gonjwa la UKIMWI kufikia mwaka 2030.” Kwa mujibu wa tamko hilo, lililoidhinishwa kwa pamoja, nchi zote:

Zinaafiki kwamba ili kupatikana kwa haki zote za binadamu na uhuru wa msingi kwa watu wote, uungwaji mkono wa mwitikio wa ulimwengu juu ya gonjwa la UKIMWI, ikiwa ni pamoja na maeneo ya kinga, tiba, na huduma kwa ujumla, na kutambua kwamba kupambana na unyanyapaa na ubaguzi dhidi ya watu wote waishio na gonjwa hilo, wanaodhaniwa kuishi na gonjwa hilo, waliohatarini kuambukizwa na walioambukizwa na VVU ni sehemu muhimu katika kupambana na maradhi ya VVU ulimwenguni.[93]

Naibu Waziri wa Afya wa Tanzania Hamisi Kigwangalla alisema, “Serikali inapongeza kazi iliyofanywa kuandaa tamko hilo. Kutafsiriwa kwa sera za dunia katika ngazi ya taifa ni jambo muhimu sana kwa maendeleo.”[94]

Wiki chache tu baadae, Tanzania ikabadilisha mawazo. Ikaanza kutekeleza mlolongo wa sera ambazo zinakanusha haki, inazuia mapambano dhidi ya VVU. Hii ni pamoja na kupiga marufuku vilainishi, kuzuia semina za kutembelea watu, na kufunga kwa nguvu vituo vya msaada ambavyo vinatoa huduma za VVU na zingine kwa wana-LGBT na makundi maalum.

Wizara ya afya ambayo kwa ujumla wanaharakati wa LGBT walikuwa wakiiona kama mshirika wao taratibu ikaanza kuwatisha juu ya kile kinachodaiwa kuwa ni “kuhamasisha mapenzi ya jinsia moja:”

Hivi karibuni zimeibuka taarifa kwamba baadhi ya NGO, kwa kutumia mgongo wa shughuli za kupambana na VVU, wamekuwa wakihamasisha vitendo vya mapenzi ya jinsia moja ambayo ni kinyume na sheria….. Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ingependa kufafanua kwamba inazingatia utoaji bora wa huduma na ushauri kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) na mashirika mengine ya kimataifa, lakini yote haya lazima yachukuliwe na kutumika kwa mujibu wa muktadha wa Tanzania kupitia mashauriano na wadau mbalimbali, kuhakikisha kwamba yanaendana na sheria za nchi, mila, na tamaduni. Hii ni pamoja na kuzingatia Sheria ya Makosa ya Jinai.[95]

Wataalamu wa afya ya jamii wamekuwa wakiitambua hiyo jinai, pamoja na unyanyapaa na ubaguzi, inawazuia wana-LGBT kupata huduma za afya na kudhoofisha jitihada za kupambana na VVU.[96] Shirika la Afya Duniani (WHO) bila kumung’unya maneno linakemea uwekaji jinai katika kitendo cha mapenzi ya jinsia moja.[97] Tume ya Afrika ya Haki za Watu na Binadamu imesisitiza:

Kufanya jinai, ukatili na ukiukwaji mwingine wa haki za binadamu kwa misingi ya utambulisho wa kijinsia ni kinyume na sheria ya kimataifa ya haki za binadamu. Ina mchango hasi mkubwa pia katika maambukizi ya VVU na afya ya umma, ikichangia kuchochea mazingira ya hofu yanayowakimbiza wana-LGBT mbali na huduma za VVU. Umiliki wa bidhaa za VVU na zingine za afya zinazoaminiwa kuwa ni kwa matumizi ya wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wengine (kama vile vilainishi) zimekuwa zikitumika kama Ushahidi katika kesi za jinai. Hofu ya madhara yake yanaweza kuzuia utumiaji wa huduma za kiafya na kuwazuia wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wengine kuweka wazi tabia zao za kingono kwa watoa huduma za afya.[98]

Wataalamu wa afya wanaamini pia kwamba nchini zinapaswa kufanya juhudi za uhakika kushughulikia maambuki ya VVU miongoni mwa makundi maalum. Shirika la Afya Ulimwenguni linasisitiza kwamba “Pasipo kushughulikia mahitaji ya makundi maalum, mapambano ya uhakika dhidi ya VVU hayatafikia.”[99] Kuyalenga makundi maalum ni muhimu katika kufikia malengo ya Shirika la Ukimwi la Umoja wa Mataifa (UNAIDS) ya kumaliza UKIMWI ifikapo mwaka 2030.[100] Serikali zisiposhughulikia vya kutosha maambukizi yaliyolimbikizana miongoni mwa makundi maalum, si tu wanashindwa kuwalinda waliohatarini wachache, lakini inaingiza hatarini afya nzima ya umma.

Toni, mwanaharakati asiye na jinsia ya asili, alisema baadhi ya maofisa wa afya waliendelea kujihusisha na programu mbalimbali za afya kwa wana-LGBT na makundi maalum, lakini wakati huo huo wananyamazisha madai ya wanaharakati wa haki za binadamu:

Kuna wakati tulienda katika mkutano ambapo tuliambiwa [na maofisa wa afya wa serikali], ‘Hampaswi kuisema vibaya serikali, serikali ni kama baba yenu na mnapaswa kuitii.’ Tukizungumza kuhusu haki za binadamu wanasema ‘Huu sio wakati mwafaka.’[101]

Makame, mwanaume asiye na jinsia ya asili, aliiambia Human Rights Watch, “Nahisi kwamba Wizara ya Elimu haijali kabisa. Wanajaribu kututafsiri sisi kama vile ni tabia mbaya ya kubadilishwa.”[102] Leticia, mwanaharakati ambaye ni mwanamke anayevutiwa kwa wanawake wenzao, alitoa uchambuzi wa mchanganuo wa ushirikiano na washirika wa zamani katika sekta ya afya: “Unajua, kila mtu anamuogopa rais. Hawawezi kutukingia kifua. Wanatuambia kwamba wanajua kinachoendelea, lakini lazima walinde nyadhifa zao.”[103]

Kupigwa Marufuku kwa Vilainishi

Vilainishi vya maji na vile vya silika ni nyenzo muhimu katika kujikinga na VVU. Mipira ya kiume inaweza kupasuka wakati wapenzi wanajamiana kupitia njia ya haja kubwa bila kutumia kilainishi, au wanapotumia mafuta ya kujipaka kama vile Vaseline. Miongozo ya UNAIDS zinasema kwamba programu za kujikinga na VVU “wakati wowote lazima zihakikishe upatikanaji wa vilainishi vya maji na silika pamoja na mipira ya kiume,” vikisema kwamba vilainishi ni “vya muhimu sana kwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wengine, wafanyabiashara ya ngono, watu wasio na jinsia za asili na wanawake waliojifungua” ili kuongeza utelezi na kupunguza msuguano wakati wa kujamiiana. [104] Shirika la Afya Duniani (WHO) linaelezea “programu jumuishi ya mipira ya kiume na vilainishi” kama muhimu katika mapambano dhidi ya VVU miongoni mwa makundi maalum, ikiwa ni pamoja na wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume, watu wasio na jinsia ya asili, wafanyabiashara ya ngono, watu waliopo gerezani na kwenye vifungo vingine, na watu wanaojidunga na madawa ya kulevya.[105] WHO linaidhinisha vilainishi vya aina vyote – vya maji na vile vya silika, lakini kwakuwa vilainishi vya maji ndio vinapatikana kwa wingi, baadhi ya waliohojiwa, pamoja na maofisa wa Tanzania, walitumia jina la “vilainishi vya maji” hata walipokuwa wakimaanisha vilainishi vya mafuta vya aina yoyote ile.[106]

Vilainishi vya maji na silika havitengenezwi nchini Tanzania. Kabla ya mwaka 2015, wakati vilainishi vilikuwa havikatazwi, vilichukuliwa kama sehemu ya dawa ambayo ingeweza kuingizwa nchini pasipo ruhusa ya Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA), ambayo ni sehemu ya Wizara ya Afya, na mwaka 2013 na 2014 TFDA ilizuia kontena mbili za vilainishi ambazo zilikuwa zimeagizwa na mashirika yasiyo ya kiserikali yanayofanya kazi katika afya ya umma.[107] Kama ilivyojadiliwa katika Sehemu ya I hapo juu, mkanganyiko juu ya upatikanaji wa vilainishi kwa ujumla ndio uliosababisha serikali kuifutia usajili asasi ya Tanzania Sisi Kwa Sisi Foundation (TSSF) mwezi Aprili 2014.[108] Kwa upande mwingine, Chuo Kikuu cha Muhimbili kiliruhusiwa kusambaza pakiti za vilainishi kwa washiriki wa majaribio ya utafiti mwaka 2012.[109]

Shirika la Accountability International (zamani lilijulikana kama AIDS Accountability International), ambalo ni shirika lenye makao yake makuu nchini Afrika Kusini na lililojikita kwenye utafiti na utetezi likiwa na lengo la kuwajibisha serikali juu ya ahadi zake za afya ya umma, liliandaa mkutano jijini Dar es Salaam mwezi Mei 2014 na kuhudhuriwa na washiriki 78 kutoka asasi za kiraia za Kitanzania, ambazo zilikutana kusaidia kutengeneza vipaumbele vya Mfuko wa Kimataifa katika kazi yake ya kupambana na VVU/UKIMWI nchini Tanzania. Waliorodhesha “kiasi kidogo cha huduma rafiki kwa makundi maalum,” ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa mipira ya kiume na vilainishi, kama kipaumbele cha pili kwa rasilimani za Mfuko wa Kimataifa.[110] Wizara ya Afya ya Tanzania ilichapisha miongozo ya taifa juu ya programu za VVU kwa makundi maalum Septemba 2014, ikisisitiza kwamba “kuongeza upatikanaji, unafuu wa gharama na matumizi ya vilainishi vinavyofaa kwa mipira ya kiume miongoni mwa watu kutoka makundi maalum kupitia programu maalum za kusambaza ni njia muhimu katika kupambana na VVU.”[111] Nyaraka za mpango wa Zanzibar wa kupambana na VVU zilikuwa tayari zimetaka upatikanaji wa vilainishi kwa makundi maalum tangu mwaka 2011, [112] na ofisi ya Waziri Mkuu wa Tanzania ilitaka hivyo mwaka 2013, kupitia Mkakati wa Tatu wa Taifa wa Kupambana na VVU na UKIMWI, ambao ulitaka kuongezwa kwa upatikanaji wa vilainishi vya maji kwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume na wafanya biashara ya ngono.[113]

PSI shirika la Kimarekani, hatimaye likapata ruhusa ya kuingiza vilainishi mwaka 2015 kama sehemu ya mradi uliofadhiliwa na Mfuko wa Kimataifa wa kupambana na UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria. Mradi wa PSI, wa kuelimisha wanaume wanaofaya mapenzi na wanaume juu ya uwepo wa bidhaa za kujikinga na VVU, uliisha muda si mrefu. Wakati fulani, Mamlaka ya Dawa na Chakula ilitaka kuzuia mzigo wa vilainishi bandarini. Moja ya kamati ya usimamizi ya Mfuko wa Kimataifa iliyopo nchini ikaandika rasmi kwa serikali kuomba mzigo huo uachiwe, wakikumbusha kwamba vilainishi vimo katika Mpango Mkakati wa Taifa. Wizara ya Afya ikawaandikia TFDA ikiwaomba waviachie vilainishi hivyo, TFDA ikakubali. Shirika lingine la Kimarekani, JHPIEGO, lilianza kuingiza na kusambaza vilainishi mwaka 2016 kama sehemu ya mradi wake unaofadhiliwa na PEPFAR/USAID wa Sauti, ambao ulijumuisha mafunzo ya rika juu ya VVU kwa makundi maalum na yale yaliyo katika hatari. [114]

Usambazaji wa vilainishi wa JHPIEGO haukudumu kwa muda mrefu. Waziri wa Afya Ummy Mwalimu akatangaza vita rasmi katika hotuba yake ya Julai 15, 2016, iliyonukuliwa hapo awali.[115] Tarehe 19 Julai, Wizara ya Afya ikachapisha waraka uliorudisha marufuku ya vilainishi, ukidai kwamba usambazaji wa vilainishi “unapingana na tamaduni zetu,” na kupinga kile alichokiita “uhamasishaji wa mapenzi ya jinsia moja.”[116]

Tarehe 23 Julai, Naibu Waziri wa Afya Hamisi Kigwangalla akachapisha katika ukurasa wake wa Twitter kwamba vilainishi bado vitaendelea kuwepo katika vituo vya afya vya serikali, lakini serikali haitaendelea kuruhusu NGO kuvisambaza kwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume.[117] Siku iliyofuata, waraka katika ukurasa wa Facebook wa Mwalimu ukafafanua kwamba marufuku haihusu wasambazaji wote wa vilainishi, lakini maalum kwa “mashirika yasiyo ya kiserikali (NGO) ambayo hununua na kusambaza vilainishi kwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume.” Waraka ukatishia kufutia usajili mashirika yote ambayo hayatatii amri hiyo.[118] Human Rights Watch ilimwandikia Mwalimu mwezi Agosti 2016 kuonyesha wasiwasi wao kuhusiana na madhara ya kiafya ya marufuku (angalia kiambatanisho I) lakini haikupokea majibu.

Kigwangalla alipoongoza uvamizi akiwa na polisi kwa shirika lisilo la kiserikali la CHESA tarehe 15 Agosti, imejadiliwa zaidi katika Sehemu ya III chini, moja ya malengo ya uvamizi huo ilikuwa ni kutafuta vilainishi, hata kama polisi hawakupata chochote.[119]

Mwalimu alitoa waraka mwingine mwezi Oktoba 2016 ambao ulionekana kusema kwamba si tu usambazwaji unaozuiwa lakini hata matumizi binafsi ya vilainishi kama namna ya kujikinga na VVU hayaruhusiwi pia:

Kwa wakati huu, vilainishi vya maji havitatumika tena kama mbinu ya kujikinga na VVU. Serikali na jamii nzima ya Tanzania inahitaji uthibitisho zaidi juu ya njia hii ikiwa inafanya kazi kweli na kukubalika kwake nchini kabla haijapigiwa chepuo kuwa ni madhubuti katika kujikinga na VVU. Itakapokubalika, Serikali itafikiria kuijumuisha katika mfumo wa manunuzi na usambazaji pamoja na bidhaa zingine za afya.[120]

Human Rights Watch iliwauliza wanaume 26 wanaovutiwa kimapenzi na wanaume na wale wanaovutiwa kimapenzi na jinsia zote tuliowahoji mwaka 2018 na 2019 ikiwa walikuwa na uwezo wa kupata vilainishi vya maji na vya silika. Kumi na sita kati yao walisema hawakuwa wanavipata. Baadhi ya wahojiwa walisema wanatumia mafuta ya nazi kama vilainishi, wakati wengine walikuwa wanatumia mafuta ya kujipaka mwilini kama vile Vaseline au mafuta ya watoto, ambapo yote yanaweza kuharibu mpira wa kiume.[121] Baadhi walisema walikuwa wanatumia mate, ambayo hayalainishi vya kutosha na yanaweza kusababisha kupasuka kwa mpira wa kiume.[122] Wahojiwa hawa walisema walifahamu umuhimu wa vilainishi vya maji kama njia ya kujikinga na VVU na - hatari ya kutumia mafuta ya kujipaka kama vilainishi – zaidi kupitia semina zilizofanywa na mashirika ya LGBT ambayo hayaruhusiwi tena kufanya kazi zao – lakini hawakuwa na namna nyingine tena.

Ahmed, mwenye umri wa miaka 39 anayevutiwa kimapenzi na jinsia zote anayefanya kazi na shirika lililojikita katika afya na haki ya wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wengine, alielezea:  “Hivi sasa hali ni mbaya zaidi, [vilainishi] havipatikani popote pale…. Nilikuwa na vilainishi kutoka ofisini ambavyo nilikuwa nimeviweka na nilikuwa bado navitumia na kuwapa wengine kwa siri, lakini sasa havipo tena.”[123]

Wanaume kadhaa wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wengine walisema waliweza kununua vilainishi aidha vya maji au vya silika katika maduka ya dawa. Lakini wengine hawakuweza kumudu.[124] Hata wale walio na uwezo, maduka ya dawa waliwawekea vikwazo vingine. Jephter, mwanaume anayevutiwa kimapenzi na mwanaume mwenye umri wa miaka 27 aishie Dar es Salaam, alisema “Hata kupata KY [mafuta] ni changamoto, kwasababu ukienda dukani kuinunua, wanataka uwe umeandikiwa na daktari, na kama huna karatasi ya daktari, mara nyingi hawakuuzii.”[125]

Victor, mwanaume anayevutiwa kimapenzi na mwanaume mwenye umri wa miaka 25 aishie Dar es Salaam, alisema baadhi ya maduka ya dawa pia yanabagua kwa misingi ya muonekano wako wa kijinsia:

Kabla ya kupigwa marufuku kwa vilainishi, ningeweza kwenda na kuvipata katika vituo vya msaada na katika NGO zinazotoa huduma za afya kwa wana-LGBT. Lakini baada ya kupigwa marufuku, hakuna sehemu ambayo naweza kuvipata. Nyakati zingine naenda katika maduka ya dawa kununua tu KY lakini inakuwa kazi sana, kunakuwa na maswali mengi sana, na wanaouza hizo dawa hawatuungi mkono kwasababu ya muonekano wetu….. kama hatuonekani kama wanaume wanaovutiwa na wanawake, wanatuuliza ‘Kwanini unataka kutumia KY?’[126]

Victor hakufanikiwa kupata vilainishi katika hospitali za serikali, kitu ambacho analaumu kwamba kilitokana na maneno ya chuki ambayo Mkuu wa Mkoa Paul Makonda aliyasema:

Unapozungumzia chochote kinachohusiana na masuala ya LGBT, vilainishi, mipira ya kiume, ni ngumu sana katika hospitali za serikali. Kwasababu mkuu wetu wa mkoa anasema ‘Hatutaki kuwaona wana-LGBT.’ Nilijaribu mara nyingi sana kupata vilainishi lakini hawakunikubali. Wananiuliza, ‘Ya nini? Unaumwa?’ Nilijaribu Mwananyamala, Amana, na Hospitali ya Kibamba.[127]

Marufuku ya Vituo vya Msaada na Semina za Kijamii za Kujikinga na VVU

Utafiti wa aina yake wa Lancet wa Oktoba 2019 uligundua kwamba sheria kandamizi zinaendana na upimaji mdogo wa VVU na uelewa wa hali zao za VVU miongoni mwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume barani Afrika. Ilihitimisha kwamba, “Kupanuliwa kwa huduma za kijamii, pamoja na kuongezeka kwa msaada wa tiba na ushauri nasaha kutoka mashirika rafiki ya LGBT, itakuwa muhimu katika kuwashawishi wanaume wanaofanya ngono na wanaume wengi zaidi kupima na kupata tiba ya VVU.”[128] UNAIDS pia wamesisitiza kwamba jitihada za kijamii na zinazoongozwa na watu wa rika/ mwelekeo unaofanana ni moja ya njia bora za kuwafikia makundi ya wanyonge kwa elimu ya VVU.[129] Katika nchi ambazo mapenzi ya jinsia moja ni kosa la jinai, watoa huduma, hasa mashirika ya kijamii, lakini nyakati zingine NGO za kimataifa pia – zinaweza kupatwa na unyanyasaji kwa kutoa huduma za afya kwa wana-LGBT pia.[130] Lakini nchini Tanzania, serikali imepiga marufuku rasmi huduma hizo, ikiwanyima wana-LGBT haki ya kujikinga na pia kutibiwa VVU.

Miaka michache kabla ya msako, mashirika kadhaa yasiyo ya kiserikali, ya kitaifa na kimataifa, yalianzisha vituo vya misaada yakiwalenga makundi maalum kwa ajili ya huduma za VVU, kama njia mbadala wa hospitali za umma na kliniki ambako kuna ubaguzi wa hali ya juu. Vituo hivi vilitoa huduma za kupima VVU na ushauri nasaha kwa hiari, na taarifa zingine zihusuzo VVU, elimu ya ngono na afya ya uzazi. Zingine zilitumika pia kama mahali pa kuchukulia dawa za kupunguza makali ya VVU (anti-retroviral therapy (ART)). Vituo vingine vya msaada vilitoa huduma za afya ya akili na vingine hata vikaruhusu wanufaika wasiokuwa na uwezo kupata chakula na mahali pa kuoga.[131] Vituo vya misaada vikawa vyanzo vya jamii kwa wana-LGBT Tanzania, nyakati zingine hata kwa wanawake wanaovutiwa kimapenzi na wanawake na wale ambao wanavutiwa kimapenzi na jinsia zote ambao hawakuwa walengwa wakubwa wa huduma za VVU vituo hivi vilifanyika kuwa sehemu salama kwao kwa huduma za afya, mikutano, na hata kupiga soga tu na rafiki zao.  [132] Wafanyakazi walikuwa wamefundishwa juu ya mahitaji ya kiafya ya wana-LGBT na makundi maalum na hawakuwa wabaguzi.

Hata hivyo, baada ya marufuku ile ya mwezi Julai 2016  juu ya usambazaji wa vilainishi, serikali ilipiga marufuku pia semina za VVU kwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume zilizokuwa zikifanywa na mashirika ya kijamii. Mwezi Oktoba, wizara ilitoa tamko ambalo lilifunga rasmi shughuli zote za mashirika ya asasi za kiraia ambayo yalikuwa yakifanya huduma za muhimu, kazi zilizookoa Maisha za kuwaelimisha wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wengine kuhusu namna ya kujikinga na kupata tiba za VVU.[133] Tamko hilo lilisimamisha pia vituo vyote vya msaada vilivyokuwa vikiwalenga wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume:

Progamu za vituo vya afya vya KP zitaendelea kutekelezwa kwa wamakundi yote maalum na makundi yaliyohatarini. Hata hivyo, shughuli za semina za kijamii kwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume katika vituo vya msaada vitasubiri uandaaji wa huduma kamili za VVU na zinazofanana ndani ya jamii.[134]

Vituo vingi kati ya vile vilivyoathirika vilikuwa sehemu ya Mradi wa Sauti, mradi unaofadhiliwa na PEPFAR unaolenga kupunguza maambukizi ya VVU miongoni mwa makundi ya wanyonge, ukitekelezwa na USAID na kusimamiwa moja kwa moja na shirika la kimataifa lisilo la kifaida JHPIEGO, linalohusiana na Chuo Kikuu cha John Hopkins. JHPIEGO, moja ya watoaji wakubwa wa huduma za VVU kwa makundi maalum nchini Tanzania, ikasimamisha huduma zake mara moja zilizokuwa zikiwalenga wanaume wanaofanya ngono na wanaume.[135] Mashirika ya kijamii pia yaliathirika. Toni, mwanamke asiye na jinsia ya asili anayefanya kazi na shirika linalotoa huduma za VVU kwa wanawake na wanaume wasio na jinsia za asili na wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume, aliiambia Huma Rights Watch kwamba “Haiwezekani tena kwetu sisi kufanya kazi sasa hivi. Kimsingi unakuwa umekaririwa.” Aliongeza “Tulikuwa na mkutano na (maofisa wa afya wa serikali) na wakasema hawataki kusikia chochote kuhusiana na masuala ya LGBT. Walidai kwamba tunaajiri.”[136]

Makame, mwanaharakati asiye na jinsia ya asili, alielezea kazi ambayo shirika lake ilikuwa inafanya kabla ya marufuku na namna gani imezuiwa:

Kabla, tulikuwa na programu ya kutoka nje ambapo tunawatafuta watu waliobadilisha jinsia halafu tunawapeleka katika kituo cha afya ambapo wanapata huduma bure za matibabu ya kansa ya kizazi, na matibabu ya VVU, na matibabu ya magonjwa mengine ya zinaa kama vile kaswende. Tulitoa sana elimu juu ya kujikinga na matibabu ya VVU na pia kutoa ushauri kwa watu waliobadilisha jinsia. Hospitali Rafiki tulizokuwa tukitumia zote zilikuwa zinaungwa mkono na serikali – serikali ilijua kile tulichokuwa tukikifanya. Programu ilisimamishwa na mambo yakabadilika. Palikuwa na poromoko kubwa la watu walioacha kutumia ARVs. Mazingira hayakuwa rafiki, hatukuwa na cha kufanya. Wafadhili wote pia walisimama kwa muda, wakiangalia hali inakwendaje, ikiwa walikuwa tayari kuendelea ama la.[137]

Wanaume wengi wanaovutiwa kimapenzi na wanaume walisema walikuwa wanategemea sana semina za kijamii kama chanzo cha kwanza cha taarifa za afya. King alielezea aina za faida alizozipata kutoka semina na kijamii:

Nilikuwa na uwezo wa kupata elimu juu ya masuala yahusuyo VVU na magonjwa ya zinaa na matumizi sahihi ya ARV, ulaji wa mlo bora, na mambo mengine yahusuyo afya, na nilikuwa naweza pia kuwaelimisha wengine ambao hawakuwa na nafasi ya kushiriki katika shughuli kama hizo. Lakini sasa, hii haifanyiki tena.[138]

Amy, mtu asiyependa kujitambulisha na jinsia yoyote, alisema kupitia semina zile, “Nilifaidika na mengi maana niliweza kujifunza maswala ya elimu ya stadi za maisha ambayo iliniwezesha kujitambua mwenyewe na thamani yangu, pia kupata elimu ya maswala ya VVU, na magonjwa ya zinaa.”[139] aliongeza:

Serikali ya Tanzania ilitakiwa ikae na mashirika na baadhi ya wawakilishi wa jamii yetu na kusikiliza maoni yetu kabla ya kuamua kuyafungia mashirika yanayofanya shughuli za kupunguza maambukizi ya VVU kwa jamii ya LGBT, Pia inatakiwa ijue kuwa sisi ni miongoni mwa jamii ya watanzania, si haki kabisa Kutuondolea haki yetu ya kupata huduma rafiki, maana kukosekana kwa mashirika hayo ni changamoto kubwa sana kwa jamii yetu maana itasababisha kuongezeka kwa maambukizi ya VVU na magonjwa ya ngono miongoni mwetu.

Mwezi Februari 2017, Wizara ya Afya ilienda mbali zaidi, ikiamuru vituo vya msaada takribani 40 vinavyowahudumia makundi maalum na yaliyo hatarini (sio tu wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume), 18 kati ya hivyo vilikuwa vikiendeshwana JHPIEGO, kufunga huduma zao. Waziri wa Afya Mwalimu alidai “uchunguzi maalum” uliofanywa na Wizara ya Katiba na Sheria ulibaini kwamba “mbali na kujihusisha na shughuli za VVU na UKIMWI, baadhi ya washiriki wa utekelezaji wa miradi hiyo walikuwa wanahamasisha ushoga, kinyume na sheria za nchi.” Hivyo akaagiza: “Matumizi ya ‘Vituo vya Msaada’ kwa kutoa huduma za afya na VVU kwa makundi maalum na yaliyopo hatarini havitaruhusiwa tena.”[140]

Wana-LGBT walihojiwa na Human Rights Watch waliathirika sana na kufungwa kwa vituo vya msaada. Ronnie, mwanaume asiye na jinsia ya asili mwenye umri wa miaka 28, alijiskia kwamba wana-LGBT walikuwa wanatengwa kwa namna ya pekee. “Kuna huduma za wasioona, viziwi, lakini wanayaacha makundi mengine nyuma.”[141]

Victor, mwanaume anayevutiwa kimapenzi na mwanaume, mwenye umri wa miaka 25 ambaye ana virusi vya Ukimwi, alisema kwamba vituo vya msaada vilimpatia huduma za kutosha zaidi ya hospitali za serikali:

Vituo vya msaada ni mahali ambapo wanatuelewa zaidi. Ikiwa una ugonjwa, ni rahisi. Daktari anakuelewa….. ikiwa una virusi vya ukimwi unaweza kupata elimu ya lishe, elimu ya ustahimilivu. Unadhani katika hospitali za serikali tunaweza kupata dakika tano za kuongea na daktari kuhusu ustahimilivu? Wamepiga marufuku vituo vyote vya msaada, hivyo kwakweli tunakufa.[142]

Makame, mwanaume asiye na jinsia ya asili, alisema madaktari katika vituo vya msaada walikuwa na uelewa juu ya utofauti wa jinsia. Hakupata tabu ya kunyanyasika akielezea kila mara jinsia yake mpya.

Unapata huduma rafiki. Unakuwa huru zaidi kuzungumza na daktari. Unazungukwa na watu wanaojua wewe ni nani hasa, badala ya kuhangaika kwenda na kuelezea watu wewe ni nani hasa.[143]

Kwa Leticia, mwanamke anayavutiwa kwa wanawake wenzao, ilikuwa wazi kwake kwamba ili kuyafikia makundi maalum, mbadala wa hospitali za serikali ulikuwa ni lazima:

Baadhi ya watu hawajisikii kwenda katika vituo vya afya vya serikali. Hili limekuwa tatizo kwa miaka mingi. Sasa kwanini tunavipoteza vituo vyetu vya msaada ambavyo tulidhani vilikuwa rafiki, na kulazimishwa kwenda kwa vile vinavyoendeshwa na serikali?[144]

Jephter, mwanaume anayevutiwa kimapenzi na mwanaume, aliwaelezea watumishi katika kituo cha afya kama “watu wazuri sana”[145] Kinyume chake, Japhet alikuwa anaogopa sana kwenda katika hospitali za serikali kiasi ambacho hajawahi kwenda kwenye hospitali ya serikali hata moja, hata kama ana virusi vya Ukimwi, kwasababu anaamini atafanyiwa unyanyapaa.

Vituo vya msaada vilikuwa vinatoa rufaa kwa wahudumu wengine wa afya walio rafiki kwa wana-LGBT kwa masuala ya afya ambayo hawakuwa na uwezo wa kuyashughulikia wenyewe. Medard, mwanaume anayevutiwa kimapenzia na mwanaume, mwenye umri wa miaka 38, anakumbuka:

Kila nilipokuwa na tatizo la kiafya, niliweza kwenda kwenye vituo hivyo kupata msaada au kuunganishwa na mtoa huduma ambaye hakuwa mbaguzi, ambaye alinihudumia kama watu wengine. Siku hizi, hata kama nina tatizo la kiafya, sina mahali pa kwenda ambapo naweza kulielezea tatizo langu, hivyo nanyamaza tu [na kukwepa kupata huduma].[146]

Medard alimalizia kwa kusema, “Ningependa serikali ya Tanzania kuwaruhusu kuchu (wana-LGBT) kupata huduma za afya. Ikiwa hatupati huduma, tutakufa.”[147]

Ahmed, 39, alisema hata kama alijua kwamba baadhi ya mashirika yaliendelea kutoa elimu ya VVU kwa wanaume wanaofanya mapenzia na wanaume kwa kificho, alikuwa anaogopa kwenda kupata huduma hizo kwasababu za hatari ya kukamatwa. “Kuna watu kadhaa ambao wamekamatwa kwasababu walikuwa wanakusanyika pamoja, kupata elimu ya masuala ya VVU na vitu kama hivyo. Hivyo naogopa kwenda kwa hilo, kwasababu naweza kukamatwa pia.”[148]

Unyanyapaa na Ubaguzi katika Vituo vya Afya vya Serikali

Waziri wa Afya Ummy Mwalimu, katika tamko lake la Februari 2017 kupiga marufuku vituo vya msaada rafiki kwa wana-LGBT kwa huduma za VVU, lilitaka wana-LGBT waende kupata huduma katika hospitali na kliniki za serikali. Aliagiza pia vituo vyote vya afya “kuhakikishika kwamba huduma za afya na VVU zinatolewa kwa watu wote pasipo ubaguzi wa aina yoyote.”[149] Naam, chini ya sheria yenyewe ya Tanzania ya mwaka 2008 ya Kuzuia na Kudhibiti VVU, wahudumu wa afya wanaowahudumia watu waishio na VVU lazima watoe huduma “pasipo ubaguzi wala unyanyapaa wa aina yoyote.”[150]

Kwa mujibu wa waraka wa Februari 2017 wa Wizara ya Afya, ikiwa mtu yeyote kutoka kundi maalum na walio hatarini atafanyiwa ubaguzi katika kituo cha afya cha serikali, “anapaswa kutoa taarifa kwa Mganga Mkuu wa Wilaya (DMO), au kwa Mganga Mkuu wa Mkoa wa Wilaya au Mkoa huo, na kama ni lazima aende hata Wizara ya Afya, kupitia kitengo cha Mawasiliano.”[151] Hakuna yeyote kati ya waliohojiwa na Human Rights Watch ambaye amewahi kupeleka malalamiko yake katika ofisi yoyote ya serikali. Kuwa kosa la jinai na kuchanganya na unyanyasaji kumetengeneza vikwazo kwa mtu kujitokeza rasmi kuwa ni LGBT katika ofisi ya serikali ili kushtaki ubaguzi aliofanyiwa.

Pamoja na kutokuwepo kwa taarifa, ubaguzi katika sekta ya afya ni wa hali ya juu, kama ulivyoelezwa kwa kina hapa chini. Human Rights Watch na WASO walinukuu visa vingi vya ubaguzi katika utoaji wa huduma za afya mwaka 2013.[152] Wanaharakati kadhaa wa LGBT waliiambia Human Rights Watch kwamba kati ya mwaka 2013 na 2016 walikuwa katika ushirikiano kati ya mashirika ya afya ya serikali na NGO za kimataifa zililenga kuwakumbusha/kuwasisitiza wanataaluma ya afya  juu ya haki na mahitaji ya kiafya ya makundi maalum. Inawezekana kwamba programu kama hizo ziliboresha namna wanataaluma ya afya walivyokuwa wakiwahudumia wana-LGBT, lakini hata hivyo walikosa nguvu na fursa ya kwenda kwa kina katika kuibua mabadiliko muhimu katika fikra za kibaguzi ndani ya muda mfupi.

Osman, mwanaume anayevutiwa kimapenzi na wanaume, mwenye umri wa miaka 24 na muathirika wa VVU, alisema Oktoba 2017 mfanyakazi wa afya katika hospitali ya serikali, Sinza Palestina, ambapo alikuwa akienda kupata matibabu ya VVU, alimwambia,”Wewe ni kijana mzuri, kwanini unafanya mapenzi na makuchu? Ndio maana umepata UKIMWI, kwasababu vitendo hivyo vinamkasirisha Mungu.” Osman aliongeza, “Waliniambia pia kuacha hii michezo na kuokoka, kumfukuza Shetani, ambaye ananifanya kufanya mapenzi na makuchu, na kupata mke, kuoa na kuwa na familia.”  Kila mara aliporudi katika hospitali hiyo, aliendelea kupata unyanyasaji, hadi alipoondoka na kupata NGO, Pasada, ambayo iliyokuwa ikitoa huduma hizo kirafiki. Osman alisema kuna wakati, kabla ya kupata Pasada, aliacha kutafuta huduma kabisa. “Sikutaka kurudi tena katika hospitali ile [Sinza Palestina] kwasababu ya ukatili wao.” [153]

Suleiman, mwanaume anayevutiwa kimapenzi na wanaume, mwenye umri wa miaka 25 aishie Dar es Salaam, alienda hospitali ya Mwananyamala mwezi Septemba 2018 kupima VVU. Alielezea hivi kilichompata pale:

Hawakupenda nilipowaambia kuwa mimi navutiwa kimapenzi na wanaume wenzangu. Walikuwa wakinitukana, mtu wa mapokezi, daktari na nesi, wote. Niliwaambia mimi navutiwa na wanaume kwasababu nilihitaji kuwa wazi kwao. Wakaniambia kwamba nitafute hospitali nyingine kuhudumia afya yangu, na sio hospitali hiyo, lakini walinipa majibu na sikuwa na VVU. Walikuwa wakitumia lugha mbaya – ‘Kama wewe ni mwanaume unayevutiwa na wanaume wenzako, siku nyingine usije katika hospitali hii, kwasababu hatutibu watu kama wa aina yako.’ Walisema haya mbele ya watu wengine. Nilijisikia vibaya. Nilinyamaza tu na kuchukua vitu vyangu na kwenda nyumbani.[154]

Victor, mwanaume anayevutiwa kimapenzi na wanaume, alisema alikwenda hospitali ya Mwananyamala waka 2018 akiwa na dalili ambazo alidhani ni za kaswende ya njia ya haja kubwa, daktari akamkaripia, “Kwanini unafanya hivi?” na kumuita “muovu.” Akihofia kwamba watu wengine waliokuwepo karibu wangesikia na kumshambulia, Victor aliondoka kwa daktari huyo na kwenda kutafuta dawa mwenyewe katika duka la dawa.[155]

Leila, mwanamke asiye na jinsia ya asili, aliiambia Human Rights Watch kwamba mwaka 2016 mtoa huduma katika hospitali ya Mwananyamala alimwambia, “Matendo yako hayampendezi Mungu.” Mtoa huduma huyo, ambaye alimuona kama ni mwanaume anayevutika na wanaume wenzake, alimwambia aoe, awe na watoto, na kuwa na heshima kwa familia na jamii yake. Katika tukio lingine, Leila alisema, katika Hospitali ya Mwananyamala, “Jopo la madaktari waliitwa kuja kunishangaa kwa kuwa kuchu [m-LGBT].”[156]

Ronnie, mwanaume asiye na jinsia ya asili, mwenye umri wa miaka 28, alisema,wauguzi katika Hospitali ya Mwananyamala walimuuliza swali la kiunyanyapaa kuhusu muonekano wake wa kijinsia:

[Ukienda katika hospitali za serikali, wanakuwa na maswali mengi sana, baadhi yao wanakuangalia halafu wanaanza kucheka. Wanaweza wakaanza kukuuliza maswali ya kipuuzi. Wewe ni mvulana au msichana? Kwanini unavaa nguo hizi/kama hizi? Wauguzi waliniuliza hivyo pale Hospitali ya Mwananyamala. Sikuwajibu kwamba mimi ni mwanaume nisiye na jinsia yangu ya asili. Nilikuwa na maswali kichwani: ‘Kama nikisema kwa wazi, wanaweza kuita polisi na kusema huyu anafanya hivi na vile.’ Na wengine, ukijibu kwamba wewe ni mwanaume usiye na jinsia ya asili, hakuna atakayekuelewa. Ukisema ‘nafanya hivi na vile,’ watakutukana tu. Hivyo sikuwahi kuwaambia – kamwe.[157]

Hassan, mwanamke asiye na jinsia ya asili kutoka Tanga, alithibitisha kwamba watu wasio na jinsia za asili wanakutana na changamoto fulani katika hospitali za serikali. “Ukiwaambia [jinsia yako] wanatuona kama tumechanganyikiwa, na nyakati zingine hata wanakunyima huduma. Kwahivyo unakwenda tu katika duka la dawa kununua dawa na kunywa.”[158]

Watu wengi tuliowahoji walisema hawakujisikia huru kuwa wawazi juu ya jinsia zao au mwelekeo wao wa kingono katika vituo vya afya vya serikali. Ethan, mwanaume asiye na jinsia ya asili, mwenye miaka 22, alikwenda kupata huduma katika hospitali za serikali lakini bila kuwa wazi kuhusu jinsia yake: “Nilikuwa naogopa kuwaambia kuhusu jinsia yangu, kwasababu nilijua watashtuka.”[159] Wagonjwa wasipozungumza kwa uwazi kwa wahudumu wao wa afya, ikiwa ni pamoja na mweleko wao kimapenzi au utambulisho wa jinsia zao, watoa huduma wanaweza wakashindwa kuwapa huduma katika kiwango wanachokihitaji.

Unyanyapaa na ubaguzi katika vituo vya afya vinaweza kusababisha wana-LGBT kutokutafuta matibabu kabisa. Abdi, mwanaume anayevutiwa kimapenzi na wanaume wenzake, mwenye umri wa miaka 22, alisema, “Nimekutana na unyanyapaa wa hali ya juu sana kiasi kwamba wakati mwingine nachukia kwenda kwenye hizo hospitali za serikali. Kwasababu unakwenda pale kupata huduma za afya, lakini badala yake, wauguzi na madaktari wanaanza kukuhudumia, kama vile, ‘Hicho unachokifanya sio kizuri, jaribu kuacha umrudie Mungu wako,” au wakati mwingine, ‘Ni mapepo ndio yanakufanya upende hiki, unahitaji kwenda kanisani na kusali.”[160] Abdi anasema mara nyingi aliamua kutokwenda kutafuta huduma badala ya kuvumilia matibabu ya kibaguzi.

Stanley, mwanaume asiye na jinsia ya asili mwenye umri wa miaka 28, alisema amekuwa akiogopa kutafuta huduma katika vituo vya afya vya serikali tangu alipokwenda kufanyiwa upasuaji wa kifua kuondoa matiti nje ya nchi. “Nilijua wangeninyanyapaa, kwasababu wahudumu wengi wa afya wa serikali hawaelewi masuala ya watu waliobadili jinsia.”[161] Kutokuwepo kwa vituo vya afya vilivyo na wafanyakazi waliopitia mafunzo maalum juu ya utambulisho wa kijinsia, hakujua mtoa huduma mwingine yeyote yule ambapo angekuwa na uhakika wa kuhudumiwa kwa staha.

Kufungwa kwa vituo vya msaada rafiki kwa wana-LGBT na ubaguzi katika hospitali za serikali maana yake ni kwamba baadhi ya wana-LGBT wanatafuta huduma za afya katika hospitali binafsi maalum ambazo zinafahamika kuwa rafiki zaidi. Lakini kwa wengi wao, huduma hizo hazipo tena. Victor, mwanaume anayevutiwa kimapenzi na mwanaume mwenzake aliyesema kwamba alikuwa anafanya biashara ya ngono, aliiambia Huma Rights Watch: “Nimewahi kufanya ngono na madaktari mara mbili ili nipate huduma – na madaktari wawili tofauti. Hivi ndivyo naweza kulipa. Sina pesa ya kuwalipa. Hivyo wakiniomba nifanye nao mapenzi, inabidi niseme ndio.”[162]

Upatikanaji Mdogo wa Tiba za Kufubaza Virusi Vya UKIMWI

Upatikanaji wa huduma za VVU zilizo rafiki, bila kuhukumiwa ni suala la kufa na kupona, kama lilivyogusiwa na wahojiwa kadhaa hapo awali. Moja kati ya kitu cha kusikitisha sana ambacho Human Rights Watch ilikisikia kutoka kwa wanaharakati wa LGBT na maofisa wa UNAIDS ni kwamba katika nyakati tofauti kati ya mwaka 2016 na 2018, udhalilishaji wa wazi kwa wana-LGBT na ukosefu wa sehemu salama wa kupata matibabu ilimaanisha kwamba watu wenye VVU waliacha kupata matibabu. Baadhi ya wale walioacha kupata matibabu ya kufubaza virusi vya UKIMWI walikufa, hata hivyo Human Rights Watch haikuweza kuthibitisha kwamba vifo hivyo vilitokana na kutokuweza kupata matibabu.

Shirika la Afya Duniani linashauri kwamba kila anayeishi na VVU apatiwe matibabu ya kufubaza virusi vya UKIMWI, bila kujali idadi ya CD4  (aina ya seli nyeupe za damu), na Tanzania inazingatia miongozi hii, ikitoa huduma za bure za matibabu ya kufubaza virusi vya UKIMWI. Kwa mujibu wa makadirio ya UNAIDS, asilimia 72 ya watu wazima wanaoishi na VVU nchini Tanzania walikuwa wakipata matibabu ya kufubaza VVU mwaka 2018, ikionyesha maendeleo makubwa ukilinganisha na muongo mmoja uliopita, hata kama Tanzania ilibaki nyuma kutoka maono ya UNAIDS ya kufikia asilimia 90 ya matibabu ifikapo mwaka 2020.[163]

Utaratibu wa kwanza wa kawaida wa matibabu nchini Tanzania inahusisha kunywa vidonge vitatu mara moja kwa siku.[164] Wengi wa watu wanaoishi na VVU wanapata matibabu yao mara moja kwa mwezi, ambapo wanaweza kuchukua dawa zao katika maduka ya dawa na kliniki maalum. Utumiaji wa bila kukosa wa ART ni muhimu katika kufubaza VVU, afya ya watu wanaoishi na VVU, na kuzuia uambukizaji na kushindwa kwa matibabu.[165]

Human Rights Watch iliwahoji wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wanaoishi na VVU ambao bado wanaendelea kupata matibabu ya kufubaza virusi vya UKIMWI (anti-retroviral therapy, ART) kwa muda wote wa msako pasipokuwa na vikwazo. Lakini Victor, anayeishi na VVU mwenye umri wa miaka 25, alisema:

Kuna wakati sikwenda kuchukua ARV zangu. Kwasasa ni shwari, lakini wakati wa masuala ya kisiasa, au wakati wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wenzao wanashambuliwa, siendi. Hivyo nampigia simu daktari wangu, namwambia nitampa pesa ya soda, halafu tunaweza kukutana baa anapomaliza kazi yake na hivyo ndivyo navyozipata. Lakini kama tungekuwa na kituo cha msaada, tusingekuwa na tatizo hili.[166]

Makame, mwanahaharakati asiye na jinsia ya asili, alisema kwamba kwasababu ya kauli za kichochezi kutoka kwa maofisa wa serikali,

Watu wengi wasio na jinsia za asili waliotakiwa kupata dawa walisimama. Walikuwa wanatarajia vurugu katika maeneo yao. Watu wasio na jinsia zao za asili wanajulikana kirahisi, wanaonekana kuwa tofauti, kwahivyo kwao walikuwa wanaogopa sana. Waliokuwa na pesa walikuwa wanazituma kwa daktari kuja na kuwatibu nyumbani kwao, lakini wengine hawakupata matibabu kabisa. Kwasasa, tunajaribu kuwapigia simu na kuwafatilia wale tuliokuwa tunawapa rufaa, na wengine wameanza kuja kupata matibabu. Lakini sasa hawawezi kwenda kwenye vituo vya msaada vilivyopigwa marufuku, kwahivyo tunajaribu kutafuta sehemu nyingine na kuzifanya rafiki.[167]

Leticia, mwanaharakati ambaye ni mwanamke anayevutiwa na wanawake wenzao, aliiambia Human Rights Watch katika mahojiano ya Oktoba 2018:

Katika kipindi kifupi cha tangu kufungwa kwa vituo vya msaada, naweza kutaja watu watano waliofariki. Hawa walikuwa ni mifano ya kuigwa kutoka wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wenzao na sasa wamefariki. Afizi mwenyewe amepimwa na kukutwa na VVU kati ya mwaka 2005 au 2008. Lakini miezi miwili au mitatu baada ya vituo vya msaada kufungwa akasema hakuna faragha tena, na akaacha kwenda kuchukua dawa zake na kupata Kifua Kikuu na kufariki. Alifariki Juni [2018]. Kaoge, yule aliyefanya mahojiano na kuibua gumzo, alifariki [Novemba 2017]. Kaoge alisema, “Hakuna haja ya mimi kuishi, wacha niende.”
Awali, watu wote hawa walikuwa wanakunywa dawa zao. Walikuwa wanakuja katika vituo vya msaada kusalimia na kuchukua dawa zao. [Lakini] hatuna tena kituo cha msaada.[168]

Human Rights Watch iliwauliza wanaharakati wengine wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wenzao juu ya vifo vitokanavyo na VVU katika jamii. Mmoja alisema anawajua watu 15 waliokufa ndani ya miaka miwili baada ya msako ulioanza mwaka 2016, wakati mwingine alisema anawajua watu 17 waliokufa ndani ya miezi 18. Human Rights Watch hawakuweza kuthibitisha takwimu hizi.

Madhara ya Afya ya Akili ya Ukosefu wa Upatikanaji wa Huduma Zinazowajumuisha LGBT

Wahojiwa wawili walielezea msongo wa mawazo wanaoupata kutokana na msako wa chuki wa serikali dhidi ya wana-LGBT kuwa unasababisha matatizo ya afya ya akili wakati ule ule ambao vituo vya msaada vimefungwa, ambavyo baadhi yake vilikuwa na washauri marafiki kwa wana-LGBT uhaba wa sehemu salama kushughulikia hayo masuala. 

Toni, mwanaharakati, aliripoti msongo wa kisaikolojia baada ya kukwepa chupuchupu kukamatwa katika misako miwili ya polisi katika warsha za maswala ya afya na haki za binadamu. Alisema:

Ilibidi niende ku-Google kuelewa aina na msongo wa mawazo niliyokuwa nao. Nilikuwa najisikia kama kila kitu kinaanguka kama nyumba ya karata – kama vile mtu amezisukuma karata na fimbo na kila kitu kilikuwa kinaanguka. Sikuwa na muongozo wowote wa namna gani ya kupata msaada wa afya ya akili.[169]

Ronnie, mwanaume asiye na jinsia ya asili, pia alizungumzia madhara ya afya ya akili ambayo aliyapata yeye na wanaume wengine wasio na jinsia ya asili katika shirika lao kwasababu ya kutokuwa na uwezo wa kuelezea jinsia zao kwa uwazi:  

Nina bima ya afya na naweza kwenda katika kila hospitali, lakini siwezi kuwaambia kwamba sina jinsia ya asili – Nitawaambia kwamba mimi ni mwanamke na wananitibu. Lakini kuna madhara mengine mengi – masuala ya kisaikolojia kwa wanachama wetu. Hawawezi kusema wazi kile wanachowaza, kile walichonacho ndani. Watakuwa wananyamaza kimya. Hawawezi kusema wazi, “Nimeambukizwa na msichana mwenzangu,” Hivyo itakuwa inawatafuna ndani kwa ndani. Ni ngumu, ni ngumu, inauma, lakini huwezi kufanya chochote.[170]
 

III. Mashambulizi kwa Asasi za Kiraia za LGBT

Kwa mujibu wa katiba ya Tanzania, kila mtu ana haki ya “kukusanyika kwa uhuru na Amani, kukutana na kushirikiana na watu wengine, na kwa sababu hiyo, kueleza mawazo yake hadharani na kuunda na kujiunga na vyama na mashirika yaliyoundwa kwa madhumuni ya kutunza na kuendeleza imani yake au vitu vyovyote apendavyo.”[171] Lakini haki za kukusanyika na kujieleza zinashambuliwa nchini Tanzania. Wanachama na wanasiasa, vyombo vya habari, na asasi za kiraia wote wamekuwa wakishambuliwa.[172]

Katika muktadha huu wa kutokuvumilia uhuru wa kukusanyika na kujieleza, ikichanganywa na chuki ya kimfumo kwa wana-LGBT, haishangazi kwamba asasi za kiraia za LGBT zinashambuliwa. Tamko la Waziri wa Sheria Harrison Mwakyembe katika mkutano wa kikanda wa kiserikali Mbeya Julai 2016 kwamba angefanya kazi na Wizara ya Mambo ya Ndani kushitaki mashirika yoyote yaliyokuwa yanaunga mkono ushoga, ikiwa ni pamoja na yale yaliyokuwa yanasambaza vilainishi, ulikuwa ndio mwanzo wa mashambulizi dhidi ya mashirika yanayoshughulika na kuwezesha wana-LGBT kupata huduma za afya na haki.[173]

Kufutiwa Usajili na Vitisho vya Kufuta Usajili wa Mashirika Yasio ya Kiserikali

Mashirika ya Asasi za Kiraia nchini Tanzania lazima yajisajili kwa Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, ambayo yapo chini ya Wizara ya Afya, Maendelo ya Jamii, Wazee, Jinsia na Watoto. Lazima yatoe majina yao, maono yao, na nakala ya katiba yao.[174] Chini ya Sheria ya NGO ya 2002, cheti cha NGO kinaweza kusitishwa ikiwa shirika hilo litakiuka masharti yaliyowekwa katika cheti hicho au “kufanya kazi kinyume na katiba yake.”[175]

Agosti 1, 2016, Msajili wa NGO alitoa barua ikionyesha nia yake ya kutaka kulifutia usajili shirika la Community Health Education and Advocacy Services (CHESA), shirika la kijamii linaloshughulikia afya na haki za binadamu miongoni mwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wenzao na jumuia nzima ya LGBT kwa upana. CHESA inatafsiri maono yake kwamba “kutangaza ustawi wa afya na Haki za Binadamu ikiwa na lengo la kuhakikisha upatikanaji wa jumla wa huduma za afya, ikiwa ni pamoja na huduma za afya za awali, haki za huduma za afya za VVU na elimu ya uzazi.”[176] Miongoni mwa shughuli zake wakati huo, CHESA ilisambaza vilainishi kama sehemu ya Mradi wa Sauti, jitihada za shirika lisilo la kiserikali la afya ya jamii la Kimarekani JHPIEGO. Barua ya msajili iliitaka CHESA kujibu shutuma kwamba ilikuwa inatangaza ushoga.

Tarehe 15 Agosti, Naibu Waziri wa Afya Kigwangala anaongoza uvamizi katika ofisi za CHESA jijini Dar es Salaam, akiwa pamoja na askari polisi na maofisa usalama. Uvamizi huo, ulionukuliwa katika ukarasa wa Twitter wa Kigwangala, kidhahania unafanana na mbinu zinazotumiwa na Rais Magufuli, ambaye alikuwa anajulikana kwa kufanya ziara za bila taarifa katika ofisi za serikali ambazo alizihisi kuwa na rushwa au kutokuwa na maadili ya kazi ya kutosha.[177] Maofisa usalama walipekua ofisi, wakachukua ripoti mbalimbali, na kumuhoji mkurugenzi mkuu wa CHESA John Kashiha na wafanyakazi wengine kuhusu shutuma za kuhamasisha ushoga. Kigwangalla aliuliza maswali kuhusiana na ripoti kivuli ambayo CHESA na mashirika mengine ilikuwa imewasilisha katika Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa kama sehemu ya mchakato wa Mapitio ya Wazi ya Msimu (UPR process), na kuwanyang’anya nakala za ripoti hiyo. Polisi walimuita tena kituoni Kashiha siku iliyofuata kwa maswali zaidi na kumuhoji kwa takribani saa nane kuhusu kazi za CHESA kabla ya kumuachia.[178]

Tarehe 30 Agosti, CHESA ilifungua kesi ya kikatiba ikidai kwamba uvamizi ule ulikiuka uhuru wake wa kukutana na kuomba pingamizi dhidi ya juhudi zozote zile za kuwafutia usajili.[179] Kashiha aliiambia Human Rights Watch kwamba Mahakama Kuu iliunga mkono pingamizi, na CHESA waliweza kuendelea kufanya shughuli zao wakati kesi yake dhidi ya serikali ikiendelea.[180]

Lakini shirika hilo lilishambuliwa tena baada ya polisi kuvamia mkutano wake wa kisheria ambao CHESA iliuandaa ikishirikiana na shirika lenye makazi yake Afrika Kusini liitwalo Initiative for Strategic Litigation in Africa (ISLA) mwezi Oktoba 2017, ikiwakamata washiriki, kama ilivyoelezwa zaidi hapa chini. Mwezi Oktoba 20, Msajili wa NGO alitoa amri kusimamisha kazi za CHESA, kwa shutuma kwamba lilikuwa likihamasisha ndoa ya jinsia moja.[181]

Hatimaye, mwezi Aprili 2019, Msajili wa NGO akafuta cheti cha usajili kabisa cha CHESA, pamoja na vyeti vingine vya shirika la LGBT na moja ambalo linafanya kazi na wafanya biashara ya ngono wa kike. Msajili akayashitaki mashirika hayo kwa “kuhamasisha vitendo visivyo na maadili” na kukiuka “sheria, maadili na mila za Tanzania.”[182]

Kama CHESA ilivyosema katika nyaraka ambayo haikuchapishwa lakini walipewa Human Rights Watch, kutokana na kwamba wana-LGBT nchini Tanzania wana washirika wachache sana serikalini au katika asasi za kiraia kubwa ambao wako tayari kuchukua hatua kuzingatia haki zao, kushindwa kuhakikisha uhuru wa kukusanyika wa mashirika ya LGBT “unasababisha kushindwa kulinda haki za binadamu na uhuru wa wanachama wa mashirika haya. Ukizingatia hatari yao na chuki ya jamii dhidi yao, kuwanyima haki ya kukusanyika ni sawa na kuwanyima haki zao za binadamu kwa ujumla.”[183]

 

Uvamizi katika Mikutano na Warsha za Afya na Haki

Chini ya serikali ya Magufuli, polisi pande zote Tanzania bara na Zanzibar wameongeza matukio ya uvamizi wa mikutano binafsi, warsha na mafunzo yanayofanywa na mashirika ya LGBT na makundi mengine yanayoshughulikia afya na haki. Katika serikali zilizopita, wanaharakati wa LGBT waliweza kukutana pasipo kipingamizi chochote katika ofisi zao au katika hoteli karimu na kumbi nyinginezo.

Uvamizi wa kwanza wa aina hiyo ulifanyika Disemba 13 2016, wakati polisi walipoingilia mkutano wa mkakati wa makundi maalum katika hoteli jijini Dar es Salaam. Madhumuni ya mkutano, ulioitishwa na mashirika ya Kitanzania yanayoshughulikia udhibiti wa madhara na haki na afya ya wana-LGBT na wanaofanya biashara ya ngono, ilikuwa ni kujadili changamoto katika kutengeneza programu kwa makundi maalum ukizingatia msako unaofanywa na serikali ya Tanzania dhidi ya makundi manyonge. Polisi waliwakamata watu nane, ikiwa ni pamoja na waendesha mada. Waliachiwa siku hiyo hiyo pasipo mashitaka rasmi, lakini polisi waliendelea kushikilia vitambulisho vya washiriki na kuwataka kuripoti polisi kila siku.[184] Huko kuripoti polisi kwa kila siku ni sehemu ya unyanyasaji unaotumika mara kwa mara nchini Tanzania wakati polisi wanapokosa ushahidi wa kutosha kufungua mashtaka ya jinai rasmi.[185]

Stanley, mwanaume asiye na jinsia asili mwenye umri wa miaka 28, alikuwa mmoja wa washiriki waliokamatwa. Anakumbuka:

Tulikuwa washiriki kama 20 hivi na watoa mada wawili kutoka Kenya. Nakumbuka ilikuwa siku ya tatu, baada ya chakula cha mchana, ambapo mara polisi walivamia hoteli. Waliamuru wanaharakati wote wasimamishwe, na wakaanza kupekua chumba kimoja baada ya kingine, vyote hoteli nzima. Baadhi ya washiriki waliona kilichokuwa kinaendelea na kufanikiwa kukimbia au wakajidai kuwa ni wageni wa kawaida wa hoteli, lakini polisi walifanikiwa kutukamata kama watu nane hivi. Walitupeleka Kituo Kikuu cha Polisi. Halafu wakatushtaki kwa kuhamasisha masuala ya ushoga nchini Tanzania, kwa msaada wa wazungu….
Mwanasheria alikuja na kututoa, lakini kwa sharti la polisi kwamba tuwe tunarudi kuripoti kituoni kila siku. Kwa miezi miwili, tuliendelea kuripoti. Wakati huo waliendelea kuangalia simu zetu, wakipekuwa ofisi zetu na nyumbani kwetu na hotelini kwetu, kupata ushahidi wa kuunga mkono mashtaka yao, na hatimaye hawakupata ushahidi wowote na wakaamua kutuacha twende.[186]

Uvamizi mkubwa uliofuata wa mkutano uliohusiana na LGBT ulikuwa Septemba 2017, wakati polisi walipovamia mkutano ulioandaliwa na shirika, linalofanya kazi na wana-LGBT na wafanyabiashara ya ngono na familia, wenzi na marafiki zao juu ya kujikinga na VVU na haki za binadamu. Mkutano ulikuwa ukishughulikia uhusika wa mzazi katika kujikinga na VVU na msaada kwa wanafamilia wa mtu kutoka makundi yaliyo hatarini, na wengi wa watu 20 waliokamatwa na polisi walikuwa ni wazazi.

Abdulkarim, mshiriki, alijibu:

Tulikuwa katikati ya mafunzo kuhusu masuala ya afya. Polisi walikuja wakatukamata na wakatushutumu kwa kuwafundisha watu kuwa wanaovutiwa na watu wa jinsia zao na kuhamasisha mahusiano ya jinsia moja. [187]

Abdulkarim alisema polisi waliwashikilia kwa siku mbili kabla ya kuwaachia kwa dhamana. Ilibidi washiriki waendelee kuripoti kituo cha polisi kwa miezi minne hadi kesi yao ilipofutwa.[188]

Tarehe 17 Oktoba, 2017, wanasheria na wanaharakati wanaowakilisha shirika liitwalo Initiative for Strategic Litigation in Africa walitembelea Tanzania kukutana na wanachama wa CHESA na wanaharakati wengine wa LGBT kujadili uwezekano wa kutengeneza mashitaka aidha katika mahakama za ki-Tanzania au zile za kanda juu ya sera za afya za serikali zilizokuwa zikiwanyima haki ya afya wana-LGBT.

Amy, mshiriki aliyeponea chupuchupu kukamatwa, anaelezea kilichotokea:

Tulikuwa katika mkutano uliokuwa umeandaliwa na CHESA katika hoteli moja mjini, tukiwa katika mapumziko mafupi, ambapo mara tukaona mtu akiturekodi kupitia simu yake ya mkononi…. Tukaanza kujiuliza maswali, huyu ni nani, kwanini anaturekodi. Tukaamua kusimamisha mkutano…. Tulikuwa tunapata chakula cha mchana mara mfanyakazi wa hoteli akaja kutujulisha kwamba polisi wapatao tisa walikuwa wamevamia chumba cha mkutano na kumkamata John Kashiha na mmoja wa watoa mada aliyeitwa Sibongile..… Mwenzangu mmoja na mimi tukakimbia kwenda kujificha chooni na tukakaa huko tangu saa saba mchana hadi kumi na mbili jioni. Halafu tukaamua kutoka, na mtumishi mmoja wa hoteli akaja kutuambia kwamba mwenzetu mmoja alikuwa amekamatwa na akapelekwa Kituo Kikuu cha Polisi.[189]

Sibongile Ndashe, mwanasheria maarufu wa Afrika Kusini na mkurugenzi wa ISLA, aliiambia Human Rights Watch, “Waliokuja kutukamata walikuja wakiwa na dokezo na ajenda ya mkutano wetu. Aidha kundi letu lilikuwa limeingiliwa na mmoja wa wana usalama au kuna mtu miongoni mwetu aliyewatumia taarifa hizo.” Katika kituo cha polisi alisema:

Hakuweza hata kutaja kosa letu. Nilikuwa nawaambia ‘Mnasema tumevunja sheria, shtaka ni nini? Mnasema tunahamasisha ushoga, nini vigezo vya kosa hilo?’…. Nilimpigia simu Balozi wa Afrika Kusini nchini na mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu waje kituo cha polisi. Baada ya hapo, polisi hata hawakuwa na haja na sisi tena na walijua kwamba wanahitaji kutuachia huru sasa, lakini walifanya haya mambo ya kipuuzi ya kuchukua alama za vidole vyetu, kupiga picha. Katika fomu za dhamana waliandika --’ (mkato) badala ya mashitaka. Tuliachiwa kwa wakili wetu na tukaambiwa turudi siku iliyofuata.[190]

Lakini hata polisi ambao mwanzoni walikuwa wamebeba mashitaka yetu walionekana kukata tamaa ya kuendelea na mashitaka, baadhi ya polisi walionekana kutaka kuchunguza zaidi. Kesi ikahamishiwa zoni nyingine, Ndashe alisema. Oktoba 20, polisi waliwachukua washiriki 12 na kuwarudisha ndani, wakiwashikilia  katika Kituo Kikuu cha Polisi. Kamanda wa Polisi wa Dar es Salaam Lazaro Mambosasa alienda mahakamani mara mbili siku zilizofuata, Oktoba 23 na 24, akitafuta ruhusa ya kufanya vipimo vya njia ya haja kubwa kwa wanasheria na wanaharakati ili kupata ushahidi wa vitendo vya ushoga. Hakimu aliyakataa maombi yake.[191]

Oktoba 26, polisi waliwaachia wafungwa 12 kwa dhamana. Siku iliyofuata, polisi ilimchukua Ndashe na wenzake Waafrika Kusini na Uganda kwenda uhamiaji kwaajili ya kuondolewa nchini. Ndashe anakumbuka kwamba ofisa wa uhamiaji alikataa kuwaondoa nchini pasipo sababu, akimtaka polisi kurudi na amri ya kuondoshwa nchini. Ndashe anaeleza, “Katika hati ya kuondoshwa nchini, ilikuwa imeandikwa ‘kuhamasisha ushoga.””[192] ISLA ina mpango wa kupinga kile inachokiita kuwa ni uondoshwaji nchini kinyume na sheria katika Mahakama Kuu ya Tanzania.

Washiriki wa Kitanzania walitakiwa kuripoti polisi kwa siku kadhaa hadi pale polisi walipowaambia kwamba hawakuhitajika kuendelea kuripoti tena. Haijulikani kama kuna kesi yoyote ambayo bado iko wazi.[193]

Leticia, mwanamke anayevutiwa kwa wanawake wenzao alikamatwa katika mkutano huo, anaelezea jinsi gani kukamatwa kwao kulivyokuwa kusiko na maana: “Wala hatukuwa tunazungumzia jinsia zetu katika mkutano huo. Tulikuwa tunazungumzia tu unapotaka kufungua kesi na unaona haki zako zimekiukwa, unafuatiliaje”[194]

Makame, mwanaume asiye na jinsia ya asili aliyekamatwa katika uvamizi, ukamatwaji umekuwa na madhara ya kudumu:

Kukamatwa kwetu kuligonga vichwa vya habari, kwahivyo tulipotoka, watu wengi walitujua sisi ni kina nani. Kwahivyo kurudi nyumbani kwetu na katika maeneo yetu, maisha yalikuwa magumu sana. Baadhi yetu ilibidi tuhamie nyumba zingine. Baadhi yetu ambao walikuwa wanaishi na wazazi wao walifukuzwa. Nilikuwa Napata wageni, watu ambao hata sikuwajua walikuwa wanakuja nyumbani kwangu na kuuliza maswali. Hivyo ilibidi nihame.[195]

IV. Ukamataji Holela na Upimaji wa Nguvu wa Njia ya Haja Kubwa

Ukandamizaji wa haki ya afya unaofanywa na serikali ya Tanzania unafanyika katika muktadha mkubwa wa unyanyasaji dhidi ya wana-LGBT, ikiwa ni pamoja na ukamatwaji wa Watanzania wa kawaida kwa misingi ya kile kinachodhaniwa kuwa utambulisho wao wa mwelekeo wa kingono au kijinsia. Ukamataji Tanzania bara unafanyika chini ya kifungu cha 154 cha Sheria ya Makosa ya Jinai ya Tanzania ambayo hufanya jinai “kumuingilia mtu yeyote kinyume cha maumbile” ikiwa na kifungo cha hadi maisha jela; kifungu cha 157, kinachofanya jinai “matendo ya aibu baina ya wanaume” na kifungu cha 138A, juu ya “maonesho machafu yasiyofaa baina ya watu wawili.”[196] Zanzibar, sheria inazuia “matendo ya wanawake kuingilia wanawake” pamoja na vitendo vichafu vya makosa ya kuingiliana kinyume na maumbile.[197]

Ukamataji kwa misingi ya kudhani utambulisho wa mtu wa mwelekeo wake wa kingono au utambulisho wa kijinsia kunaweza kutafsiriwa kama ukamataji holela na ukiukwaji wa haki. Lakini inachangia pia katika kufanya mazingira ya tabia ya kutafuta msaada wa kiafya kuharibiwa. Victor, mwanaume anayevutiwa kimapenzi na wanaume wengine, mwenye umri wa miaka 25 anayeishi na VVU, alielezea njia mojawapo ambapo hofu ya kukamatwa inaingilia upatikanaji wa huduma ya afya:  

Rafiki yangu mtu anayefanya ngono na wanaume wenzake. Alikamatwa [kwasababu ambazo haziendani na mwelekeo wake wa kingono] na akawekwa chini ya ulinzi wa polisi, lakini ilichukua mwezi mzima kumpatia vidonge vya kufubaza virusi vya UKIMWI (ARVs). Bado yupo mikononi mwa polisi. Kama wanaharakati tunajadiliana nani anayeweza kwenda kumpelekea huyo mtu vidonge vyake. Kila mtu anasema ‘Nikienda polisi, watanikamata mimi pia.’ Kwahivyo nikajitolea na kwenda, lakini polisi wakawa wananiuliza kila siku, ‘Wewe ni nani? Unamjuaje huyu? Unatokea kwenye NGO? Upo na hao mashoga? Polisi walimtambua kama mwanaume anayefanya mapenzi na wanaume wengine. Ndio maana wana-LGBT wanaogopa kwenda pale na kumpatia vidonge vyake. Watauliza, “Wewe ni nani? Ukisema, Ni rafiki yangu, watauliza, Nyie ni marafiki kiasi gani? Wewe ni shoga?’[198]

Human Rights Watch na shirika la Wake Up and Step Forward Network (WASO) liliripoti mwaka 2013 juu ya zaidi ya visa 12 kati ya mwaka 2007 na 2012 ambapo polisi waliwakamata wana-LGBT kwa misingi ya kuwashutumu kwa vitu kama “kutembea kama mwanamke,” kutembea na mpenzi wa jinsia moja, au kuishi na mwenza wa jinsia moja. Katika kisa kimoja, ofisa mmoja aliamuru kukamatwa kwa mvulana anayevutiwa kimapenzi na wanaume baada ya kujaribu kuratibu semina juu ya masuala ya afya kwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wengine. Katika visa mbalimbali, polisi waliwatesa au kuwanyanyasa kingono watu waliowashutumu kuwa ni LGBT. Hakuna kesi hata moja kati ya hizi, zilizopelekea ufunguliwaji wa mashitaka. Mara nyingi polisi huwaachia watu baada ya kupokea rushwa, au baada ya kuwashikilia kwa siku kadhaa wakiwa hawana Ushahidi wowote dhidi yao. [199]

Hilo limebadilika lakini, chini ya serikali ya Magufuli. Polisi wanaonekana kuwa na bidii zaidi katika kutafuta ushahidi dhidi ya watu wanaoshutumiwa kuwa LGBT, ikiwa ni pamoja na kuwafanyia vipimo vya nguvu vya njia ya haja kubwa. Watuhumiwa kadhaa walishikiliwa kwa muda mrefu zaidi ya siku kadhaa, na wengine walipelekwa mahakani. Ukamatwaji wa watu wanaoshukiwa kuwa ni LGBT si njia rahisi tena kwa polisi wasiowaaminifu kujipatia rushwa, lakini ni sehemu ya kampeni hasi kubwa dhidi ya wana-LGBT Tanzania.

Ukamatwaji Unaoambatana na Vipimo vya Nguvu vya Njia ya Haja Kubwa

Upimwaji wa nguvu wa njia ya haja kubwa ni aina ya ukatili, isiyo ya kibinadamu na kufanya kitendo hicho nyakati zingine kuwa katika kiwango cha mateso, kama ilivyojadiliwa katika Sehemu ya VI hapa chini. Katika miaka ya hivi karibuni, nchi kama Lebanoni, Kenya na Tunisia wamechukua hatua kupiga marufuku vitendo hivyo vya upimaji wa nguvu wa njia ya haja kubwa kuwa kama ni udhalilishaji. Lakini Tanzania kwa upande mwingine, umevirasimisha vitendo hivyo.

Disemba 2016, katika kipindi cha siku saba, polisi visiwani Zanzibar waliwakamata wanaume wapatao saba ambao waliamini kuwa wanavutiwa kimapenzi na wanaume wengine. Polisi ilifanya baadhi ya ukamataji huu nyumbani, mwingine katika sherehe na mwingine mtaani. Polisi waliwaachia wawili mara moja baada ya kuwakamata na kuwachukua wanaume wengine tisa hadi Hospitali ya Mnazi Mmoja (hospitali kubwa ya umma Zanzibar) ambapo madaktari waliwapima kwa nguvu njia ya haja kubwa, matumizi ya kwanza ya upimaji huo yanayojulikana kwa umma nchini Tanzania. Wanaume hao waliwekwa kizuizini kwa siku kama tano hivi kisha kuachiliwa baadae kwa dhamana. Kesi dhidi yao haijafungwa bado, kwa kadiri wanaharakati wa Zanzibar wajuavyo, na wanaume hao hawakuwahi kuona majibu ya vipimo vile, ambavyo madaktari waliwapatia polisi.[200]

Mwezi Februari 2017, Naibu Waziri wa Afya Kigwangalla alitoa amri hadharani ya kukamatwa kwa watu watatu, Kaoge (mwanamke asiye na jinsia ya asili aliyehojiwa mwaka 2016 na Clouds TV, na kuelezewa kimakosa katika vyombo vya habari kuwa ni mwanaume anayevutiwa kimapenzi na wanaume wenzake) na vijana wengine watumiaji wakubwa wa mtandao wa Instagram, kwa kutuhumiwa “kutangaza mapenzi ya jinsia moja.”[201] Mwezi Machi, polisi kutoka kituo cha Oyster Bay jijini Dar es Salaam walimkamata mmoja wao Johnnie D. Walimkamata kwa siku tano na kumfanyia kipimo cha nguvu cha njia ya haja kubwa katika Hospitali ya Mwananyamala.[202] Johnnie D aliiambia Human Rights Watch:

Walinipeleka hospitali na kunipima VVU. Halafu wakaniambia nipige magoti, wakanivua nguo, halafu wananiingizia kitu kama mti hivi wenye umbo la bapa kwa mbele. Polisi ndio walikuwa wanawaambia madaktari nini cha kufanya. Sidhani kama walikuwa na amri ya mahakama. Kulikuwa na polisi mmoja ndani ya chumba wakati wananifanyia uchunguzi huo. Ilikuwa inauma sana. Nilijisikia vibaya.[203]

Johnnie D aliachiwa kwa dhamana lakini alitakiwa kuendelea kuripoti polisi kwa siku kadhaa, ambapo baadae aliambiwa aache kuripoti, bila maelezo yoyote yale ikiwa kesi yake imefungwa.[204]

Polisi, kwa kufuata amri ya viongozi wa Kijiji, waliwakamata watu takribani 17 kijijini kaskazini mwa Tanzania tarehe 25 na 26 Januari 2019, wakiwalenga wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume na watu wengine wasiopenda kujitambulisha na jinsia yoyote ile pamoja na watu wengine ambao walidhaniwa tu kuwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume wengine, na kuwaweka kizuizini kwa siku nne hadi sita. Muathirka mmoja, Kim, aliiambia Human Rights Watch:

Nilikuwa nyumbani mara wakaja watu wawili wakiwa na pikipiki wakaniambia mkuu wa kituo cha polisi (kijijni) anataka kuzungumza na mimi. Nilidhani kwasababu wiki iliyopita nilikwenda kuripoti juu ya mtu mmoja nje ya club alinitukana, na kunitishia kwamba angenipiga na kuniua nikimsogelea. Lakini kwa bahati mbaya hawakumkamata yule mtu na akakimbia, akatoroka. Hivyo nilipokwenda polisi, nilidhani inahusiana na kesi hiyo, na nilishtuka kwasababu walianza kunitendea isivyopaswa, wakinisukuma, “vua viatu vyako, tupe simu yako na funguo,’ halafu wakaniweka chini ya ulinzi pasipo maelezo yoyote ya tatizo ni nini. Halafu nilipokuwa jela. Niliwaona watu wengine walio na jinsia tata kama mimi ndipo nikajua kwanini nilikuwa pale lakini sikuwa na uhakika. Halafu kadiri muda ulipokwenda, wengine waliendelea kuja wakielezea kisa kama changu – ‘Nilichukuliwa tu nikiwa kazini, sijui kwa nini.’ Sote tulijuana.  Mimi na rafiki yangu ndio tulio wazi [kuhusu utambulisho/mwelekeo wetu wa kijinisia/kimapenzi]. Baadhi ya wengine waliokuwa wakija walikuwa bado wanajificha kuhusu mwelekeo wao wa kimapenzi. Na wengine walioendelea kuja ilikuwa ni kwasababu ya tetesi tu kwamba inawezekana wakawa pia ni wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume…. Halafu tukaanza kuchukuliwa mtu mmoja baada ya mwingine na kupelekwa kuhojiwa, na wakawa wananilazimisha niseme kwamba ninashiriki vitendo vya mapenzi ya jinsia moja kitu ambacho nilikataa, na wakanitishia kunipiga, lakini nikasema nitaenda kulalamika dhidi yao mahakamani.[205]

Kim alishangaa wakati ambapo polisi, Januari 28, badala ya kuwapeleka mahakamani, waliwapeleka kwenye gari la polisi kutoka kituo cha polisi walichokuwa wanashikiliwa na kwenda baa ya Kijiji hadi kwenye ukumbi wa mikutano uliopo juu ya baa hiyo, ambapo waliwakuta viongozi wa Kijiji wamekusanyika hapo, pamoja na bwana mmoja ambaye Kim anamfahamu kuwa ni mpiga picha, ambaye alipiga picha za watuhumiwa wote lakini, kadiri Kim anavyojua, hakuzichapisha katika vyombo vya habari wala mitandao ya kijamii. Kim aliongeza:

Viongozi wa Kijiji wakaanza kutukosoa, kututukana, kutudhalilisha, kutupiga picha…. Baada ya hapo mmoja wa viongozi wa Kijiji akasema ‘Nyie watu mnapaswa kusafirishwa mpelekwe nje ya nchi yetu na jamii yetu, mna tabia mbaya, hiki ni kinyume na dini yetu na sheria yetu.’ [206]

Januari 29, Kim alisema, polisi waliwachukua hadi hospitali ya wilaya ambapo walifanyiwa vipimo vya nguvu vya njia ya hajakubwa, ambavyo vilifanywa na madaktari huku polisi wakiangalia. Alielezea uchunguzi huo na namna gani ambavyo bado uliendelea kumsababishia maumivu wiki mbili baadaye wakati Human Rights Watch walimfanyia mahojiano:

Hawa madaktari walitufanyia vipimo hivi vya njia ya haja kubwa. Maofisa wa polisi walikuwepo wakiwa wameshika bunduki, walikuwa wengi sana…. Tulikwenda katika wadi ya kina mama wajawazito. Walichukua nyenzo fulani ya chuma wakatuingizia – walituingizia katika sehemu zetu za haja kubwa, na ilikuwa inauma sana, sana, sana. Wakawa wanasema ‘Kohoa, jaribu kukohoa’ wakati chuma lile likiwa ndani ya njia zetu za haja kubwa, na wakati nikiwa nakohoa ndio walikuwa wananiingizia hilo li chuma. Lilikuwa ni jambo la kikatili sana na lenye maumivu sana. Wakawa wanaminya korodani na uume wangu. Kila kitu kuhusiana na kipimo kile kilikuwa cha kikatili sana. Na wakayatunza majibu – hatukuyaona matokeo wala kuwa na muwakilishi yeyote ambaye angetuchukulia majibu ya kipimo. Polisi walikuwa wamejaa chuki sana. Hadi sasa bado nina lengelenge kwa sababu chuma lile lilikuwa kubwa sana. Kimwili, bado sijapona vizuri, hata kiakili, kwasababu ya vipimo vile na jinsi walivyokifanya.[207]

Watuhumiwa wale waliachiwa, wengine Januari 29, wengine Januari 30, Kim alisema. Kim alikimbia Tanzania kutafuta hifadhi, akiamini asingeweza kuwa salama tena kijijni kwake.[208]

Mwanaharakati Zanzibar aliiambia Human Rights Watch kwamba mwezi Agosti 2019, kikundi cha wananchi kiliwakamata wanaume wawili ambao kiliwashuku kuwa na mapenzi ya jinsia moja, na kuwapeleka polisi. Mwanaharakati alisema alijaribu kuzungumza na mmoja wa wanaume hao baada ya kuwa ameachiwa, aliyesema kwamba polisi walimpeleka Hospitali ya Mnazi Mmoja na kumfanyia kipimo cha nguvu cha njia ya haja kubwa.[209]

Ukamataji Unaohusiana na Hofu ya “Ndoa za Jinsia Moja”

Wasiwasi wa kimaadili juu ya tetesi za uchumba au ndoa za jinsia moja zimechochoe baadhi ya ukamataji. Geita, kaskazini mwa Tanzania, polisi waliwakamata watu wanne mwezi Disemba 2017 baada ya kipande cha video kusambaa kikiwaonyesha wanawake wawili wakibusiana katika baa, ambapo baadhi ya vyombo vya habari vilisema kwamba ilikuwa ni sherehe ya “kushika uchumba.”[210] Mwendesha mashitaka wa serikali aliwashitaki wanawake katika video hiyo kwa  kufanya vitendo vichafu katika video hiyo, wakifafanua kwamba walikuwa wanashitakiwa kwa “kuonyesha vitendo vya kishoga na kubusiana kwa mdomo mbele ya hadhara.” Walimshitaki pia mmliki wa baa ile kwa kuwa “mshehereshaji” na “kuwa sehemu ya ufanywaji wa kitendo kichafu,” pamoja na mtu aliyepiga video ile na kuiweka katika mtando, alishitakiwa kwa “kusambaza ujumbe kwa hiari” chini ya Sheria ya Makosa ya Mtandao ya mwaka 2015.[211] Hii ilikuwa ndio kisa cha kwanza kinachojulikana cha wanawake kushitakiwa kwa kushutumiwa kuwa katika mapenzi ya jinsia moja nchini Tanzania. Mwezi Mei 2019, wakati kesi ikiendelea kusikilizwa ambapo mahakama ilikataa kupokea Ushahidi wa maandishi kwa misingi kwamba mtuhumiwa alikuwa amelazimishwa kutia saini ushahidi ule, upande wa mashitaka uliitaarifu mahakama kwamba hautaendelea na mashitaka yale. Lakini, siku nne baadae, polisi iliwakamata wale wale watu wanne na waendesha mashitaka wa serikali wakafungua mashitaka yale yale kwa wale ambao mashitaka yao yalikuwa yamefutwa. Wakati wa uandishi wa ripoti hii, kesi yao ilikuwa bado iko wazi.[212]

Visiwani Zanzibar, ukamataji wa wanaume kumi kwa kile polisi walichokiita “ndoa ya wapenzi wa jinsia moja” ilisababisha habari kubwa duniani kote Novemba 2018, muda mfupi baada ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda alivyotishia kuwasaka na kuwakamata wanaume wote wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wenzao.[213] Kwa mujibu wa mwanaharakati Zanzibar, Mkuu wa Mkoa anayesimamia mkoa wa Kusini Magharibi wa Zanzibar unaojumuisha Stone Town, Ayoub Mohammed aliitikia wito wa makonda wa Novemba 2018 wa kuwakamata wanaume wote wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wenzao.[214]

Human Rights Watch ilizungumza na fadil, mmoja wa wanaume waliokamatwa visiwani Zanzibar. Alisema:

Tulikuwa tumetoka kwa mapumziko na kwenda pembeni ya mji katika fukwe iitwayo Chwakwa Beach, tukifurahia tu mwisho wa wiki. Tulikuwa watu kumi na tatu. Tulikuwa tumekaa tu pale, ambapo mara tu polisi wakatukamata na kuanza kutupiga. Walisema mambo ya kututukana, kama vile kwamba sisi tulikuwa wasenge na kwamba tulikuwepo pale kusherehekea harusi. [215]

Fadil alisema wanaume wachache walifanikiwa kukimbia, lakini polisi ilimkamata yeye na tisa wengine na kuwashikilia katika kituo cha polisi cha Chwakwa. “Tulipouliza tumefanya kosa gani, walisema tunadhaniwa kuwa na uhusiano wa jinsia moja na pia kwamba tulikuwa ufukweni kurasimisha ndoa ya wanaume wawili.” [216]

Polisi waliwashikilia watu hao bila mawasiliano yoyote kwa siku tano, alisema Fadil. Aliongeza:

Tulinyimwa chakula na maji. Ilibidi tunywe maji kutoka bombani. Baada ya habari za kukamatwa kwetu kusambaa Zanzibar nzima, [shirika la kijamii] likaja na kutusaidia kupata dhamana.[217]

Kama sharti la dhamana yao, wanaume hao walitakiwa kuripoti kituo cha polisi kila wiki. Fadil alisema aliacha kwenda kuripoti polisi Januari 2019: “Polisi walikuwa wanapoteza tu muda na pesa zetu.” Hakujua kama kesi yao bado iko wazi. [218]

“Kutembea Ukiwa LGBT”

Pamoja na visa hivi mashuhuri, Human Rights Watch iliwahoji pia wana-LGBT wengine nane ambao walikamatwa kati ya mwaka 2016 na 2018 wakiwa katika shughuli zao tu za kila siku.

Suleiman, mwanafunzi wa chuo kikuu, alisema maofisa wawili wa polisi walimkamata yeye wakati akitembea kuelekea darasani akiwa na rafiki yake wa kiume ambaye huvutiwa kimapenzi na wanaume wengine pamoja na marafiki wengine kadhaa wa kike jijini Dar es Salaam Machi 2018:

Nilikuwa natembea tu barabarani na rafiki zangu, tukitoka chuo, nikashtuka pale polisi alipokuja usoni kwangu na kunichukua tu kunipeleka katika kituo cha polisi. Polisi walikuwa wanalalamika kuhusu wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wengine waliopo katika jamii. Sijui kwanini walinidhania mimi, inawezekana ni kutokana na namna nilivyokuwa natembea…. Walinipeleka katika gari lao kisha wakanipeleka kituo cha polisi Magomeni. Walinipiga vibao na kuzungumza lugha mbaya dhidi yangu. Walimpiga kibao rafiki yangu pia. Walisema kwamba naiaibisha jamii, na kuniuliza kwanini nilikuwa vile, na kuniambia niache kufanya hivyo vitu na kuanza kuwa mwanaume wa kweli.[219]

Suleiman alisema polisi waliwapigia simu babu na bibi yake, ambao walilipa rushwa ya shilingi 50,000 (sawa na $22) ili kuachiliwa. Alisema polisi waliwaambia babu na bibi yake “kunilinda nisitembee na wasichana na mashoga ili kuepuka kuwa kama vile.”[220]

Wengine walikamatwa kiholela wakiwa katika baa na nyumbani kwao kwasababu aidha polisi au mmoja wa wanafamilia wao aliwahisi kuwa ni wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wengine. Victor, mwanaume anayevutiwa kimapenzi na wanaume wengine jijini Dar es Salaam, alisema yeye na mpenzi wake walikamatwa nyumbani kwao mwezi Machi 2017 baada ya majirani kuwaripoti polisi. Walishikiliwa kwa siku tatu au nne hadi walipolipa rushwa ya shilingi 100,000 ($43) kuachiwa huru. Walipokuwa mikononi mwa polisi, Victor alisema, mwenzi wake alibakwa mara mbili na mshikiliwa mwenzao.[221]

Ahmed alikamatwa April 2017 pamoja na rafiki zake wengine wanne wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wengine jijini Dar es Salaam:

Tulikuwa baa tunakunywa na wanaume wengine wanaovutiwa kimapenzi na wanaume… mara tukawa tumekamatwa na polisi. Walituambia, ‘Mlikuwa mnakunywa pombe usiku sana hivyo mnapaswa kupelekwa kituo cha polisi.’ Tulipelekwa Mabatini halafu ndipo masuala ya mwelekeo wa jinsia yetu yakaanza kuibuka, wakisema, ‘Ni makuchu, ni mashoga, na wanalewa hadi usiku.’

Ahmed alisema polisi waliwashikilia usiku kucha bila ya kuwaeleza mashtaka dhidi yao. Waliachiwa baada ya kulipa rushwa.[222]

Hassan, mwanamke asiye na jinsia yake ya asili kutoka Tanga, alisema mwaka 2017, polisi walimkamata akiwa anapata kinywaji baa, na kumpeleka kituo cha polisi cha Chumbageni. Alipowauliza polisi kwanini alikamatwa, anasema, “Walinijibu kuwa mimi ni kinara au kiongozi wa ushoga hapa mkoani Tanga na nimekuwa nahamasisha ushoga hapa mkoani Tanga ambalo jambo hilo limekuwa kero kwa wananchi.”

Hassan alipelekwa mahakama ya Kongwe na kushitakiwa kwa kuwa “mzururaji.” Hakimu alipogundua kwamba nilikuwa mwanamke nisiye na jinsia yangu ya asili, alisema, “wakanilazimisha kuvua nguo za kike nilizokuwa nimevaa na kunipa nguo za kiume zilizokuwepo pale mahakami, halafu wakanipa onyo kuacha mara moja hiyo biashara ya mapenzi ya jinsia moja.” Hassan aliachiwa kwa dhamana.[223]

Medard, mwenye umri wa miaka 38, alisema kwamba Machi 2018, mwenyekiti wa mtaa katika eneo analoishi jijini Dar es Salaam siku moja alikuja mlangoni kwangu usiku wa manane akiwa na wanaume watano, wawili wao walikuwa wamebeba silaha. Walimuhoji kuhusu mpenzi wake na kumshutumu kwa “kuhamasisha ushoga” eneo lile. Medrad alisema, “Walinipiga mgongoni na fimbo, na kunipeleka kituo cha polisi cha Madale. Nilipofika katika kituo cha polisi, polisi walinipiga na virungu na kunitukana.” Alishikiliwa kwa siku tatu kabla jirani yake kuja kulipa rushwa na kuachiwa huru.[224]

Fena, mwanaharakati asiye na jinsia ya asili, alisema kwamba polisi wa Tanzania waliwalenga hasa wanawake wasiokuwa na jinsia ya asili kwa ukamataji wa holela. Alisema kwamba siku moja mwishoni mwa mwaka 2019, polisi walimkamata kiholela, wakamlazimisha kuvua nguo, na kuyaminya matiti yake kabla ya kumwachia kuondoka, na kwamba huko nyuma, polisi walimlazimisha kufanya nae mapenzi ili wamwachie. Alisema pia kwamba maofisa wa usalama katika uwanja wa ndege waliwahi kuwavua nguo wanaume na wanawake wasiokuwa na jinsia za asili.[225]

 

V. Kuzidisha Mashambulizi na Usaidizi wa Kimataifa

Tanzania inategemea sana misaada ya nje, ikiwa ni pamoja na katika mapambano yake dhidi ya VVU. Tangu mwaka 2016, wahisani wameonyesha wasiwasi wao juu ya msako dhidi ya LGBT, ikiwa ni pamoja na madhara yake katika haki ya afya. Mwezi Disemba 2016, Balozi Deborah Birx, Mratibu wa mradi wa Marekani wa UKIMWI Duniani na mkuu wa PEPFAR, ambao wanatoa msaada mkubwa kwa Tanzania katika matibabu ya kufubaza virusi vya UKIMWI alisema:

Tumeeleza wazi kabisa kwamba PEPFAR hii ni msaada wetu wa asilimia 100 kwa watu walio katika hatari ya kuambukzwa VVU/UKIMWI. Na nadhani kwamba itakapofika wakati ambapo itakuwa wazi kwamba serikali ya Tanzania haiamini kwamba kila mtu katika nchi yake anastahili kupata huduma ya afya, itakuwa ngumu kwetu kuendelea na aina hii ya uwekezaji nchini Tanzania.[226]

Katika wakati ambapo inaendelea kuwa wazi kabisa kwamba sera za serikali zinakinzana na misingi mikuu ya huduma za afya kwa wote, mwitikio wa kimataifa umekuwa ukitofautiana. Wahisani wanakabiliwa na chaguzi ngumu. Kutokana na asilimia kubwa ya msaada kutoka kwa wahisani kwa ajili ya programu za kitaifa za VVU, na hasa zile za matibabu ya kufubaza VVU, wahisani wamekuwa wakijaribu kupima na kuwa na sababu za kuogopa kwamba kukata au kusimamisha misaada itawaumiza Watanzania; na kama kusitishwa kwa misaada kutatokana na unyanyasaji unaowaumiza wana-LGBT, jamii hizi zitakuwa ‘mbuzi wa kafara’ katika macho ya umma. Wakati huo huo kuendelea kutoa misaada katika utendaji ambao unapingana wazi na sera za wahisani na viwango vya ulimwengu vya utendaji na ahadi inaweza kuonekana kama vile ni kubariki vitendo vya kibaguzi vinavyokiuka haki za binadamu.

Matukio kadhaa yaliyonukuliwa katika ripoti hii, ikiwa ni pamoja na kukamatwa kwa wanasheria wa shirika la Afrika Kusini Initiative for Strategic Litigation in Africa (ISLA) katika mkutano jijini Dar es Salaam Oktoba 2017 na matumizi ya vipimo vya nguvu vya njia ya haja kubwa kama mbinu ya kutafuta Ushahidi wa vitendo vya mapenzi ya jinsia moja, yamechangia katika muendelezo wa matamko ya kimataifa juu ya msako wa chuki kwa wana-LGBT wa Tazania. Makemeo hayo yalikuwa na matokeo madogo sana yanayoweza kuonekana, isipokuwa, mwishoni mwa mwaka 2018, wakati Paul Makonda, mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, alipotaka kukamatwa kwa “wanaume wote wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wengine” jijini humo. Katika mkutano wake na waandishi wa habari Oktoba 31, makonda alisema watakao kamatwa “watapimwa” kuhusika na mapenzi ya jinsia moja, akimaanisha vipimo vya nguvu vya njia ya haja kubwa. Alisema pia kwamba wale watakaotaka “kubadilika” watapatiwa “ushauri” – akimaanisha tiba ya kubadilishwa, mbinu inayopigwa vita na yenye madhara ya kujaribu kubadilisha mwelekeo wa mtu wa kimapenzi au utambulisho wake wa kijinsia – huku wengine wakifungwa gerezani maisha. Alitangaza, “Hapa Dar es Salaam, ushoga si haki ya binadamu.”[227]

Makonda akawataka watu kumtumia kwa njia ya jumbe fupi za simu (SMS) majina ya wanaodhaniwa kuwa wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wengine, akadai kwamba amekwisha pokea majina yapatayo 200, jambo lililowatisha sana jumuia ya wana-LGBT jijini Dar es Salaam. Siku zilizofuata, baadhi ya wana-LGBT walilikimbia jiji la Dar es Salaam, wengine wakirudi vijijni kwao au kuomba hifadhi kwa ndugu na jamaa zao katika miji ya pembezoni na Dar es Salaam ambapo walidhani hawataweza kufikiwa na kinachodaiwa kikundi kazi cha Makonda, huku wengine wakikimbia Tanzania kabisa.[228] Wanaharakati wa LGBT waliripoti kwa Human Rights Watch kwamba baadhi ya watu waliokuwa wanaishi na VVU waliamua kukaa nyumbani kwa siku nyingi, wasiende kuchukua dawa zao za ARV kwa kuogopa kukamatwa.[229]

Baadhi ya wana-LGBT walitoa taarifa za unyanyasaji ulioongezeka kutoka kwa majirani zao ambao walionekana wakifanya vile kutokana na chuki zao dhidi ya wana-LGBT. “Ilikuwa inaogopesha sana, na tulipitia wakati mgumu sana,” alisema Fena, mwanaharakati asiye na jinsia ya asili, ambaye yeye mwenyewe alikimbilia Nairobi, Kenya kwa miezi mingi, na kusema kwamba wanawake wengine wengi wasiokuwa na jinsia za asili walikumbwa na unyanyasaji siku chache baada ya tamko la Makonda kutoka kwa wananchi wa kawaida na polisi pia.[230]

Muitikio kutoka jamii ya kimataifa ulikuwa wa wazi, haraka na mpana. Kamishna wa Tume ya Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa Michelle Bachelet alikemea msako huo kwa lugha kali, akiyaita matamshi ya Makonda kuwa ni “leseni ya kufanya unyanyasaji, uonevu, vitisho, na udhalilishaji kwa wale wanaodhaniwa kuwa ni wana-LGBT.”[231] Makamu Mkuu wa Serikali wa Ireland alituma barua kwa aliyekuwa waziri wa mambo ya nje wa wakati ule Augustine Mahiga tarehe 2 Novemba 2018, akiitaka serikali kukanusa matamshi hayo na kusimamisha pendekezo hilo la Makonda la msako.[232] Takribani balozi tatu zilizopo jijini Dar es Salaam walimwita Waziri wa Mambo ya Nje kukemea matamshi ya Makonda.[233]

Serikali ya Tanzania ililiona hilo. Tarehe 4 Novemba, Waziri wa Mambo ya Nje alitoa kauli kuitenga serikali na kauli ya Makonda yenye chuki dhidi ya wana-LGBT.  Tamko lilisema, kwa sehemu:

Katika mkutano wake na waandishi wa habari, mheshimiwa mkuu wa mkoa alitangaza kampeni ya kuwashughulikia watu wanaovutika kimapenzi na watu wenye jinsia kama zao jijini Dar es Salaam. Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ingependa kufafanua kwamba mawazo haya ni yake mwenyewe na si ya serikali. Zaidi, serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ingependa kuchukua fursa hii kukumbusha na kusisitiza kwamba itaendelea na kuheshimu makubaliano yote ya kimataifa kuhusu haki za binadamu yaliyosainiwa na kufanywa kuwa sehemu ya sheria za ndani.[234]

Lakini siku hiyo hiyo ambayo Wizara ya Mambo ya nje inatoa kauli ya upatanishi, habari zikaibuka kwamba wanaume kumi walikuwa wameshikiliwa visiwani Zanzibar kwa tuhuma za kushiriki harusi ya watu wa jinsia moja.[235] Hata kama ukamataji wenyewe ulikuja kabla ya kauli ya wizara ya Mambo ya Nje, maofisa waandamizi wa serikali hawakutaka kukubali au kukemea ukamatwaji, na wanaume wale wakabaki kizuizini hadi Novemba 8. Zaidi, Novemba 9, alipoulizwa Bungeni na Mbunge ambaye aliyekuwa anadai kwamba Tanzania imesalimu amri baada ya shinikizo la kimataifa kuruhusu ndoa za jinsia moja na watu wanaovutiwa kimapenzi na watu wenye jinsia kama zao, Waziri wa Mambo ya Ndani wa wakati ule Kangi Lugola akasema, “Tanzania si mahali sahihi kwa vitendo hivyo; kamwe hatutaruhusu haya mambo hayo yafanyike. Tuna sheria zinazozuia hayo mambo.”[236]

Idara ya Mambo ya Nje ya Marekani ilitoa tamko tarehe 9 Novemba kukemea hali nzima ya unyanyasaji, vitisho na ubaguzi pamoja na ukamataji wa wana-LGBT.[237] Waziri wa Mambo ya Nje wa Denmark alitangaza tarehe 14 Novemba kwamba Denmark itazua kiasi cha dola milioni 10 ($10 milioni) cha msaada kwa Tanzania kwa misingi ya haki za binadamu, ikiwa ni pamoja na unyanyasaji kwa misingi ya muonekano wa ulengwa wa kimapenzi na kwamba fedha zingine zitaelekezwa kutoka serikalini kwenda kwa asasi za kiraia.[238] Denmark walirudisha msaada wiki chache baadae bila kuweka wazi sababu hasa za kubadilisha uamuzi wao.[239]

Wawakilishi wa Afrika wa asasi ya International AIDS Society (IAS), wakiandika kwa niaba ya IAS nzima, walikemea pia jitihada hasi dhidi ya wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wengine nchini Tanzania ikiwa ni pamoja na ukamataji Zanzibar na kufungwa kwa vituo vya msaada. IAS ilisema Disemba 2018: “Vitendo hivi ni tofauti na ahadi iliyotolewa na Tanzania kumaliza UKIMWI ifikapo mwaka 2030.”[240]

Kuingilia kwa Benki ya Dunia

Benki ya Dunia, ambayo ndio mfadhili mkubwa kabisa wa Tanzania, ni mara chache sana kuzungumza na nchi wateja wake kuhusu masuala ya haki za LGBT.[241] Hata hivyo, baada ya chama cha wafanyakazi wake wana-LGBT, kiitwacho GLOBE, kujua kuhusu kauli za uchochezi za Makonda na kuelezea wasiwasi wao ndani ya ofisi, Novemba 7 Benki ilitoa tamko kusitisha ziara zake zote Tanzania kwa misingi kwamba haitaweza kuwalinda wafanyakazi wake ambao ni LGBT wasikamatwe.[242] Karibu muda huo huo, benki ilitangaza kwamba itazuia dola milioni 300 za mkopo wa elimu kutokana na sera ya Tanzania ya kukataa kuwaruhusu wanafunzi wajawazito na kina mama watoto kusoma katika shule za sekondari za umma.[243]

Novemba 17, makamu wa rais wa Benki ya Dunia kwa Afrika, Hafez Ghanem, na wafanyakazi wengine waandamizi walikutana na Rais Magufuli kuelezea wasiwasi wao juu ya masuala yote, pamoja na Sheria ya Takwimu ya Tanzania, ambayo ilifanya jinai kuchapisha takwimu zinazokinzana na zile rasmi zilizotolewa na serikali.[244] Katika mkutano huo, Ghanem aliwasilisha masuala haya matatu kama vitu visivyokuwa na mjadala, akisema benki haitaweza kuendelea kufanya biashara na Tanzania kama itaendelea kuwatesa wana-LGBT na kukataa kubadilisha mpango wake kuhusu kuwaruhusu wasichana kupata elimu na Sheria ya Takwimu.[245] Baada ya mkutano huo, Benki ya Dunia ilichapisha tamko lililosema:

Rais ameihakikishia Benki kwamba Tanzania haitatekeleza vitendo vyake vya kibaguzi vinavyohusiana na unyanyasaji na/au ukamataji wa watu, kwa misingi ya mwelekeo wao wa kimapenzi.
Kama mwanachama wa Taasisi ya Benki ya Dunia, Tanzania iliidhinisha Mpango mpya wa Mazingira na Kijamii(ulioanza Oktoba 2018), ambao uliimarisha kujitoa kwa Benki katika ujumuishaji kijamii wa makundi ya watu wanyonge na walio hatarini na kutowabagua kwa misingi ya umri, jinsia, kabila, dini, fizikia, kiakili na ulemavu mwingine, hali zao za kijamii, kiraia na kiafya, mwelekeo wa kimapenzi, asili yao na hali ya kiuchumi.[246]

Mkutano huo, na mbinu walizotumia Benki ya Dunia, inaonekana ulizaa matunda kiasi fulani. Hadi leo hii, Tanzania haijabadilisha sera zake zozote zinazowakataza wasichana na kina mama watoto kupata elimu. Tanzania ilibadilisha Sheria ya Takwimu, ikaondoa adhabu za jinai. Maofisa wa serikali, kwa muda kidogo, walionekana kupunguza makali ya kauli zao za kichochezi dhidi ya haki za wana-LGBT. Wakati maofisa wa mahala walipotoa amri ya kukamatwa kwa wanaume 14 wanaodhaniwa kuwa ni wana-LGBT katika mji mdogo, uliojadiliwa katika Sehemu ya IV hapo juu, wanadiplomasia waliijulisha ofisi ya rais. Wanaume wale waliachiwa baada ya muda mfupi bila mashtaka yoyote na swala lile likatupiliwa mbali na mahakama ambayo walikuwa wamepelekwa.[247]

Lakini upatikanaji wa huduma za afya maalum kwa wana-LGBT bado ni ngumu kwa wana-LGBT wengi na kwa watu wa makundi maalum, kama ilivyodokezwa Sehemu ya VI.

Kuingilia kwa PEPFAR

Mfadhili mkubwa wa kazi ya kuzuia na kutibu VVU Tanzania ni Mfuko wa Dharura wa kupambana na UKIMWI wa Rais wa Marekani (PEPFAR), ambao hufanya kazi chini ya Ofisi ya Marekani ya Mratibu wa Masuala ya UKIMWI duniani. Kila mwaka, PEPFAR inatoa Mpango wa Utendaji wa Nchi kwa nchi na kanda zote 28 zinazonufaika na mradi huu.[248]

Januari 16, 2019, Mratibu wa Masuala ya UKIMWI duniani wa Marekani, Balozi Debora Birx, anayesimamia PEPFAR, aliuandikia Ubalozi wa Marekani Tanzania kuwajulisa kwamba ofisi itapunguza ufadhili wa PEPFAR kwa Tanzania kutoka dola milioni 512 mwaka 2018 kwenda dola milioni 395 mwaka 2019. Barua ilisema “utendaji usioridhisha wa nchi mwanachama” na hasa ikagusia jinsi Tanzania inavyowafanya kundi dogo la mwelekeo wa kimapenzi, pamoja na wanawake na watoto:

Ni muhimu kueleza kwamba programu ya PEPFAR/Tanzania inakumbana na vipingamizi vya pekee katika kusonga mbele. Sera rasmi na zisizo rasmi zinazoendelea kuibuka Tanzania zinakwamisha jitihada za upimwaji na matibabu kwa watu walio katika hatari kubwa zaidi ya kuambukizwa VVU, ikiwa ni pamoja na ukamatwaji wa watu wachache wenye mwelekeo tofauti wa kimapenzi, upingwaji wa matumizi ya vidonge vya uzazi wa mpango, na ufukuzwaji wa wasichana wajawazito shuleni.[249]

PEPFAR ikasema kwamba utoaji wa fedha siku za usoni utategemea maboresho, ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba “programu muhimu zitaendekea kuakisi msimamo wa serikali ya Marekani katika kushughulikia mahitaji ya wale walio katika hatari zaidi ya kuambukizwa VVU.”[250]

Katika Mkutano wa Kikanda wa Mipango wa PEPFAR uliofanyika Johannesburg mwezi Machi 2019 na kuhudhuriwa na maofisa wa PEPFAR, wawakilishi wa wizara ya afya wa Tanzania, na wawakilishi wa asasi za kiraia, maofisa wa PEPFAR waliwaambia maofisa wa Tanzania kwamba moja ya njia ya kuonyesha utayari wa kushughulikia mahitaji ya jamii iliyo katika hatari zaidi ni kupiga marufuku upimwaji wa nguvu wa njia ya haja kubwa kwa watu wanaoshutumiwa kufanya vitendo vya mapenzi ya jinsia moja. Vipimo vya nguvu vya njia ya haja kubwa vimekuwa vikifanywa na maofisa wa afya mara nyingi nchini Tanzania tangu mwaka 2016, kwa maelekezo ya polisi. Matokeo yake, Wizara ya Afya ikatuma muongozo uliotolewa Januari 2019 unaowataarifu watumishi wa afya kwamba upimaji wa nguvu wa njia ya haja kubwa unaweza kufanywa pale tu panapokuwa na amri ya mahakama kutoka kwa hakimu.[251] Hata hivyo, muongozo huo haukuzuia vipimo. Wanaharakati walipinga lugha dhaifu iliyotumika, na mtandao wa kimataifa wa MPact, kwa kushirikiana na mashirika ya Tanzania na kimataifa, wakatoa lalamiko likiitaka Tanzania kuheshimu ahadi yake iliyoitoa kwa PEPFAR na kupiga marufuku upimwaji wa nguvu wa njia ya haja kubwa. Mashirika arobaini na tano yalisaini lalamiko hilo.[252]

Kutokana na kutofikia maafikiano, PEPFAR iliwaalika wawakilishi wa serikali ya Tanzania katika mkutano wa “kukumbushia” Washington DC mwezi Aprili. Katika mkutano huo, wizara ya afya ilikuwa inasita kuahidi kupiga marufuku upimwaji wa nguvu wa njia ya haja kubwa lakini ilikubali kwamba itashirikiana na wawakilishi wa makundi maalum katika kuboresha upatikanaji wa huduma za afya na kufanyia kazi hatua za kupiga marufuku kabisa upimwaji wa nguvu wa njia ya haja kubwa.

Afisa wa PEPFAR aliwaambia Human Rights Watch kwamba mkutano ujao utakaofanyika Johannesburg kuanzia Machi 2-6, 2020, taasisi yao itajadiliana na wawakilishi wa Wizara ya Afya na asasi za kiraia juu ya hatua zilizopigwa kuelekea kuwahusisha kundi maalum katika kutekeleza programu za VVU/UKIMWI nchini Tanzania na kuondoa vikwazo vya kimuundo vya upatikanaji wa huduma. Maafisa walisema PEPFAR itafanya uamuzi wa kutoa fedha zaidi kutokana na majadiliano hayo na masuala mengine ya programu.[253]

 

VI. Wajibu Chini ya Sheria ya Kimataifa na Kikanda

Tanzania ni miongoni mwa washirika wa kimataifa na kikanda katika mikataba ya haki za kibinadamu ambapo wana majukumu ya kuhakikisha kuna upatikanaji wa huduma bora za afya, haki na uhuru, uhuru wa kujumuika pamoja, uhuru kujikusanya na kujieleza, haki ya kuwa na faragha na haki ya uhuru dhidi ya kutengwa miongoni mwa haki zingine za kibinadamu. Wakati ukosoaji wa jumuiya ya kimataifa umepamba moto juu ya ukandamizaji wa wana-LGB Tanzania, Wizara ya Mambo ya Nje iliahidi kuwa Tanzania itazidi kuheshimu na kulinda haki za kibinadamu. Ahadi hii haijaleta mafanikio yoyote ya maana ambayo yanaambatana na kiwango kinachohitajika cha kiamataifa kulingana na kesi zilizo katika kumbukumbu ya ripoti hii.

Haki ya Kupata Afya ya Kiwango Cha Juu Iwezekanavyo

Kama jinsi ambavyo ripoti hii inaonyesha, mamlaka nchini Tanzania zimekataa ushahidi uliowekwa wa njia za kuzuia VVU miongoni mwa makundi yaliyotengwa na kushindwa kuhakikisha uhuru dhidi ya kubaguliwa kwa misingi ya mwelekeo wa kimapenzi na utambulisho wa kijinsia katika katika vituo vya afya vya serikali. Kupigwa marufuku matumizi ya vilainishi inawanyima watu ambao wako katika hatari ya kupata maambukizi ya VVU / UKIMWI kifaa cha muhimu sana, kilichothibitishwa  kuwalinda wakiwa wanashiriki ngono. Katika haya na maswala mengine Tanzania imeshindwa katika kutekeleza majukumu yake ya kuhakikisha haki ya upatikanaji wa haki ya kiwango ambacho ni bora kwa afya kwa watu wote.

Tanzania imeridhia Mkataba wa Afrika wa Haki za Watu na Binadamu  (African Charter on Human and Peoples’ Rights (ACHPR)), Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiuchumi, Kijamii na Kitamaduni, (Covenant on Economic, Social and Cultural Rights (ICESCR)), na Mkataba wa Kimataifa wa Kuondoa Aina Zote za Ubaguzi Dhidi ya Wanawake – (Convention on the Elimination of All Forms of Discrimination Against Women (CEDAW)), yote ambayo inahakikisha haki ya juu ya kupata kiwango bora cha afya.[254] Kamati ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Kiuchumi, Kijamii na kitamaduni  ambayo inatoa tafsiri halali ya ICESCR, wamehitimisha kwamba haki ya afya inaweka jukumu kwa serikali kuchukua hatua muhimu kuzuia na kutibu na kudhibiti majanga na magonjwa mengine ambayo yanahitaji uanzishwaji na uzuiaji na mipango ya elimu kuhusu tabia zinazohusika na mambo ya kiafya kama magojwa yanayo ambukizwa kupitia ngono, hasa VVU/UKIMWI na yale yanayoathiri afya ya uzazi.” [255]

Kamati inasisitiza jukumu la kutoa afya bora na huduma bila ubaguzi “kisheria na kwa matendo.”[256] Jukumu la kuhakikisha haki zote chini ya ICESCR bila ya ubaguzi moja kwa moja haliruhusu ubaguzi kwa misingi ya ulengwa wa kimapenzi na kijinsia na utambulisho wa kijinsia.[257]

Tanzania pia imeridhia Mkataba wa Maputo wa Haki za Wanawake Afrika. Unaeleza kwamba nchi zinapaswa kuhakikisha „haki ya kujilinda na kulindwa dhidi ya maambukizi ya magonjwa ya zinaa ikiwemo VVU / UKIMWI.”[258]

Sheria zingine za kikanda na sera za maendeleo pia zimesisitiza wajibu wa kuchukua hatua ya kulinda afya ya makundi maalum, hasa kuhusiana na VVU. Sheria ya Jumuiya ya Africa Mashariki ya Kuzuia na Kudhibiti VVU na UKIMWI (East African Community HIV and AIDS Prevention and Management Act), ambayo ilitungwa na kupitishwa mwaka 2016, inazitaka serikali  za Afrika Mashariki, ikiwemo Tanzania, kukataa unyanyapaa na ubaguzi dhidi ya makundi yaliyo katika hatari zaidi; kutekeleza mikakati kukuza na kulinda afya ya makundi ya walio katika hatari zaidi; na kuhakikisha ya kwamba mbinu za ulindaji zinazotambulika zinapatikana kwa makundi ya walio katika hatari zaidi. [259]

Miongozo ya Kikanda na Kimataifa ya Kufikia Haki ya Afya

Kuna ushahidi wa kutosha wa utendaji bora na makubaliano ya kikanda jinsi ya kutetea haki ya afya kwa makundi maalum. Kushindwa kwa Tanzania kuheshimu, kulinda na kutimiza haki ya upatikananji wa afya yenye kiwango bora cha afya inapingana na uhalisia huo. Mamlaka husika sio tu kwamba zinakandamiza amri ya kutoa huduma ya kiafya na nyenzo kwa wana- LGBT; wanafanya bidii kuwazuia watu wengine ambao wangetamani kutoa huduma hizo, ikiwemo wafadhili wa kimataifa na asasi zisizo za kiserikali nchini za Kitanzania na kimataifa.

Jumuia ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC), ambayo Tanzania ni nchi mwanachama imetoa mfululizo wa viwango vya jinsi ya kushughulikia VVU na afya ya ngono na afya ya uzazi. Kama ukanda ambao umeathirika zaidi na janga la VVU duniani, Ukanda wa SADC umeelezea ahadi ya uhakika katika mbinu za kushughulikia zitokanazo na ushahidi zinazowafikia wale wenye uhitaji zaidi bila kujali hali ya kisiasa na kitamaduni. “Viwango vya chini” vya SADC vya mwaka 2015 vinataka nchi wanachama kuzingatia “vitendo visivyo vya kibaguzi, bila kujali hali ya VVU, umri, jinsia, utambulisho wa kijinsia, dini, utamaduni wa kijamii na hali ya kiuchumi.”[260] Zaidi ya hapo, viwango vya chini vya ubora vinaitaka nchi kufanya yafutayo:

  • Kuunda sera ambazo zitafanikisha ufikiwaji wa afya ya ngono na afya ya uzazi na huduma za VVU kwa makundi maalum ikiwemo wanawake wanaovutiwa kimapenzi na wanawake wenzao, wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wenzao, wasiokua na jinsia ya asili, na walio na jinsia zaidi ya moja (LGBT).[261]
  • Kupitia mfumo wa kisheria ambao utaleta matokeo ya kufikiwa kwa huduma za afya ya ngono na afya ya uzazi na huduma za VVU na taarifa kwa makundi maalum, haswa wanaume wanaoshiriki ngono na wanaume, na kama ikihitajika kubadili sheria zao ipasavyo.[262]
  • Kutunga sheria zinazohakikisha upatikanaji na matumizi ya afya ya ngono na uzazi na huduma za VVU kwa jamii ya makundi maalum.[263]
  • Kuendeleza mipango kazi ya afya ya ngono na uzazi na VVU ambayo itajumuisha “Kuingilia kati na kwa uwazi kwa makundi maalum.”[264]
  • Kuweka mifumo kabambe, ikiwemo vituo muhimu na kutoa huduma za kijamii zilizoboreshwa na miundombinu, kuwezesha ufikiaji wa huduma za afya ya ngono na uzazi na VVU kwa jamii ya makundi maalum haswa watu wa LGBT.[265]

Mnamo Novemba mwaka 2018, SADC ilipitisha Mbinu ya Haki za Afya ya Ngono na Uzazi katika kanda ya SADC, 2019-2030, Iliyosainiwa na mawaziri wa afya wa kanda nzima ikiwemo Tanzania.[266] Kuzingatia mahitaji kuhusu viwango vya chini vinavyokubalika, mbinu inazitaka nchi wanachama "kuhakikisha ya kwamba mazingira ya kisheria na siasa ni ya kufaa kwa upatikanaji wa haki za afya ya ngono na uzazi” kwa makundi yote ya wananchi, huku makundi maalum yakitajwa pia.[267] Misingi inayozingatiwa kwenye mbinu hii ni pamoja na “matazamo unaozingatia mwelekeo wa jinsia, wenye maono na mabadiliko…na ambao unalinda na kukuza ustawi wa kimwili mshikamano na uhuru wa kujiamulia kwa wote, kufanya kipaumbele kwa utoaji wa huduma kuhakikisha hakuna anayeachwa nyuma” pamoja na matazamo wa haki za kibinadamu katika utoaji wa huduma za afya ya kingono na kizazi, ikiwa ni pamoja na haki ya kila mtu kupata kiwango cha juu zaidi cha afya kiwezekanacho.” Mbinu inataka kuondolewa kwa vizuizi vya kisera, kitamaduni, na kijamii vinavyodidimiza matumaini ya kupatikana kwa haki ya kiafya ya uzazi katika ukanda ya SADC.[268]

Tanzania pia iliunga mkono hadharani Tamko la Umoja wa Mataifa la Kisiasa la 2016 juu ya VVU na UKIMWI. Linahimiza mataifa kuunda mifumo na sera za afya zinazowajali na kuwahusisha watu, kwa sehemu “kwa kukuza kuwa sera hizo ziundwe kwa misingi ya mitazamo isiyo ya kibaguzi ambayo inaheshimu, inakuza na kulinda haki za binadamu, na kwa kujenga uwezo wa mashirika ya kijamii kuweza kutekeleza mipango ya huduma za uzuiaji na matibabu ya VVU / UKIMWI.” Wanachama wa Umoja wa Mataifa walikubaliana kuwa “kutambua kwamba “mapambano dhidi ya HIV yanaweza kuharakishwa kwa kulinda na kukuza upatikanaji wa taarifa sahihi, kiwango cha juu, zitokanazo na ushahidi juu ya VVU, mafunzo na huduma isiyokuwa na unyanyapaa na ubaguzi” na kujitolea “kuongezea tena maradufu juhudi zisizobagua za kuzuia VVU kwa kuchukua hatua zote kutekeleza mitazamo ya kuzuia iliyo kamilifu na inayotegemea ushahidi ili kupunguza maanbukizi mapya ya VVU.”[269]

Kwa kuzingatia utendaji uliyo bora zaidi ulimwenguni kote, Ripoti ya Kuziba Mwanya wa Uzuiaji ya UNAIDS iliyochapishwa mwaka wa 2016, inaangazia mabadiliko muhimu ya sera ili “kufanikisha kumalizwa kwa janga la UKIMWI kufikia mwaka wa 2030.” Ripoti pia inapendekeza upatikanaji kwa urahisi wa mipira ya kiume, vilainishi na PrEP, na pia juhudi za kupambana na chuki kwa wana-LGBT.”[270]

Tume ya Ulimwengu kuhusu VVU na Sheria, tume ya wataalamu ambayo iliundwa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) mwaka 2010, inatoa mwito wa kutoharamishwa kwa matendo ya kimapenzi baina ya watu wa jinsia moja.[271] Ni jambo lililodhihirika wazi kwamba unyanyapaa, ubaguzi, uharamishaji na kutekelezwa kwa sheria za kibaguzi hudhoofisha huduma za VVU miongoni mwa makundi maalum.[272]

Kukaidi kwa Tanzania kuzingatia viwango bora vya utendaji kazi na viwango vya chini zaidi vya kikanda katika utendaji kazi wake unazua hatari ya kuenea kwa VVU, na kuhujumu haki ya kufikia viwango vya juu iwezekanavyo vya afya.

Haki za Uhuru wa Kukusanyika

Mkataba wa Afrika wa Haki za Watu na Binadamu, chini ya kifungu 11, unamhakikishia kila mtu uhuru wa kukutana, “haki ambayo inaweza kupunguzwa tu iwapo kuna haja ya vikwazo vilivyowekwa na sheria, haswa vile vilivyopitishwa kwa sababu za usalama wa kitaifa, usalama, afya, maadili na haki za na uhuru wa wengine.”[273]

Vile vile, chini ya kipengele cha 22 cha Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa, ambao umesainiwa na kuidhinishwa na Tanzania, vizuizi vyovyote kwa haki ya uhuru wa ushirikiano “ni sharti kuwe na sababu muhimu kwenye jamii ya kidemokrasia,” na iwe tu “kwa sababu za usalama wa kitaifa au usalama wa umma, kuzuia fujo, kulinda afya ya umma au maadili au kulinda haki na uhuru wa wengine.” Kipengele cha 2 cha mkataba huo kinazishurutisha nchi zote wanachama kuzingatia haki zote zilizoainishwa kwenye sheria hiyo, ikiwa ni pamoja na uhuru wa kushirikiana, bila kubaguliwa.[274]

Uvamizi wa mamlaka za Tanzania katika warsha na mikutano, kupigwa marufuku kwa makundi mashirika ya kijamii na kujaribu kuweka vikwazo juu ya yapi yatakayojadiliwa au kutekelezwa haiwezi kamwe kuwa ni sababu muhimu ya kulinda jamii, maadili, huduma ya kijamii na haki za wengine.

Na zaidi, vitendo hivi vya unyanyasaji hudhoofisha haki ya huduma ya afya. Kama Tume ya Haki za Binadamu na Watu ya Africa, kwenye ripoti yake kuhusu VVU na Sheria inasema:

Katika muktadha wa VVU Haki ya Kutangamana ni muhimu kuhakikisha mashirika ya kijamii ambayo yanafanya kazi ya VVU na Makundi Maalum, yanaweza kuundwa na kufanya kazi zao kikamilifu. Mashirika ya kijamii wanafanya kazi muhimu katika kutekeleza na kusaidia watu ambao wana VVU, kukuza mabadiliko muhimu ya kisheria, kupambana na ubaguzi na unyanyapaa, na kuzuia uambukizaji na uenezaji wa VVU. Vikwazo vyovyote kwa uhuru wa kushirikiana ni lazima viwe ni vya sababu ya lazima, za viwango sawa na za kihalali. Mashirika ambayo yanafanya kazi katika sekta ya VVU kupitia utoaji wa huduma, kuelimisha, maswala mabadiliko ya kisheria, utetezi – au wale wanaofanya kazi na makundi maalum - ni lazima wakubaliwe kujisajili, kutafuta ufadhili na kufanya kazi zao bila kusumbuliwa wala kuogopa. Vikwazo katika uwezo wa kukubaliwa kuunda shirika unaweza kuwa na athari hasi kwa mashirika ya kijamii na zaidi sana, kwenye janga la VVU.[275]

Haki ya Faragha

Uharamishaji wa vitendo vya mapenzi ya jinsia moja kwa watu wazima ambao wamekubaliana kushiriki katika tendo hilo kwa faragha ni kukiuka haki yao za faragha, na pia ni kukiuka haki yao ya uhuru dhidi ya kutengwa, haki hizi ambazo kila mmoja anahakikishiwa chini ya Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa - International Covenant on Civil and Political Rights (ICCPR) - ambayo Tanzania ni mshiriki.[276] Kumkamata mtu mzima ambaye amekubali kushiriki tendo la ngono la watu wa jinsia moja ni kukiuka marufuku ya kuzuiliwa kiholela.[277]

Kipengele cha 16 katika Katiba ya Tanzania pia kinalinda haki ya faragha.[278] Hakuna mtu ambaye amewahi kuleta kesi mahakamani Tanzania ili kujua iwapo kipengele hiki kinaweza kutumika katika kulinda haki ya wanaoshiriki ngono kwa faragha, lakini mahakama inaweza kuona kwamba sheria zinazopiga marufuku ngono baina ya washiriki wa jinsia moja ambao ni watu wazima waliokubaliana ni ukiukaji wa katiba.

Haki ya Kutokubaguliwa

Tume ya haki za Binadamu na Watu Afrika iliweza kupata kuwa tangu mwaka 2006 ya kuwa kubaguliwa kwa msingi wa mwelekeo wa kijinsia kunakiuka vipengele vya kutokubaguliwa vilivyomo katika Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu.[279] Katika maazimio yake 275 ya mwaka 2014, tume imekemea aina zote za ubaguaji watu kwa msingi ya muonekano halisi au ule wa kuonekana wa kujamiiana na utambulisho wa kijinsia.[280]

Katiba ya Tanzania pia inazuia kubagua watu. Kipengele cha 9, “Utafutaji wa Ujamaa na Kujitegemea,” sets forth:

Serikali na mashirika yake yote yana wajibu wa kuelekeza sera na mipango yake katika kuhakikisha kwamba utu wa mwanadamu umelindwa na kuheshimiwa kwa kuendana na kiini/kusudio la Tamko la Kimataifa la Haki za Binadamu, na kwamba namna zote za dhuluma, vitisho, ubaguzi, rushwa, mateso ama upendeleo zinaondolewa.[281]

Ibara ya 13 ya Katiba imeweka bayana kuwepo kwa haki na usawa na kulindwa kisheria na kukataza serikali kutunga sheria za kibaguzi.[282]

Haki ya Kutokuteswa

Madaktari jijini Dar es Salaam na Zanzibar wametekeleza, kufuatia amri ya polisi, uchunguzi wa lazima wa njia ya haja kubwa kwa wanaume na wanawake wasio na jinsia ya asili wanaotuhumiwa kushiriki katika mapenzi ya jinsia moja. Uchunguzi wa nguvu wa njia ya haja kubwa bila hiari ni aina ya ukatili, unyama na tendo la kushusha hadhi, ambalo kwa wakati mwingine huweza kufikia kiwango cha mateso.[283] Baadhi ya watu waliohojiwa na Human Rights Watch walisema ya kwamba walipitia uchunguzi huo kama njia moja ya ukatili wa kingono, na kwa maoni ya Human Rights Watch, matendo haya ni sawa na unyanyasaji wa kingono.

Kamati ya Umoja wa Mataifa kuhusu Mateso mara ya kwanza ilikemea vitendo vya kutekeleza uchunguzi wa nguvu wa njia ya haja kubwa uliokuwa ukifanyika Misri (Egypt) mnamo mwaka 2002.[284] Kundi Kazi la Umoja wa Mataifa kuhusu Kuzuiliwa kiholela (UN Working Group on Arbitrary Detention) linashikilia ya kwamba, “uchunguzi wa njia ya haja kubwa wa kulazimishwa unakiuka marufuku iliyowekwa dhidi ya ukatili, unyama na kushushwa hadhi, hata kama… umetekelezwa kwa lengo la kuadhibu, kumlazimisha mshukiwa akiri jambo, au kuendeleza ubaguzi.”[285]

Ofisi ya Kamishna wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Binadamu (OHCHR) imetoa witu kwa mataifa kupiga marufuku vipimo vya nguvu vya njia ya haja kubwa.[286] Mashirika kumi na mbili ya Umoja wa Mataifa yalilaani visa hivyo vya uchunguzi kwenye kauli ya pamoja iliyotolewa Septemba 2015 kuhusu unyanyasaji dhidi ya watu wa LGBT.[287] Mwakilishi Maalum wa masuala ya Mateso wa Umoja wa Mataifa ameelezea vipimo vya nguvu vya njia ya haja kubwa kuwa “ni vya kuingilia na kushusha hadhi”[288] “tendo ambalo halina manufaa yoyote kimatibabu ila linachukuliwa kama utesaji na unyanyasaji.[289]

Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, kupitia kwa Kamati yake ya Kuzuia Mateso Barani Afrika - (CPTA), imewataka nchi wanachama:

Kuhakikisha ya kuwa mateso au unyanyasaji haufanyiki dhidi ya watu binafsi kwa msingi ya mwelekeo wa kingono au mwelekeo wa kijinsia. Haswa, mataifa yanapaswa kujizuia juu ya kuunda sheria na sera ambazo athari yake itakuwa ni kuchochea utekelezaji wa mateso na unyanyasaji kwa misingi ya hali hii na vitengo vya serikali, watu binafsi au taasisi zingine zozote

Kauli ya Jumla ya Tume hiyo, nambari. 4 inaelezea vipimo vya kulazimishwa vya njia ya haja kubwa kama aina ya mateso.[290]

Marufuku dhidi ya mateso ni msingi mkuu wa sheria za kimataifa ambayo imenukuliwa kwenye Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa (International Covenant on Civil and Political Rights), Mkataba wa Afrika wa haki za Binadamu na Watu, na Maagano ya Umoja wa Mataifa dhidi ya Mateso, na Tanzania ni nchi mwanachama wa mikataba yote hii mitatu. Marufuku dhidi ya mateso, ukatili, unyama na kushusha hadhi ni sheria imara na yeyote yule haruusiwi kuipuuza wala kuiondoa. Utesaji hauwezi kuhalalishwa katika mazingira yoyote yale.[291]

VII. Shukrani

Ripoti hii ilifanyiwa utafiti na Neela Ghoshal, mtafiti mwandamizi kwenye programu ya Haki za LGBT ya shirika la Human Rights Watch, pamoja na mshauri nchini Tanzania ambaye hakutaka jina lake litajwe kwa sababu za kiusalama, na iliandikwa na Neela Ghoshal. Imehaririwa na Graeme Reid, Mkurugenzi wa Haki za LGBT katika Human Rights Watch, na Joe Amon, mshauri wa afya na haki za binadamu katika Human Rights Watch. Jael Akinyi Onyango, alieko katika mafunzo ya vitendo katika idara ya Afrika ndani ya Human Rights Watch, pia amechangia utafiti wa historia kwa ajili ya ripoti hii.

Ripoti imehakikiwa na Joseph Saunders, Naibu Mkurugenzi wa Programu. Michael Garcia Bochenek, kaimu mshauri wa kisheria, na Oryem Nyeko, mtafiti wa kitengo cha Afrika katika Human Rights Watch, pia walichangia kwenye ripoti hii. Stephen Leonelli na George Ayala wa MPact Global Action walihusika kama wahakiki wa nje ya shirika, kama vile walivyofanya baadhi ya wanaharakati wa wana-LGBT Tanzania.

Anjelica Jarrett, Mratibu wa Programu ya haki za LGBT alichangia kwa usaidizi wa uandishi. Fitzroy Hepkins, meneja mkuu wa utawala, na Jose Martinez, afisa wa utawala, pia walitoa usaidizi kwa uchapishaji.

Human Rights Watch inawatambua na kuwashukuru watu wa LGBT kutoka Tanzania ambao walitusimulia simulizi zao, na pia wanaharakati wengi wa LGBT wa Kitanzania na kikanda, wanaharakati wa haki za binadamu, na wanasheria ambao walitoa maoni muhimu kwa masuala yanayohusu ripoti hii.

 

Faharasa

 

Jinsia Asilia: Utambulisho wa kijinsia wa mtu ambao unaendana na jinsia aliyozaliwa nayo au anayojitambulisha nayo na ambayo anaishi nayo.

Jinsia: Mfumo wa kijamii na kitamaduni (ambao ni tofauti na jinsia aliyopewa mtu wakati wa kuzaliwa) unaotumika kutofautisha mtazamo wa jamii juu ya “Uuke” na “Uume.”

Jamii ya Walio Wachache Kingono na Kijinsia: Neno linalojumuisha watu walio na utata wa tambulisho wa kingono na kijinsia.

LGBT: Wanawake wanaovutiwa kimapenzi na wanawake wengine, wanaume wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wengine, wanaovutiwa kimapenzi na jinsia zote, na wabadili jinsia wa kike/kiume [lesbian, gay, bisexual and transgender]; ni neno jumulishi kwa makundi na utambulisho ambao mara nyingine hujumuishwa kama “watu walio wachache kingono na kijinsia.”

Makundi Maalum: Makundi ambayo yameathirika zaidi na VVU yakilinganishwa na jamii kiujumla, bila kujali aina ya janga ama muktadha wa eneo. Shirika la Afya Duniani linaeleza makundi maalum kama wanaume wanaoshiriki ngono na wanaume, wafanyakazi wa ngono, wanaojidunga madawa ya kulevya, wafungwa walioko magerezani, na wengine walio katika maeneo yaliyodhibitiwa, na wabadili jinsia.

Makundi Maalumu na yaliyo Hatarini: Makundi maalum na wengine ambao hali zao zinawafanya wawe hatarini au ambao wanapitia ukandamizaji, ubaguzi, kutengwa na vikwazo kijamii, kiuchumi, kitamaduni na kunyimwa haki nyingine. Nchini Tanzania ‘Makundi yaliyo hatarini” mara nyingi hutumika kumaanisha haki za wasichana wanaobalehe, watoto mayatima, watoto wanaoishi mitaani na jamii za wachimba migodi na wavuvi.

Muonekano wa Kijinsia: Sifa na tabia za nje ambazo jamii inazitambua kama za “kike” “jinsia mseto” ama “kiume” kujumuisha sifa kama za mavazi, muonekano, tabia, mtindo wa nywele, jinsi ya kuongea na tabia na muingiliano wa kijamii.

Mwelekeo wa Kijinsia: Jinsi mtu anavyoelezea mvuto wake wa kingono na kimapenzi. Neno hili linaelezea jinsi mtu anavutiwa kimsingi na watu wa jinsia moja ama jinsia tofauti, au jinsia zote mbili au kutovutiwa na jinsia yoyote.

Mtu Mwenye Jinsia Tofauti na Asili/Mbadili Jinsia: Utambulisho wa mtu ambaye jinsia yake ya kuzaliwa (ambayo alipewa alipozaliwa) hauwiani na jinsia anayoishi au jinsia anayoidhania (jinsia ambayo anaridhia zaidi kujitambulishwa kwayo au angependa kujitambulisha angepewa fursa hiyo). Mtu anayetamani kubadili jinsia yake kwa kawaida huchukua au angependa kuchukua utambulisho wa kijinsia unaowiana na jinsia anayoipendelea, lakini anaweza kutamani au asitamani kubadilisha mwili wake ili ulingane na jinsia anayotamani kuchukua.

Mwanaume asiye na jinsia ya asili: Mtu ambae alizaliwa kama mwanawake lakini anajitambulisha ama kujieleza kama mwanaume. Mwanaume asiye na jinsia asili kiujumla huelezewa kwa viwakilishi vya kiume. 

Mwanamke asiye na jinsia ya asili: Mtu ambae alizaliwa kama mwanaume lakini anajitambulisha ama kujieleza kama mwanamke. Mwanamke asiye na jinsia asili kiujumla huelezewa kwa viwakilishi vya kike.

Utambulisho wa Kijinsia: Hisia za ndani za mtu binafsi, kuwa na hisia zaidi kwamba yeye ni wa kike au kiume au vyote viwili, au kuwa na hisia kiumbe kingine ila cha kike au kiume.

Vituo vya Msaada: Nchini Tanzania, vituo vinavyotoa huduma za kiafya kwa makundi maalumu kwa msisitizo wa huduma zinazohusiana na Virusi vya Ukimwi na afya ya masuala ya ngono, Ikijumuisha kujikinga na virusi vya Ukimwi, Upimaji, Matibabu, Ushauri nasaha, Sindano na mabomba ya sindano na uhamasishaji kuhusu vifaa vya ngono salama.

Wanaovutiwa na jinsia zote: Utambulisho wa kijinsia kwa mtu ambaye anavutiwa kingono na kimapenzi na jinsia zote.

Wanaume wanaoshiriki ngono na wanaume: Wanaume wanaoshiriki katika matendo ya ngono na wanaume wenzao lakini ambao huenda wanaweza kujitambulisha au wasijitambulishe kama “kuchu”, “mashoga” au “wanashiriki ngono na jinsia moja” ama “kushiriki ngono na jinsia zote”. Mara nyingine wanatambulika kwa kifupi kutumia herufi MSM [men who have sex with men].

 

 

[1] Kikundi Kazi cha Makundi Maalumu na Waliowachahe Kiulekeo wa Mapenzi, “United Republic of Tanzania, Joint Stakeholder Submission to the United Nations, Universal Periodic Review, For 25th session Aprili –Mei 2016,” 2016, https://www.upr-info.org/sites/default/files/document/tanzania_united_republic_of/session_25_-_may_2016/js8_upr25_tza_e_main.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[2] Baraza la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu, Kikundi Kazi cha mapitio ya Ulimwengu ya Msimu, “Draft report of the Working Group on the Universal Periodic Review, United Republic of Tanzania,” https://www.upr-info.org/sites/default/files/document/tanzania_united_republic_of/session_25_-_may_2016/a-hrc-wg.6-25-l.9.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019). Mapendekezo yalitoka kwa Sweden, Uruguay, Chile, Canada, Ufaransa, na Norway.

[3] Ibid.

[4] “Tanzanian TV Station in Trouble for Hosting Gay Man,” Kuchu Times, Julai 6, 2016, https://www.kuchutimes.com/2016/07/tanzanian-tv-station-in-trouble-for-hosting-gay-man (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[5] Ibid.

[6] Ayo TV, “Vitu Vitatu Ambavyo Vimepigwa Marufuku na RC Paul Makonda,” Julai 7, 2016, filamu ya video, YouTube, https://www.youtube.com/watch?v=_1eKbNrkwrk&app=desktop (imepitiwa Disemba 16, 2019), 5:48-6:53.

[7] “Clouds TV Yaamriwa kuomba radhi kwa kurusha mahojiano na shoga,” IBN TV, Julai 9, 2016, http://www.ibn-tv.com/sw/2016/07/clouds-tv-ordered-to-run-apologies-on-gay-interview (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[8] Hotuba ya awali ilirushwa kupitia https://www.youtube.com/watch?v=TSPZfW1AG-U, na ikawekwa katika maandishi na Human Rights Watch, lakini haipo tena wakati wa uandishi wa ripoti hiii. Angalia pia “Waziri Ummy Mwalimu apiga marufuku hospitali na vituo vya afya vya serikali kutoa vilainishi vya kusaidia kufanya mapenzi ya jinsia moja,” post to “Karagwe Forum” (blog), Julai 16, 2016, http://juhudkaragwe.blogspot.com/2016/07/waziri-ummy-mwalimu-apiga-marufuku.html.

[9] “Tamko La Wizara Kuhusu Matumizi Na Usambazaji Wa Vilainishi Kwa Ajili Ya Udhibiti Wa Maambukizi Ya Ukimwi,” iliwekwa “Harakati Za Jiji” (blog), Julai 19, 2016, https://harakatizajiji.blogspot.com/2016/07/tamko-la-wizara-kuhusu-matumizi-na.html (imepitiwa Disemba 18, 2019).

[10] Chapisho la Twitter la Hamisi Kigwangalla, Julai 23, 2016, https://twitter.com/HKigwangalla/status/756724742653087744 na https://twitter.com/HKigwangalla/status/756723329063608321 (imepitiwa Disemba 18, 2019).

[11] “Serikali kuzifutia usajili asasi zisizokuwa za kiserikali zinazounga mkono ushoga nchini,” ITV, Julai 29, 2016, iliwekwa mwanzoni https://www.itv.co.tz/news/local/1993-33856/Serikali_kuzifutia_usajili_na_kuzishtaki_asasi_zisizokuwa_za_kiserikali_zinazounga_mkono_ushoga_nchini.html?fbclid=IwAR3bJJmV27tJd3yQZG4xSe7ggl-IEcoGDtInBjUbUgl7oIegkZAfnsIHhF8 (haionekani tena) ilinukuliwa kwenye Facebook ya Human Life International, https://www.facebook.com/HumanLifeInternational/posts/10155216627528569 (imepitiwa Disemba 17, 2019); ilichapishwa tena na Donatila, chapisho kwa “Jamii Forums” (blog), Julai 30, 2019, https://www.jamiiforums.com/threads/serikali-kuzifutia-usajili-asasi-zisizokuwa-za-kiserikali-zinazounga-mkono-ushoga-nchini.1088295 (imepitiwa Disemba 17, 2019). Angalia pia Sophie Tremblay, “‘Seeds of Hate’ Sown as Tanzania Starts LGBT Crackdown,”Guardian, Agosti 8, 2016, https://www.theguardian.com/world/2016/aug/08/seeds-of-hate-sown-as-tanzania-starts-lgbt-crackdown (Imepitiwa Disemba 17, 2019).

[12] Affidavit of John Kashiha, Miscellaneous Civil Application No. 64 of 2016, Tanzanian High Court (Main Registry), Dar es Salaam, aya ya 7 (ipo katika file la Human Rights Watch).

[13] “Tamko la Mhe. Dkt. Hamisi A. Kigwangalla (MB.) Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Kuhusu LGBT Voice Tanzania Tarehe 11/08/2016,” ilichapishwa katika “Mwanahalisi Forum” (blogu), Agosti11, 2016, http://mwanahalisiforum.com/threads/11735-DR-KIGWANGALLA-LGBT-VOICE-TANZANIA-WANAHAMASISHA-MAPENZI-YA-JINSIA-MOJA (imepitiwa Disemba 17, 2019); Jamii Forums, “N/Waziri Dr. Kigwangalla: LGBT Voice Tanzania wanahamasisha mapenzi ya jinsia moja, wajisalimishe,” imetupiwa Agosti 12, 2016, kipande cha video, YouTube, youtube.com/watch?v=xunWjepnydk (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[14] Mawasiliano ya barua pepe ya Human Rights Watch na mwanaharakati wa haki za LGBT wa kanda, Agosti 16, 2016.

[15] Affidavit of John Kashiha, Miscellaneous Civil Application No. 64 of 2016, Tanzanian High Court (Main Registry), Dar es Salaam, aya ya 7-13 (ipo kwenye faili la Human Rights Watch).

[16] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, “Tamko la Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Mhe. Ummy Mwalimu juu ya Huduma za UKIMWI kwa Makundi Maalum Tanzania, 27 Oktoba, 2016,” ipo kwenye faili la Human Rights Watch na inapatikana pia katika https://m.facebook.com/afyatz/posts/1230922863594845 (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[17] Mawasiliano ya barua pepe ya Human Rights Watch na wanaharakati na wanasheria wa Tanzania na Kenya, Disemba 14 na 18, 2016; Andrew Green, “In an Apparent Crackdown, Tanzania Government Raids NGO Meeting on Reproductive Rights,” Devex, Januari 6, 2017, https://www.devex.com/news/in-an-apparent-crackdown-tanzania-government-raids-ngo-meeting-on-reproductive-rights-89394 (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[18] Mahojiano ya simu ya Human Rights Watch na wanaharakati wa Kitanzania, Januari 2017; Edith Honan, “How Tanzania is Cracking Down on Gay People – and Getting Away with it,” BuzzFeed News, Aprili 8, 2017, https://www.buzzfeednews.com/article/edithhonan/how-tanzania-is-cracking-down-on-lgbt-people-and-getting (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[19] Ibid.

[20] Mahojiano ya Human Rights Watch na Dixon (jina bandia), Dar es Salaam, Machi 14, 2017.

[21] Ujumbe wa Twitter wa Hamisi Kigwangalla, Februari 6, 2017, https://twitter.com/HKigwangalla/status/828651474406215680?s=20 (imepitiwa Disemba 17, 2019); “Tanzania Orders Arrest of Three Men for Promoting Homosexuality,” NBC News, Februari 8, 2017, https://www.nbcnews.com/feature/nbc-out/tanzania-orders-arrest-three-men-promoting-homosexuality-n718491 (imepitiwa Disemba 17, 2019); Sharifa Marira, “Polisi Dar yaanza msako wa mashoga,” post to “Jambo Leo” (blog), Februari 2017, http://jambo-leo.blogspot.com/2017/02/polisi-dar-yaanza-msako-wa-mashoga.html (imepitiwa Disemba, 2019).

[22] Mahojiano ya simu ya Human Rights Watch na Johnnie D (jina bandia), Aprili 27, 2017.

[23] Rahma Suleiman, “Polisi Zanzibar yanasa wanaodaiwa kuwa mashoga,” IPP Media, Machi 4, 2017, https://www.ippmedia.com/sw/habari/polisi-zanzibar-yanasa-wanaodaiwa-kuwa-mashoga (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[24] Madina Issa, “Ayoub azionya NGO’s zinazohamasisha ushoga,” Zanzibar Leo, Machi 6, 2017, https://zanzibarleo.co.tz/2017/03/06/ayoub-azionya-ngos-zinazohamasisha-ushoga/ (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[25] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Tanzania Bara, “National Guideline for Comprehensive Package of HIV Interventions for Key Populations,” Second Edition, Aprili 2017, https://hivpreventioncoalition.unaids.org/wp-content/uploads/2018/03/Tanzania-KP-GUIDELINE-1.pdf (Imepitiwa Disemba 17, 2019).

[26] Global TV Online, “Rais Magufuli Apigilia Msumari Wanafunzi Kupata Mimba, Hakuna Kurudi Shule, Wanaume Jela Miaka 30,” Juni 22, 2017, kipande cha video, YouTube, https://www.youtube.com/watch?v=1EWGwQk6NqU (imepitiwa Disemba 17, 2019), 36:30.

[27] “Mwigulu Nchemba aibua vita ya ushoga,” EATV, Juni 27, 2019, https://www.eatv.tv/news/current-affairs/mwigulu-nchemba-aibua-vita-ya-ushoga (imepitiwa Disemba 17, 2019); Tim Teeman, “Mr. President, Cows Are Not Homophobic: Inside Tanzania’s LGBT Crackdown,” The Daily Beast, Juni 28, 2017, https://www.thedailybeast.com/mr-president-cows-are-not-homophobic-inside-tanzanias-lgbt-crackdown (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[28] Mawasiliano ya barua pepe kati ya Human Rights Watch na mtetezi wa haki za binadamu Zanzibar, Oktoba 24, 2019; University of Pretoria Center for Human Rights and Pan Africa ILGA , “Taarifa kwa Vyombo vya Habari: Centre for Human Rights and Pan Africa ILGA Express Grave Concern About Threats to the Right to Freedom of Association and Right to Information as Twenty are Arrested at Training Workshop in Zanzibar, Tanzania for Alleged Homosexuality,” Septemba 20, 2017, https://www.chr.up.ac.za/news-archive/1225-press-statement-centre-for-human-rights-and-pan-africa-ilga-express-grave-concern-about-threats-to-the-right-to-freedom-of-association-and-right-to-information-as-twenty-are-arrested-at-training-workshop-in-zanzibar-tanzania-for-alleged-homosexuality (imepitiwa Disemba 18, 2019).

[29] Peter Nyanje na Kate Bartlett, “Tanzania Police Vow to ‘Hunt’ Down Gays After Making 20 Arrests,” DPA, Septemba 18, 2017, https://www.africanindy.com/news/tanzania-police-vow-to-hunt-down-gays-after-making-20-arrests-11263659 (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[30] Wendy Isaack, “Facing Prosecution for Challenging HIV Policies in Tanzania,” andiko la Human Rights Watch, Oktoba 20, 2017, https://www.hrw.org/news/2017/10/20/facing-prosecution-challenging-hiv-policies-tanzania.

[31] Wizara wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Watoto na Wazee , “Taarifa Kwa Umma,” imetiwa saini na M.S. Katemba, msajili wa NGO, https://www.jamiiforums.com/mobile-gallery/5714701aa3c7d542fb90b4ae332eac22.jpg (imepitiwa Disemba 18, 2019).

[32] Judith Nyange, “kesi ya mapenzi ya jinsia moja yapigwa kalenda,” Mtanzania, Januari 9, 2018, ipo katika faili la Human Rights Watch; Mawasiliano ya barua pepe ya Human Rights Watch na mwanasheria wa Kitanzania, Septemba 25, 2018.

[33] “Tanzania: ‘Dangerous’ Plans for Homophobic Task Force Must be Abandoned Immediately,” taarifa ya Amnesty International kwa vyombo vya habari, Novemba 1, 2018, https://www.amnesty.org/en/latest/news/2018/11/tanzania-dangerous-plans-for-homophobic-task-force-must-be-abandoned-immediately (imepitiwa Disemba 18, 2019).

[34] “RC Makonda akitangaza kamati itakayotokomeza mashoga,” Oktoba 31, 2018, video, YouTube, mkutano na waandishi wa habari, https://www.youtube.com/watch?v=ZFzhwL7HggA&feature=youtu.be (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[35] “Tanzania: 10 Men Arrested in Zanzibar for Being ‘Gay,’” taarifa ya Amnesty International kwa vyombo vya habari, Novemba 6, 2018, https://www.amnesty.org/en/latest/news/2018/11/tanzania-10-men-arrested-in-zanzibar-for-being-gay (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[36] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, “Taarifa kwa Vyombo vya Habari” (Taarifa kwa Vyombo vya Habari) Dodoma, Novemba 4, 2018, https://www.bbc.com/swahili/habari-46093978 (imepitiwa Julai 21, 2019), na ipo katika faili la Human Rights Watch.

[37] Mawasiliano ya barua pepe ya Human Rights Watch na mwanadiplomasia Tanzania, Disemba 16, 2019; Christina Finn, “Diplomatic Pressure Results in Tanzania Stating Anti-Gay Crackdown is Not Government Policy,” The Journal (Ireland), Novemba 6, 2018, https://www.thejournal.ie/tanzania-lgbt-arrests-4326426-Nov2018 (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[38] Tangazo liliwekwa: https://wbappse.worldbank.org/WBG_BPC_1818SOCIETY_RSSFEEDAPPWEB/announcements/announcementresources# na kuangaliwa na Human Rights Watch lakini haipo tena katika andiko hilo. Angalia pia Hillary Orinde, “Unsafe place? World Bank Cancels Missions to Tanzania,” Standard Digital (Nairobi), Novemba 9, 2018, https://www.standardmedia.co.ke/article/2001302127/world-bank-suspends-funding-to-tanzania (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[39] “Danmark tilbageholder millioner til Tanzania for homofobi,” DR (Denmark), Novemba 14, 2018, https://www.dr.dk/nyheder/politik/danmark-tilbageholder-millioner-til-tanzania-homofobi (imepitiwa Disemba 17, 2019), tafsiri ya Kiingereza isiyo rasmi inapatikana https://www.jamiiforums.com/threads/denmark-withholds-aid-and-cancels-minister-visit-to-tanzania-over-human-rights-situation.1508470 (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[40] Alex Malanga, “Mahiga: Denmark’s Aid Intact,” The Citizen (Dar es Salaam), Novemba 30, 2018, https://www.thecitizen.co.tz/News/Mahiga--Denmark-s-aid-intact/1840340-4875198-68ftm2/index.html (imepitiwa Disemba 17, 2019); mawasiliano ya barua pepe ya Human Rights Watch na Susanne Branner Jespersen, LGBT Denmark, Disemba 4, 2018.

[41] “World Bank Statement on Lifting the Suspension of Missions to Tanzania,” Taarifa kwa Vyombo vya Habari ya Benki ya Dunia, Novemba 19, 2018, https://www.worldbank.org/en/news/statement/2018/11/20/world-bank-statement-on-lifting-the-suspension-of-missions-to-tanzania (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[42] Mahojiano na mawasiliano ya barua pepe ya Human Rights Watch na mmoja wa waliokamatwa, balozi zilizopo Tanzania na mashirika ya kimataifa, Machi 2019.

[43] Mahojiano ya simu ya Human Rights Watch na Stephen Leonelli, MPact, Septemba 19, 2019.

[44] “Tanzania: Board Revokes Six NGOs’ License,” The Citizen (Dar es Salaam), Aprili 19, 2019, https://www.thecitizen.co.tz/news/Tanzania--Board-revokes-six-NGOs--license/1840340-5079110-fhy0cl/index.html (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[45] MPact, “Prohibit Forced Anal Examinations Now! Petition to Government of Tanzania,” April 2019, https://mpactglobal.org/civil-society-petition-regarding-forced-anal-exams-in-tanzania (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[46] “Hamad Masauni: Waziri ataka wapenzi wa jinsia moja kukamatwa Zanzibar,” BBC News Online, Septemba 20, 2019, https://www.bbc.com/swahili/habari-49773733 (imepitiwa Disemba 17, 2019); KTV TZ Online, “‘POLISI KAMATENI WANAOJIHUSISHA NA USHOGA ZANZIBAR’ – MASAUNI,” imewekwa mtandaoni Septemba 21, 2019, video, YouTube, https://www.youtube.com/watch?v=8CCOsQw3UbQ (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[47] Tanganyika ilitawaliwa kikoloni na Ujerumani tangu mwaka 1880 hadi 1918, wakati Zanzibar ikiwa chini ya uangalizi wa Kiingereza. Baada ya Vita ya Kwanza ya Dunia, mwaka 1919, chini ya Umoja wa Mataifa, Tanganyika akwa chini ya Uingereza. Wakati wa uhuru mwaka 1961, nchi hizo mbili ziliungana na kutengeneza Tanzania ya leo, huku Zanzibar ikiwa na mamlaka yake kwa kiasi fulani.

[48] Human Rights Watch na WASO, “Tuchukulie kama Binadamu”: Ubaguzi dhidi ya Wafanyabiashara wa ngono, Wachache katika kundi la kijinsia na Ngono, na Watumiaji wa Dawa za Kulevya Tanzania, Juni 18, 2013, https://www.hrw.org/report/2013/06/18/treat-us-human-beings/discrimination-against-sex-workers-sexual-and-gender.

[49] Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa, Working Group on Universal Periodic Review, “Draft Report of the Working Group on the Universal Periodic Review, United Republic of Tanzania,” aya 137.66.

[50] “Tanzania’s Magufuli Sacks Officials Who Failed to Recall Public Works Budget Figures,” Reuters, Novemba 7, 2017, https://www.reuters.com/article/us-tanzania-politics/tanzanias-magufuli-sacks-officials-who-failed-to-recall-public-works-budget-figures-idUSKBN1D70E7 (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[51] “Tanzania Arrests 500 ‘Sex Workers,’” BBC News Online, Machi 13, 2016, https://www.bbc.com/news/world-africa-35815997 (imepitiwa Disemba 17, 2019); Global Network of Sex Work Projects, “Tanzanian Sex Workers and Clients Face Mass Arrest and Criminalisation,” Juni 12, 2017, https://www.nswp.org/news/tanzanian-sex-workers-and-clients-face-mass-arrest-and-criminalisation (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[52] Jared Jeffrey, “Op-Ed: Does Tanzania’s Magufuli Dare to Take on the Church?” CNBC Africa, Aprili 7, 2018, https://www.cnbcafrica.com/news/east-africa/2018/04/07/oped-tanzanias-president-john-magufuli-dare-take-church (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[53] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Na. 3 ya 2019, The Written Laws (Miscellaneous Amendments) Act, 2019, http://www.tnnc.go.tz/documents/THE_WRITTEN_LAWS_MISCELLENEOUS_NO.3_ACT_OF_2019__.pdf (imepitiwa Disemba 18, 2019); “Tanzanian Civil Society Rattled by Bill That Restricts Freedoms,” The East African, Juni 21, 2019, https://www.theeastafrican.co.ke/news/ea/Tanzania-amendment-Bill/4552908-5167054-9j08l0/index.html (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[54] Non-Governmental Organizations Act (Regulations), Government Notice No. 609 of 2018, http://www.mcdgc.go.tz/data/GN_609_NGOs_ACT_AMENDMENTS.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019), reg. 12.

[55] Human Rights Watch, “Ukimya wangu, Usalama Wangu”: Vitisho kwa Vyombo vya Habari na Asasi za Kiraia Tanzania, Oktoba 28, 2019, https://www.hrw.org/report/2019/10/28/long-i-am-quiet-i-am-safe/threats-independent-media-and-civil-society-tanzania, p. 24.

[56] Front Line Defenders, “Bibiana Mushi Acquitted,” Novemba 2, 2017, https://www.frontlinedefenders.org/en/case/judicial-harassment-two-human-rights-defenders-0 (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[57] Human Rights Watch, “Ukimya Wangu, Usalama Wangu,” uk. 21-23; Zaheena Rashid, “Tanzania Daima Ban Adds to Press Freedom Concerns,” Al Jazeera, Oktoba 26, 2017, https://www.aljazeera.com/news/2017/10/tanzania-daima-ban-adds-press-freedom-concerns-171025181519339.html (imepitiwa Disemba 17, 2019); Legal and Human Rights Centre, “Human Rights Situation Report. January – June 2018,” Agosti 2018, https://www.humanrights.or.tz/assets/images/upload/files/Mid-Year%20Human%20Rights%20Report%202018(2).pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019), p. 33; “Tanzania Authorities Cite Bias in Banning of Major English Newspaper,” taarifa ya Human Rights Watch kwa vyombo vya habari, Machi 6, 2019, https://www.hrw.org/news/2019/03/06/tanzania-authorities-cite-bias-banning-major-english-newspaper.

[58] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Sitta Tuuma, mwandishi, Mwanza, Septemba 11, 2018; “Opposition MP Matiko Held For ‘Unlawful Assembly’ in Tarime,” IPP Media, Agosti 10, 2018, https://www.ippmedia.com/en/news/opposition-mp-matiko-held-%E2%80%98unlawful-assembly%E2%80%99-tarime (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[59] Amnesty International, The Price We Pay: Targeted for Dissent by the Tanzanian State, Oktoba 28, 2019, https://www.amnesty.org/en/documents/afr56/0301/2019/en/, imepitiwa Disemba 17, 2019, uk. 29-31.

[60] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Sheria ya Vyama vya Siasa (Marekebisho), Februari 22, 2019, http://www.sol.udsm.ac.tz/images/Mypdf/Politicalparties.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019); Fumbuka Ng'wanakilala, “Tanzania MPs Grant Government Sweeping Powers Over Political Parties,” Reuters, Januari 30, 2019, https://www.reuters.com/article/us-tanzania-politics/tanzania-mps-grant-government-sweeping-powers-over-political-parties-idUSKCN1PO0IA (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[61] Human Rights Watch, “Ukimya Wangu, Usalama Wangu” uk. 42-45.

[62] Angalia pia kwa mfano, Jacob William Kahemele, “The Sanctioned Emotional, Physical and Sexual Abuse of Children in Tanzania,” Child Research Net, Mei 14, 2014, https://www.childresearch.net/papers/rights/2014_08.html (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[63] Emmanuel Muga, “Dar Plans to Introduce Tougher Anti-Gay Bill,” The East African, Machi 29, 2014, https://www.theeastafrican.co.ke/news/ea/Dar-plans-to-introduce-tougher-anti-gay-Bill--/4552908-2262374-format-xhtml-85bcn8/index.html (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[64] “Tanzania’s Blood Ivory: ‘This is Madness Now,’” CNN, Februari 13, 2014, http://amanpour.blogs.cnn.com/2014/02/13/tanzanias-blood-ivory-this-is-madness-now (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[65] Pamoja na jitihada zingine, TACAIDS walimwalika shoga asiyejificha kuzungumza na Kamati ya Bunge ya Kudumu ya VVU/UKIMWI Dodoma mwaka 2014 kuhusu haja ya kukomesha ukatili na ubaguzi ili kumaliza VVU. Katika kikao hicho na wabunge, Human Rights Watch walizungumzia matokeo ya utafiti wao wa 2013 wa pamoja na mtandao wa WASO juu ya ubaguzi dhidi ya makundi maalum na kupendekeza hatua za kupunguza ukatili wa polisi na ubaguzi katika sekta ya afya.

[66] Mahojiano kwa njia ya simu ya Human Rights Watch na Anna Maembe, katibu mkuu, Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Juni 12, 2014.

[67] Mahojiano kwa njia ya simu ya Human Rights Watch na John Kashiha, Dar es Salaam Mei 5, 2014. Human Rights Watch waliiangalia barua ya kufutiwa usajili, iliyosainiwa na Msajili wa wakati huo Marcel Katemba kwa niaba ya katibu mkuu.

[68] “Serikali Kuzifutia Usajili Asasi Zisizokuwa Za Kiserikali Zinazounga Mkono Ushoga Nchini,” ITV, ilichapishwa kwanza katika https://www.itv.co.tz/news/local/1993-33856/Serikali_kuzifutia_usajili_na_kuzishtaki_asasi_zisizokuwa_za_kiserikali_zinazounga_mkono_ushoga_nchini.html?fbclid=IwAR3bJJmV27tJd3yQZG4xSe7ggl-IEcoGDtInBjUbUgl7oIegkZAfnsIHhF8 (haionekani tena) na kuwekwa pia katika ukurasa wa Facebook wa Human Life International, https://www.facebook.com/HumanLifeInternational/posts/10155216627528569; reprinted by Donatila, post to “Jamii Forums” (blog), https://www.jamiiforums.com/threads/serikali-kuzifutia-usajili-asasi-zisizokuwa-za-kiserikali-zinazounga-mkono-ushoga-nchini.1088295. Angalia pia Sophie Tremblay, “‘Seeds of Hate’ Sown as Tanzania Starts LGBT Crackdown,” Guardian, https://www.theguardian.com/world/2016/aug/08/seeds-of-hate-sown-as-tanzania-starts-lgbt-crackdown.

[69] Global TV Online “Rais Magufuli Apigilia Msumari Wanafunzi Kupata Mimba, Hakuna Kurudi Shule, Wanaume Jela Miaka 30,” https://www.youtube.com/watch?v=1EWGwQk6NqU, 36:30. Magufuli alinukuliwa kimakosa katika baadhi ya vyombo vya habari vya Kiingereza kwamba alisema hata ng’ombe “hawayakubali” mapenzi ya jinsia moja; angalia pia Tim Teeman, “Mr. President, Cows Are Not Homophobic: Inside Tanzania’s LGBT Crackdown,” The Daily Beast, https://www.thedailybeast.com/mr-president-cows-are-not-homophobic-inside-tanzanias-lgbt-crackdown.

[70] Ken Roth, “World’s Autocrats Face Rising Resistance,” Human Rights Watch World Report 2019 (New York: Human Rights Watch, 2019), https://www.hrw.org/world-report/2019/keynote/autocrats-face-rising-resistance.

[71] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Elizabeth (jina bandia), Disemba 2016.

[72] Kwa mfano, wakati Paul Makonda alipotishia kuwakamata wanaume wote wanaovutiwa kimapenzi na wanaume wengine Tanzania, ni mwanaharakati maarufu mmoja tu wa Tanzania, Fatma Karume, rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanzania, aliyepaza sauti na kukemea mashambulizi yake (Makonda). Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na wanaharakati wa wana-LGBT wa Kitanzania, Novemba 2018.

[73] Sheria za Tanzania, Sura ya 16, Kanuni ya Adhabu, http://www.lrct.go.tz/?wpfb_dl=170 (imepitiwa Disemba 19, 2019),

Vipengele vya. 154, 155.

[74] Sheria za Tanzania, Sura ya 16, Kanuni ya Adhabu, http://www.lrct.go.tz/?wpfb_dl=170, vipengele. 157, 138A; Human Dignity Trust, “Tanzania,” https://www.humandignitytrust.org/country-profile/tanzania/ (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[75] Sheria Namba 6 ya Kanuni ya Adhabu ya Zanzibar ya mwaka 2004, http://defensewiki.ibj.org/images/9/90/Zanzibar_Penal_Code.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019), vipengele. 150, 154, 158.

[76] Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya 1977, iliyorekebishwa 2005, https://www.wipo.int/edocs/lexdocs/laws/en/tz/tz008en.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019), ibara 9, 13.

[77] Mahojiano kwa njia ya simu ya Human Rights Watch na wanaharakati wa Tanzania, Julai 2016. Kaoge, ambaye pia ameelezewa katika vyombo vya habari kwa jina lake la kuzaliwa, Godfrey Majunga, alifariki kwa ugonjwa unaohusiana na UKIMWI Novemba 8, 2019.

[78] “Tanzanian TV Station in Trouble for Hosting Gay Man,” Kuchu Times, https://www.kuchutimes.com/2016/07/tanzanian-tv-station-in-trouble-for-hosting-gay-man.

[79] Ayo TV, “Mambo Yaliyopigwa Marufuku na RC Paul Makonda,” https://www.youtube.com/watch?v=_1eKbNrkwrk&app=desktop, 5:48-6:53.

[80] “Tanzanian TV Station in Trouble for Hosting Gay Man,” Kuchu Times, https://www.kuchutimes.com/2016/07/tanzanian-tv-station-in-trouble-for-hosting-gay-man; “Clouds TV Ordered to Run Apologies on Gay Interview,” IBN TV, http://www.ibn-tv.com/sw/2016/07/clouds-tv-ordered-to-run-apologies-on-gay-interview; Edith Honan, “How Tanzania is Cracking Down on Gay People – and Getting Away With It,” BuzzFeed News, https://www.buzzfeednews.com/article/edithhonan/how-tanzania-is-cracking-down-on-lgbt-people-and-getting.

[81] Hotuba halisi ilichapishwa https://www.youtube.com/watch?v=TSPZfW1AG-U, na kunakiliwa na Human Rights Watch, lakini haipatikani tena hadi kuandikwa kwa ripoti hii. Angalia pia “Waziri Ummy Mwalimu apiga marufuku hospitali na vituo vya afya vya serikali kutoa vilainishi vya kusaidia kufanya mapenzi ya jinsia moja,” ilichapishwa “Karagwe Forum” (blog), http://juhudkaragwe.blogspot.com/2016/07/waziri-ummy-mwalimu-apiga-marufuku.html.

[82] Shirika la Afya Duniani, “Consolidated Guidelines on HIV Prevention, Diagnosis, Treatment and Care for Key Populations: 2016 Update,” https://apps.who.int/iris/bitstream/handle/10665/246200/9789241511124-eng.pdf;jsessionid=18BD154698A96B4377976E45459674F0?sequence=1 (imepitiwa Disemba 17, 2019), p. xii.

[83] Avert, “HIV and AIDS in Tanzania,” imebadilishwa Oktoba 1, 2019, https://www.avert.org/professionals/hiv-around-world/sub-saharan-africa/tanzania (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[84] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Afya na Maendeleo ya Jamii, Programu ya Kitaifa ya Kudhibiti UKIMWI, “Consensus Estimates on Key Population Size and HIV Prevalence in Tanzania,” Julai 2014, https://www.healthpolicyproject.com/pubs/391_FORMATTEDTanzaniaKPconsensusmtgreport.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019). Utafiti uliofanywa na Chuo Kikuu cha Muhimbili mwaka 2014 uligundua kwamba maambukizi ya VVU ya asilimia 22.3 miongoni mwa wanaume wanaofanya ngono na wanaume jijini Dar es Salaam. Elia John Mmbaga et al., “Hiv Prevalence and Associated Risk Factors Among Men Who Have Sex with Men in Dar Es Salaam, Tanzania,” Journal of Acquired Immune Deficiency Syndromes, 2017, imepitiwa Disemba 17, 2019, doi:10.1097/QAI.0000000000001593.

[85] UNAIDS Country Factsheets, “United Republic of Tanzania,” 2018, https://www.unaids.org/en/regionscountries/countries/unitedrepublicoftanzania (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[86] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, “Global AIDS Response Country Progress Update,” Machi 31, 2014, https://www.unaids.org/sites/default/files/country/documents/TZA_narrative_report_2014.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[87] Shirika la Afya Duniani, Policy Brief, Transgender People and HIV, Julai 2015, https://apps.who.int/iris/bitstream/handle/10665/179517/WHO_HIV_2015.17_eng.pdf (imepitiwa Disemba 19, 2019), p. 7.

[88] Stefan D. Baral, “Worldwide Burden of HIV in Transgender Women: A Systematic Review and Meta-Analysis,” The Lancet 13 (2013), imepitiwa Disemba 17, 2019, doi:10.1016/ S1473-3099(12)70315-8.

[89] Mfuko wa Kimataifa wa Kupambana na UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria, “Tanzania Joint TB and HIV Concept Note,” 2014, uk. 68, ipo katika faili la Human Rights Watch. Uzuiaji wa VVU unaolenga jamii kiujumla, ambao hauzingatii mahitaji na tabia maalum ya vikundi kama vile wanaume wanaofanya ngono na wanaume wenzao na wabadilishi jinsia, unaweza kutofanikiwa; kama Human Rights Watch na WASO walipata katika ripoti yetu ya 2013, wanaume kadhaa waliohojiwa hawakujua kuwa wanaweza kuambukizwa VVU kupitia ngono ya mkundu. Human Rights Watch na WASO, “Tuchukilie kama Binadamu,”  uk. 22.

[90] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Global AIDS Response Country Progress Report, https://www.unaids.org/sites/default/files/country/documents/TZA_narrative_report_2014.pdf, p. 8. Takwimu za hivi karibuni zaidi hazipatikani.

[91] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ofisi ya Waziri Mkuu, “The Second National Multi-Sectoral Strategic Framework on HIV and AIDS (2008-2012),” Oktoba 2007, https://www.ilo.org/wcmsp5/groups/public/---ed_protect/---protrav/---ilo_aids/documents/legaldocument/wcms_125595.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019), uk. 57; Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ofisi ya Waziri Mkuu, “Tanzania Third National Multi-Sectoral Framework for HIV and AIDS (2013/2014-2017/2018),” Novemba 2013, http://www.nationalplanningcycles.org/sites/default/files/country_docs/Tanzania/nmsf-iii_eng_final_report_2013mail.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019); Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Tanzania Bara, “National Guideline for Comprehensive Package of HIV Interventions for Key Populations,” Septemba 2014, https://www.hivsharespace.net/sites/default/files/resources/7.%202014%20Tanzania_KP_Comprehencive_Guideline_sept_29th_2014%20%281%29.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019). Hata chini ya uongozi wa Kikwete, baadhi ya vifaa katika mikakati hii ya afya ilikuwa na utata: wakati nakala ya Kiingereza ya Mpango Mkakati wa Taifa ya 2008-2012 hata ilitaka kuondoa ujinai katika kitendo cha ngono ya jinsia moja ya hiari, nakala ya Kiswahili iliondoa lugha hii.

[92] Mahojiano ya njia ya simu kati ya Human Rights Watch na aliyekuwa mwakilishi wa shirika la misaada, Oktoba 13, 2019.

[93] Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Makubaliano yaliyofikiwa na Mkutano Mkuu tarehe 8 Juni 2016, “Political Declaration on HIV and AIDS: On the Fast Track to Accelerating the Fight against HIV and to Ending the AIDS Epidemic by 2030,” A/RES/70/266, https://www.unaids.org/sites/default/files/media_asset/2016-political-declaration-HIV-AIDS_en.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[94] UNAIDS, “Tanzania Supports the Release of Zero Draft 2016 Political Declaration Ahead of High-Level Meeting on Ending AIDS,” Januari 13, 2017, http://rstesa.unaids.org/highlights/2017/item/20-tanzania-supports-the-release-of-zero-draft-2016-political-declaration-ahead-of-high-level-meeting-on-ending-aids (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[95] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, “Statement by the Minister for Health, Community Development, Gender, Elderly and Children. Hon. Ummy Mwalimu on Key Population HIV Services in Tanzania, 27th October, 2016,” ipo katika faili la Human Rights Watch; inapatikana pia https://m.facebook.com/afyatz/posts/1230922863594845.

[96] UNAIDS, “Guidance Note 2012: Key Programmes to Reduce Stigma and Discrimination and Increase Access to Justice in National HIV Responses,” http://files.unaids.org/en/media/unaids/contentassets/documents/document/2012/Key_Human_Rights_Programmes_en_May2012.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019); Kamisheni ya Dunia ya VVU na Sheria, Hatari, Haki, na Afya, Julai 2012, https://hivlawcommission.org/wp-content/uploads/2017/06/FinalReport-RisksRightsHealth-EN.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019), sura ya 3.3; Kamisheni ya Dunia ya VVU na Sheria, Hatari, Haki, na Afya: Jalizo, Julai 2018, https://hivlawcommission.org/wp-content/uploads/2018/09/HIV-and-the-Law-supplement-FINAL.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[97] “Taasis Kumi na Mbili za UN Zimetoa Tamko la Pamoja juu ya Haki za wana-LGBT,” Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Mjumbe wa Haki za Binadamu, Septemba 29, 2015, https://www.ohchr.org/EN/NewsEvents/Pages/DisplayNews.aspx?NewsID=16511&LangID=E (imepitiwa Disemba 19, 2019).

[98] Tume ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, UKIMWI, Sheria na Haki za Binadamu katika Mfumo wa Haki za Binadamu Afrika: Changamoto Kuu na Fursa ya Mrejesho Sahihi, isiyokuwa na tarehe, https://www.unaids.org/sites/default/files/media_asset/HIV_Law_AfricanHumanRightsSystem_en.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019), p. 87, aya. 118.

[99] Shirika la Afya Duniani, “Consolidated Guidelines on HIV Prevention, Diagnosis, Treatment and Care for Key Populations: 2016 Update,” https://apps.who.int/iris/bitstream/handle/10665/246200/9789241511124-eng.pdf;jsessionid=18BD154698A96B4377976E45459674F0?sequence=1, pp. 2-3.

[100] Haley Mahler na Audrey Weber, “A Future Without AIDS Begins and Ends with Key Populations,” FHI 360, Julai 19, 2018, https://degrees.fhi360.org/2018/07/a-future-without-aids-begins-and-ends-with-key-populations (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[101] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Toni (jina bandia), Oktoba 9, 2018.

[102] Mahojiano kwa njia ya video kati ya Human Rights Watch na Makame (jina bandia), Julai 3, 2018.

[103] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Leticia (jina bandia), Oktoba 4, 2018.

[104] UNAIDS, “Guidance Note: Condom and Lubricant Programming in High HIV Prevalence Countries,” 2014, https://www.unaids.org/sites/default/files/media_asset/condoms_guidancenote_en.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[105] Shirika la Afya Duniani, “Policy Brief: HIV Prevention, Diagnosis, Treatment and Care for Key Populations: Consolidated Guidelines,” Julai 2014, https://apps.who.int/iris/bitstream/handle/10665/128049/WHO_HIV_2014.8_eng.pdf;jsessionid=074B99A85B01F51C534F997091DC543B?sequence=1 (imepitiwa Disemba 17, 2019), kurasa: 3-4.

[106] Shirika la Afya Duniani, “Use and Procurement of Additional Lubricants for Male and Female Condoms: WHO/UNFPA/FHI360: Advisory Note,” 2012, https://apps.who.int/iris/bitstream/handle/10665/76580/WHO_RHR_12.33_eng.pdf;jsessionid=D95B2E0D1D6229BB61C68B10A61F2176?sequence=1 (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[107] Mahojiano ya Human Rights Watch na afisa wa UNFPA, Dar es Salaam, Julai 2,2012; mahojiano ya Human Rights Watch na mashirika yasiyo ya kiserikali na TCAIDS, Dar es Salaam, Mei 2014.

[108] Mahojiano ya na mtumishi wa UNAIDS na John Kashiha, Dar es Salaam, Mei 5, 2014.

[109] Mawasiliano kwa njia ya jumbe fupi za simu (SMS) na mwanaharakati aliyeshiriki katika mashtaka, Novemba 19, 2019.

[110] AIDS Accountability International, “Tanzania Civil Society Priorities Charter: An Advocacy Roadmap for the Global Fund to Fight AIDS, Tuberculosis and Malaria New Funding Model,” Mei 2014, http://www.aidsaccountability.org/wp-content/uploads/2014/02/Tanzania-Civil-Society-Priorities-Charter.pdf (imepitiwa Dicemba 17, 2019). Mtafiti was Human Rights Watch researcher alihudhuria mkutano.

[111] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Tanzania Bara, “National Guideline for Comprehensive Package of HIV Interventions for Key Populations,” https://www.hivsharespace.net/sites/default/files/resources/7.%202014%20Tanzania_KP_Comprehencive_Guideline_sept_29th_2014%20%281%29.pdf.

[112] Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mpango Mkakati wa Taifa wa Kudhibiti UVV II, (ZNSP-II), 2011-2016, https://hivhealthclearinghouse.unesco.org/sites/default/files/resources/Zanzibar_ZNSPII2011-2016.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[113] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ofisi ya Waziri Mkuu, “Tanzania Third National Multi-Sectoral Framework for HIV and AIDS (2013/2014-2017/2018),” http://www.nationalplanningcycles.org/sites/default/files/country_docs/Tanzania/nmsf-iii_eng_final_report_2013mail.pdf.

[114] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na aliyekuwa mwakilishi wa shirika la kutoa, Oktoba 13, 2019.

[115] Hotuba ya awali ilichapishwa hapa: https://www.youtube.com/watch?v=TSPZfW1AG-U, na ikanakiriwa na Human Rights Watch, lakini haipo tena wakati huu wa uandishi. Angalia pia “Waziri Ummy Mwalimu apiga marufuku hospitali na vituo vya afya vya serikali kutoa vilainishi vya kusaidia kufanya mapenzi ya jinsia moja,” post to “Karagwe Forum” (blog), http://juhudkaragwe.blogspot.com/2016/07/waziri-ummy-mwalimu-apiga-marufuku.html.

[116] “Tamko La Wizara Kuhusu Matumizi Na Usambazaji Wa Vilainishi Kwa Ajili Ya Udhibiti Wa Maambukizi Ya Ukimwi,” chapisho kwa “Harakati Za Jiji” (blog), https://harakatizajiji.blogspot.com/2016/07/tamko-la-wizara-kuhusu-matumizi-na.html.

[117] Hamisi Kigwangalla, machapisho ya Twitter, Julai 23, 2016, https://twitter.com/HKigwangalla/status/756724742653087744 and https://twitter.com/HKigwangalla/status/756723329063608321 (imepitiwa Disemba 19, 2019).

[118] Waraka huu ulichapishwa katika ukurasa binafsi wa Facebook wa Mwalimu hapa: https://www.facebook.com/Ummy-Ally-Mwalimu-1694185450859688/?fref=ts ana ulipitiwa Human Rights Watch mara kadhaa Julai na Agosti 2016. Hauonekani tena kwa umma. Picha ya chapisho la waraka ipo katika faili la Human Rights Watch; angalia Kiambatanisho IV.

[119] Mawasiliano ya barua pepe ya Human Rights Watch na mwanaharakati wa kikanda wa haki na afya, Agosti 15, 2016.

[120] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, “Statement by the Minister for Health, Community Development, Gender, Elderly and Children. Hon. Ummy Mwalimu on Key Population HIV Services in Tanzania, 27th October, 2016,” ipo katika faili la Human Rights na inapatikana pia https://m.facebook.com/afyatz/posts/1230922863594845.

[121] Kwa mfano, mahojiano kati ya Human Rights Watch na Yahya, eneo limefichwa, Juni 9, 2018; Fadil, eneo limefichwa, Januari 24, 2019; King, eneo limefichwa, Mei 21, 2018, na Medard, eneo limefichwa, Mei 18, 2018. Angalia pia UNAIDS, “Guidance Note: Condom and Lubricant Programming in High HIV-Prevalence Countries,” https://www.unaids.org/sites/default/files/media_asset/condoms_guidancenote_en.pdf, p. 5.

[122] Kwa mfano, Human Rights Watch iliwahoji King, eneo limefichwa, Mei 21, 2018; Medard, eneo limefichwa, Mei 18, 2018; na Suleiman, kwa njia ya simu, Oktoba 2, 2018.

[123] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Ahmed kwa njia ya smu (jina bandia), Mei 22, 2018.

[124] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Yahya (jina bandia), eneo limefichwa, Juni 9, 2018. Kwa mujibu wa muhojiwa mmoja, bei ya chupa moja ya kilainishi katika duka la dawa jijini Dar es Salaam iko kati ya shilingi 3,000 na 12,000, au dola $1.30 na $5.20.

[125] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Jepheter (jina bandia), eneo limefichwa, Mei 25, 2018.

[126] Mahojiano ya simu kati ya Human Rights Watch na Victor (jina bandia), Septemba 28, 2018.

[127] Ibid.

[128] James Stannah et al., “HIV Testing and Engagement with the HIV Treatment Cascade Among Men Who Have Sex with Men in Africa: A Systematic Review and Meta-Analysis,” The Lancet 6 (2019), imepitiwa Disemba 17, 2019, doi:10.1016/S2352-3018(19)30239-5.

[129] Angalia, kwa mfano, UNAIDS na Stop AIDS Alliance, Communities Deliver: The Critical Role of Communities in Reaching Global Targets to End the Aids Epidemic, 2015, https://www.unaids.org/sites/default/files/media_asset/UNAIDS_JC2725_CommunitiesDeliver_en.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[130] Watoaji huduma za afya ulimwenguni kote wamejikuta katika wakati mgumu na vyombo vya sheria kwa kutoa huduma kwa makundi maalum. Kwa mfano, nchini Uganda mwaka 2014, polisi walivamia mradi wa Walter Reed Project, shirika la afya maarufu la Kimarekani linalotoa uhuduam za VVU kwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume, wakachukua mafaili. Nchini Cameroon mwaka 2018, polisi walivamia ofisi za shirika la vijana linalotoa huduma za VVU kwa makundi maalum. Polisi wamebumba mashitaka kama vile “kutangaza ushoga” kuhalalisha uvamizi wao, hata kama hakuna makosa kama hayo katika Kanuni ya Adhabu ya nchi nyingi, ikiwa ni pamoja na Uganda na Cameroon. “Uganda: Anti-Homosexuality Act’s Heavy Toll,” Taarifa ya Human Rights Watch kwa vyombo vya habari, Mei 14, 2014, https://www.hrw.org/news/2014/05/14/uganda-anti-homosexuality-acts-heavy-toll; “Cameroon: Arrest and Arbitrary Detention of Five Members of the Association Avenir Jeune de l’Ouest (AJO),” International Federation for Human Rights (FIDH) urgent appeal, Aprili 30, 2018, https://www.fidh.org/en/issues/human-rights-defenders/cameroon-arrest-and-arbitrary-detention-of-five-members-of-the (imepitiwa Disemba 19, 2019). Human Rights Watch haina taarifa ya nchi nyingine yoyote zaidi ya Tanzania ambayo ina maelekezo rasmi yakizuia mashirika ya kijamii kufanya warsha kwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume au makundi mengine maalum.

[131] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na mwakilishi wa shirika la Umoja wa Mataifa, Dar es Salaam, Machi 9, 2017.

[132] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Leticia (jina bandia), Naivasha, Kenya, Juni 16, 2019.

[133] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, “Kauli ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Mh. Ummy Mwalimu juu ya Huduma za VVU kwa Makundi Maalum nchini Tanzania, 27 Oktoba, 2016,” ipo kwenye faili la Human Rights Watch; inapatikana pia hapa https://m.facebook.com/afyatz/posts/1230922863594845.

[134] Ibid. Msisitizo kutoka nakala ya asili.

[135] Mahojiano ya simu kati ya Human Rights Watch na mwakilishi wa JHPIEGO, Oktoba 2, 2019.

[136] Mahojiano ya simu kati ya Human Rights Watch na Toni (jina bandia), Oktoba 9, 2018.

[137] Mahojiano ya video kati ya Human Rights Watch na Makame (jina bandia), Julai 3, 2018.

[138] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na King (jina bandia), eneo limefichwa, Mei 21, 2018.

[139] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Amy (jina bandia), eneo limefichwa, Mei 28, 2018.

[140] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, “Kauli ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Mh. Ummy Mwalimu juu ya Huduma za VVU kwa Makundi Maalum na yale yaliyo hatarini nchini Tanzania, na utekelezaji wake: 16 Februari, 2017,” www.nacp.go.tz/site/download/STATEMENT_ENGLISH.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019) na ipo katika faili la Human Rights Watch.

[141] Mahojiano ya simu kati ya Human Rights Watch na Ronnie (jina bandia), Septemba 7, 2018.

[142] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Victor (jina bandia), Septemba 28, 2018.

[143] Mahojiano kwa njia ya video kati ya Human Rights Watch na Makame (jina bandia), Julai 3, 2018.

[144] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Leticia (jina bandia), Oktoba 4, 2018.

[145] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Jephter (jina bandia), eneo limefichwa, Mei 25, 2018.

[146] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Medard (jina bandia), eneo limefichwa, Mei 18, 2018.

[147] Ibid.

[148] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Ahmed (jina bandia), Mei 22, 2018.

[149] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, “Kauli ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Mh. Ummy Mwalimu juu ya Huduma za VVU kwa Makundi Maalum na yale yaliyo hatarini nchini Tanzania, na utekelezaji wake: 16 Februari, 2017,” 16 Februari 2017, ipo kwenye faili la Human Rights Watch.

[150] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, VVU na UKIMWI (Kuzuia na Kudhibiti) Sheria, 2008, https://www.lrct.go.tz/download/laws_2008/28-2008_The%20HIV%20&%20AIDS%20(Prevention%20&%20Control)%20Act,%20Act%20No%2028%20of%202008.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[151] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, “Kauli ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Mh. Ummy Mwalimu juu ya Huduma za VVU kwa Makundi Maalum na yale yaliyo hatarini nchini Tanzania, na utekelezaji wake: 16 Februari, 2017, ipo katika faili la Human Rights Watch.

[152] Human Rights Watch na WASO, “Tuchukulie kama Binadamu.”

[153] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Osman (jina bandia), eneo limefichwa, Mei 22, 2018.

[154] Mahojiano ya simu kati ya Human Rights Watch na Suleiman (jina bandia), Oktoba 2, 2018.

[155] Mahojiano ya simu kati ya Human Rights Watch na Victor (jina bandia), Novemba 19, 2019.

[156] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Leila (jina bandia), eneo limefichwa, Mei 18, 2019.

[157] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Ronnie (jina bandia), Septemba 7, 2018.

[158] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Hassan (jina bandia), eneo limefichwa, Juni 28, 2018.

[159] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Ethan (jina bandia), eneo limefichwa, Mei 25, 2018.

[160] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Abdi (jina bandia), eneo limefichwa, Julai 4, 2018.

[161] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Stanley (jina bandia), eneo limefichwa, Mei 24, 2018.

[162] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Victor (jina bandia), Septemba 28, 2018.

[163] Avert, “HIV and AIDS in Tanzania,” https://www.avert.org/professionals/hiv-around-world/sub-saharan-africa/tanzania.

[164] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mpango wa Taifa wa Kudhibiti UKIMWI, “National Guidelines for the Management of HIV and AIDS,” Oktoba 2017, http://nacp.go.tz/site/download/NATIONAL_DECEMBER_2017.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019), uk. 183.

[165] Roger Pebody, “Taking Drugs On Time,” aidsmap, Januari 2017, https://www.aidsmap.com/about-hiv/basics/taking-drugs-time (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[166] Mahojiano ya simu kati ya Human Rights Watch na Victor (jina bandia), Septemba 28, 2018.

[167] Mahojiano ya video kati ya Human Rights Watch na Makame (jina bandia), Julai 3, 2018.

[168] Mahojiano ya simu kati ya Human Rights Watch na Leticia (jina bandia), Oktoba 4, 2018.

[169] Mahojiano ya simu kati ya Human Rights Watch na Toni (jina bandia), Oktoba 9, 2018.

[170] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Ronnie (jina bandia), Septemba 7, 2018.

[171] Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, 1977, imerekebishwa 2005, https://www.wipo.int/edocs/lexdocs/laws/en/tz/tz008en.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019), kipengele 20(1).

[172] Human Rights Watch, “Ukimwa Wangu, Usalama Wangu.”

[173] “Serikali Kuzifutia Usajili Asasi Zisizokuwa Za Kiserikali Zinazounga Mkono Mapenzi ya Jinsia Moja Nchini,” ITV, mara ya kwanza ilichapishwa https://www.itv.co.tz/news/local/1993-33856/Serikali_kuzifutia_usajili_na_kuzishtaki_asasi_zisizokuwa_za_kiserikali_zinazounga_mkono_ushoga_nchini.html?fbclid=IwAR3bJJmV27tJd3yQZG4xSe7ggl-IEcoGDtInBjUbUgl7oIegkZAfnsIHhF8 (haionekani tena) na imenukuliwa katika ukurasa wa Facebook wa Human Life International, https://www.facebook.com/HumanLifeInternational/posts/10155216627528569; ikachapishwa tena na Donatila, ikachapishwa “Jamii Forums” (blog), https://www.jamiiforums.com/threads/serikali-kuzifutia-usajili-asasi-zisizokuwa-za-kiserikali-zinazounga-mkono-ushoga-nchini.1088295. See also Sophie Tremblay, “‘Seeds of Hate’ Sown as Tanzania Starts LGBT Crackdown,” Guardian, https://www.theguardian.com/world/2016/aug/08/seeds-of-hate-sown-as-tanzania-starts-lgbt-crackdown.

[174] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, “Application for Registration as a Non-Governmental Organization,” http://www.tanzania.go.tz/egov_uploads/documents/application_en.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[175] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Sheria ya Mashirika yasio ya Kiserikali ya 2002, https://www.fiu.go.tz/NGOact.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[176] Affidavit of John Kashiha, Miscellaneous Civil Application No. 64 of 2016, Tanzanian High Court (Main Registry), Dar es Salaam, aya. 6 (ipo katika faili la Human Rights Watch).

[177] Ujumbe wa Hamisi Kigwangalla katika Twitter, Agosti 15, 2016, https://twitter.com/HKigwangalla/status/765265621483450368 (ilipitiwa Novemba 20, 2019).

[178] Mawasiliano ya barua pepe kati ya Human Rights Watch na mwanaharakati wa kanda wa afya na haki, Agosti 16, 2016.

[179] Katika Mahakama Kuu ya Tanzania (Usajili Mkuu) Dar es Salaam, Miscellaneous Civil Application No. 64 of 2016, ipo katika faili la Human Rights Watch.

[180] Mahojiano ya simu kati ya Human Rights Watch na John Kashiha, Machi 9, 2017.

[181] “State Suspends NGO Supporting Gay Marriages,” Daily News, Oktoba 21, 2017, iliripotiwa pia katika AllAfrica.com, https://allafrica.com/stories/201710270211.html (ilipitiwa Disemba 17, 2019).

[182] “Tanzania: Board Revokes Six NGOs’ License,” The Citizen (Dar es Salaam), https://www.thecitizen.co.tz/news/Tanzania--Board-revokes-six-NGOs--license/1840340-5079110-fhy0cl/index.html.

[183] Ripoti isiyo rasmi ya CHESA juu ya haki za LGBTQ ana wafanya biashara ya ngono, ipo kwenye faili pia la Human Rights Watch.

[184] Mawasiliano ya barua pepe kati ya Human Rights Watch na mwanaharakati wa kanda wa afya na haki, Disemba 16, 2019.

[185] Mahojiano ya simu kati ya Human Rights Watch na mwanasheria Mtanzania, Novemba 21, 2019.

[186] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Stanley (jina bandia), Mei 24, 2018.

[187] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Abdulkarim (jina bandia), eneo limefichwa, Januari 24, 2019.

[188] Ibid.

[189] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Amy (jina bandia), eneo limefichwa, Mei 28, 2018.

[190] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Sibongile Ndashe, mkurugenzi mtendaji, Initiative for Strategic Litigation in Africa (ISLA), Cape Town, South Africa, Julai 8, 2019.

[191] Ibid.; Mawasiliano ya barua pepe kati ya Human Rights Watch na Sibongile Ndashe, Novemba 20, 2019.

[192]Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Sibongile Ndashe, Cape Town, South Africa, Julai 8, 2019.

[193] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na mwanasheria anayeifahamu kesi hii, Novemba 21, 2019.

[194] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Leticia (jina bandia), Oktoba 4, 2018.

[195] Mahojiano kwa njia ya video kati ya Human Rights Watch na Makame (jina bandia), Julai 3, 2018.

[196] Sheria za Tanzania, Sura ya 16, Kanuni ya Adhabu, http://www.lrct.go.tz/?wpfb_dl=170, vipengele. 138A, 154, 157.

[197] Sheria ya Kanuni ya Adhabu ya Zanzibar. Kipengele 6 of 2004, http://defensewiki.ibj.org/images/9/90/Zanzibar_Penal_Code.pdf, vipengele. 150, 154, 158.

[198] Mahojiano ya simu kati ya Human Rights Watch na Victor (jina bandia), Septemba 28, 2018.

[199] Human Rights Watch na WASO, “Tuchukulie kama Wanadamu,” sehemu ya III.

[200] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na ofisa wa Umoja wa Mataifa Machi 9, 2017; Mawasiliano ya barua pepe kati ya Human Rights Watch na mtetezi wa haki za binadamu Zanzibar, Oktoba 24, 2019.

[201] “Tanzania Orders Arrest of Three Men for Promoting Homosexuality,” NBC News, Februari 8, 2017, https://www.nbcnews.com/feature/nbc-out/tanzania-orders-arrest-three-men-promoting-homosexuality-n718491; Sharifa Marira, “Polisi Dar yaanza msako wa mashoga,” post to “Jambo Leo” (blog), http://jambo-leo.blogspot.com/2017/02/polisi-dar-yaanza-msako-wa-mashoga.html.

[202] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Johnnie D, Mei 2, 2017.

[203] Ibid.

[204] Mawasiliano ya barua pepe kati ya Human Rights Watch na wanasheria na wanaharakati wa Tanzania, Machi and Aprili 2017.

[205] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Kim (jina bandia), Februari 7, 2019.

[206] Ibid.

[207] Ibid.

[208] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Kim (jina bandia), Nairobi, Julai 17, 2019.

[209] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na mtetezi wa haki za binadamu Zanzibar, Septemba 17, 2019.

[210] “Lesbian Kiss Video Posted and Shared Online Lands Tanzanians in Jail,” Toronto Sun, Disemba 8, 2017, https://torontosun.com/news/world/lesbian-kiss-video-posted-and-shared-online-lands-tanzanians-in-jail/wcm/c1676af7-4b79-41a7-8c5d-71b80d14c724 (imepitiwa Disemba 17, 2019); The Guardian Reporter, “Police Launch Manhunt For Second ‘Lesbian’ Engagement Party Suspect,” IPP Media, Disemba 3, 2017, https://www.ippmedia.com/en/news/police-launch-manhunt-second-lesbian-engagement-party-suspect (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[211] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Sheria ya Makosa ya Mtandao (2015), https://rsf.org/sites/default/files/the_cyber_crime_act_2015.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019), ibara 20.

[212] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na mwanasheria anayeifahamu kesi, Novemba 21, 2019. Hati zote za mashitaka zipokatika faili la Human Rights Watch.

[213] “Tanzania: 10 Men Arrested in Zanzibar for Being ‘Gay,’” Taarifa kwa vyombo vya habari ya Amnesty International, https://www.amnesty.org/en/latest/news/2018/11/tanzania-10-men-arrested-in-zanzibar-for-being-gay.

[214] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na mtetezi wa haki za binadamu Zanzibar, Septemba 17, 2019; “Wanaohisiwa kuwa mashoga wakamatwa zanzibar,” iliwekwa “Shilawata tz” (blog), Machi 4, 2017, http://shilawata.blogspot.com/2017/03/wanaohisiwa-kuwa-mashoga-wakamatwa.html (imepitiwa Disemba 19, 2019).

[215] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Fadil (jina bandia), eneo limehifadhiwa, Januari 24, 2019.

[216] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Fadil (jina bandia), eneo limehifadhiwa, Januari 24, 2019.

[217] Ibid.

[218] Ibid.

[219] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Suleiman (jina bandia), Oktoba 2, 2018.

[220] Ibid.

[221] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Victor (jina bandia), Septemba 28, 2018.

[222] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Ahmed (jina bandia), Mei 22, 2018.

[223] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Hassan (jina bandia), eneo limehifadhiwa, Juni 28, 2018.

[224] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Medard (jina bandia), eneo limehifadhiwa, Mei 18, 2018.

[225] Mahojiano kati ya Human Rights Watch na Fena (jina bandia), Nairobi, Januari 10, 2019.

[226] Jason Beaubien, “Top U.S. AIDS Official Touts Progress, Has Tough Words for Tanzania,” NPR, Disemba 1, 2016, https://www.npr.org/sections/goatsandsoda/2016/12/01/503988997/top-u-s-aids-official-touts-progress-has-tough-words-for-tanzania (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[227] “RC Makonda akitangaza kamati itakayotokomeza mashoga,” katika mkutano na waandishi wa habari, https://www.youtube.com/watch?v=ZFzhwL7HggA&feature=youtu.be.

[228] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na wanaharakati wa Tanzania, Novemba 2018.

[229] Ibid.

[230] Uwasilishaji katika mkutano wa kanda uliohudhuriwa na Human Rights Watch, Naivasha, Kenya, Juni 16, 2019.

[231] “Bachelet: Tanzania Has Duty to Protect – Not Further Endanger – LGBT People,” Ofisi ya Kamishna Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Binadamu, taarifa kwa vyombo vya habari habari, Novemba 2, 2018, https://www.ohchr.org/EN/NewsEvents/Pages/DisplayNews.aspx?NewsID=23817&LangID=E (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[232] “Diplomatic Pressure Results in Tanzania Stating Anti-Gay Crackdown is Not Government Policy,” The Journal (Ireland), https://www.thejournal.ie/tanzania-lgbt-arrests-4326426-Nov2018.

[233] Mawasiliano kwa njia ya barua pepe kati ya Human Rights Watch na mwanadiplomasia jijini Dar es Salaam, Disemba 16, 2019.

[234] Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, “Taarifa kwa Vyombo vya Habari,” Novemba 4, 2018, ipo katika faili pia la Human Rights Watch; “Paul Makonda: Vita dhidi ya ushoga Dar es Salaam si msimamo wa serikali,” BBC Kiswahili, 5, Novemba 2018, https://www.bbc.com/swahili/habari-46093978 (19, Septemba 2019). Angalia pia Pernille Bearendtsen, “Tanzania’s Stance on Homosexuality Points to an Increasingly Repressive Political Agenda,” PRI, 13, Novemba 2018, pri.org/stories/2018-11-13/tanzanias-stance-homosexuality-points-increasingly-repressive-political-agenda (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[235] “Tanzania: 10 Men Arrested in Zanzibar for Being ‘Gay,’” Taarifa ya Amnesty International kwa vyombo vya habari, https://www.amnesty.org/en/latest/news/2018/11/tanzania-10-men-arrested-in-zanzibar-for-being-gay.

[236] “Homosexuality Illegal in Tanzania – Govt Insists,” Daily News (Dar es Salaam), ilichapiswa tena AllAfrica.com, Novemba 10, 2019, https://allafrica.com/stories/201811120100.html (imepitiwa Disemba 17, 2019); angalia pia Bunge La Tanzania, Majadiliano Ya Bunge, Mkutano wa Kumi na Tatu,” 9, Novemba 2018, https://www.bunge.go.tz/polis/uploads/documents/1543929886-9%20NOVEMBA,%202018.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[237] “Deterioration of Civil Liberties and Human Rights in Tanzania,” Taarifa ya Idara ya Mambo ya Nje ya Marekani kwa Vyombo vya Habari, Novemba 9, 2019, https://www.state.gov/deterioration-of-civil-liberties-and-human-rights-in-tanzania (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[238] “Danmark tilbageholder millioner til Tanzania for homofobi,” DR (Denmark), Novemba 14, 2018, https://www.dr.dk/nyheder/politik/danmark-tilbageholder-millioner-til-tanzania-homofobi, Unofficial English translation available at https://www.jamiiforums.com/threads/denmark-withholds-aid-and-cancels-minister-visit-to-tanzania-over-human-rights-situation.1508470 (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[239] Alex Malanga, “Mahiga: Denmark’s Aid Intact,” The Citizen (Dar es Salaam), https://www.thecitizen.co.tz/News/Mahiga--Denmark-s-aid-intact/1840340-4875198-68ftm2/index.html; Mawasiliano kwa njia ya email kati ya Human Rights Watch na Susanne Branner Jespersen, LGBT Denmark, Disemba 4, 2018.

[240] “IAS Condemns Tanzania’s Anti-Gay Initiatives,” International AIDS Society (IAS) taarifa kwa vyombo vya habari, Disemba 12, 2018, http://i-base.info/htb/35410 (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[241] Uganda ina utofauti wa pekee. “World Bank Freezes Aid to Uganda Over Gay Law,” Al Jazeera, Februari 28, 2014, https://www.aljazeera.com/news/africa/2014/02/world-bank-freezes-aid-uganda-over-gay-law-201422874410793972.html (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[242] Mkutano kati ya Human Rights Watch Kikosi Kazi cha Benki ya Dunia cha SOGI, Washington, D.C., Aprili 9, 2019. Tangazo lilichapishwa https://wbappse.worldbank.org/WBG_BPC_1818SOCIETY_RSSFEEDAPPWEB/announcements/announcementresources# lakini halipo tena hadi wakati wa kuandikwa kwa ripoti hii. Angalia pia Hillary Orinde, “Unsafe Place? World Bank Cancels Missions to Tanzania,” Standard Digital (Nairobi), https://www.standardmedia.co.ke/article/2001302127/world-bank-suspends-funding-to-tanzania.

[243] Karen McVeigh, “World Bank Pulls $300m Tanzania Loan Over Pregnant Schoolgirl Ban,” Guardian, Novemba 15, 2018, https://www.theguardian.com/global-development/2018/nov/15/world-bank-pulls-300m-tanzania-loan-over-pregnant-schoolgirl-ban (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[244] Mahojiano ya Human Rights Watch na Makamu wa Rais wa Benki ya Dunia kwa Afrika Hafez Ghanem, Washington, D.C., Februari 5, 2019.

[245] Ibid.

[246] “World Bank Statement on Lifting the Suspension of Missions to Tanzania,” Taarifa ya Benki ya Dunia kwa vyombo vya habari, https://www.worldbank.org/en/news/statement/2018/11/20/world-bank-statement-on-lifting-the-suspension-of-missions-to-tanzania.

[247] Barua ya Human Rights Watch kwa mwakilishi wa ubalozi nchini Tanzania, Oktoba 12,2019.

[248] Orodha ya wanufaika wote wa mfuko wa PEPFAR na anuani za “Muhtasari wa Dira ya Mkakati” wao zinapatikana hapa https://www.state.gov/where-we-work-pepfar (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[249] Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, “Information Memo for Chargé Inmi Patterson,” kutoka S/GAC - Ambassador Deborah Birx, Januari 16, 2019, https://www.pepfar.gov/documents/organization/289828.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019); Andrew Green, “What’s Behind PEPFAR’s Funding Cut Threats?” Devex, Juni 11, 2019, devex.com/news/what-s-behind-pepfar-s-funding-cut-threats-95053 (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[250] Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, “Information Memo for Chargé Inmi Patterson,” kutoka S/GAC - Ambassador Deborah Birx, https://www.pepfar.gov/documents/organization/289828.pdf; Andrew Green, “What's Behind PEPFAR’s Funding Cut Threats?” Devex, devex.com/news/what-s-behind-pepfar-s-funding-cut-threats-95053.

[251] Mahojiano kwa njia ya simu kati ya Human Rights Watch na Stephen Leonelli, MPact, Septemba 19, 2019. Tamko lipo katika faili la Human Rights Watch. Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wizara wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee no Watoto, Kumb. Na. CGA.16/209/01C, “Yah: Taratibu za Uchunguzi wa Kitabibu kwa Washukiwa wa Makosa ya Kujamiiana Watu wa Jinsia Moja,” Januari 14, 2019, ilipigwa sahihi na Prof. Muhammad B. Kambi, Mganga Mkuu.

[252] MPact, “Prohibit Forced Anal Examinations Now! Petition to Government of Tanzania,” https://mpactglobal.org/civil-society-petition-regarding-forced-anal-exams-in-tanzania.

[253] Mazungumzo ya barua pepe ya Human Rights Watch na Afisa wa PEPFAR, Januari 9, 2020.

[254] Makataba wa Afrika (Banjul) wa Haki za Binadamu na Watu, umepitishwa Juni 27, 1981, OAU Doc. CAB/LEG/67/3 rev. 5, 21I.L.M. 58 (1982), umeanza kufanya kazi Oktoba 21, 1986, ukakubaliwa na Tanzania Februari 18, 1984, ibara ya. 16; Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiuchumi, Kijamii na Kitamaduni (ICESCR), umepitishwa Disemba 16, 1966, G.A. Res. 2200A (XXI), 21 U.N. GAOR Supp. (No. 16) at 49, U.N. Doc. A/6316 (1966), 993 U.N.T.S. 3, umeanza kufanya kazi Januari 3, 1976, umekubaliwa na Tanzania Juni 11, 1976, ibara ya. 12; Makataba wa Kuondoa Aina Zote za Ubaguzi Dhidi ya (CEDAW), uliopitishwa Disemba 18, 1979, G.A. res. 34/180, 34 U.N. GAOR Supp. (No. 46) at 193, U.N. Doc. A/34/46, ukaanza kufanya kazi Septemba 3, 1981, ukakubaliwa na Tanzania Agosti 20, 1985, ibara ya 12.

[255] Kamati ya Umoja wa mataifa ya Haki za Kiuchumi, Kijamii na Kitamaduni, Ujumbe wa Jumla No 14, Haki ya Upatikanaji wa Kiwango cha Juu cha Afya (Ibara ya. 12), E/C.12/2000/4 (2000), aya ya 16.

[256] Ibid., aya ya 12(b).

[257] Angalia Kamati ya Umoja wa mataifa ya Haki za Kiuchumi, Kijamii na Kitamaduni, Ujumbe wa Jumla No. 20, Kutokuwa na ubaguzi katika haki za kiuchumi, kijamii na kitamaduni (ibara ya. 2,aya ya. 2, ya Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiuchumi, Kijamii na Kitamaduni (ICESCR), E/C.12/GC/20, July 2, 2009, aya ya. 32. Wakati ibara ya 12 ya ICESCR inahakikisha haki ya afya, ibara ya 12(2) inalinda watu dhidi ya ubaguzi wa kupata haki zote zilizohakikishwa na mkataba. Ujume wa Jumla wa 20 unafafanua kwamba ubaguzi unazuiliwa kwa misingi ya urengwa wa ngono na utambulisho wa kijinsia. 

[258] Itifaki ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu juu ya Haki za Wanawake Afrika, iliopitishwa na Mkutano wa Pili wa Baraza la Kawaida la Mkutano wa Umoja wa Afrika, Maputo, Septemba 13, 2000, CAB/LEG/66.6, ilianza kufanya kazi Novemba 25, 2005, ibara. 14(1)d.

[259] Mswaada wa Sheria wa Kudhibiti na Kuzuia VVU & UKIMWI wa Afrika Mashariki, ulitungwa 2016, upo katika faili la Human Rights Watch, kipengele cha 39, kipengele cha 12(b). Barua inataja moja kwa moja “ubora wa mipira ya kiume na kike,” lakini, vilainishi vya maji na silika pia vingeweza kufaa kama mbinu za kujikinga zinazotambulika. Angalia, kwa mfano, ripoti ya Shirika la Afya Duniani na UNAIDS, The Male Latex Condom: 10 Condom Programming Fact Sheets, http://www.unaids.org/en/media/unaids/contentassets/dataimport/publications/irc-pub01/jc003-malecondom-factsheets_en.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019), uk. 7.

[260] SADC, Minimum Standards for the Integration of HIV and Sexual & Reproductive Health in the SADC Region, 2015, http://menengage.org/wp-content/uploads/2016/09/Minimum-Standards-for-Integration-of-HIV-and-SRH-in-SADC-Region.pdf (imepitiwa Disemba 16, 2019), uk. 17.

[261] Ibid., uk. 19.

[262] Ibid.

[263] Ibid., uk. 20.

[264] Ibid.

[265] Ibid., uk. 21.

[266] SADC, “Statement: SADC Ministers of Health and Ministers Responsible For HIV And Aids Meet In Namibia 8th November 2018,” Windhoek, Novemba 8, 2018, https://www.sadc.int/files/3315/4169/8409/Media_Statement_-_Joint_Meeting_of_SADC_Ministers_of_Health_and_those_responsible_for_HIV_and_AIDS_.pdf (imepitiwa Disemba 19, 2019).

[267] SADC, “Strategy for Sexual and Reproductive Health and Rights in the SADC Region, 2019-2030,” Andiko la 1, Oktoba 1, 2018, http://genderlinks.org.za/wp-content/uploads/2018/11/1-Final-signed-SADC-SRHR-Strategy-2019-2030.pdf (imepitiwa Disemba 16, 2019), uk. 36. Andiko hili liliidhinishwa Novemba 2018.

[268] Ibid., uk. 29, 44.

[269] Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Azimio lililofikiwa na Bara Kuu tarehe 8 Juni 2016, “Political Declaration on HIV and AIDS: On the Fast Track to Accelerating the Fight against HIV and to Ending the AIDS Epidemic by 2030,” A/RES/70/266, https://www.unaids.org/sites/default/files/media_asset/2016-political-declaration-HIV-AIDS_en.pdf.

[270] UNAIDS, Ripoti ya Ufa wa Kujikinga, 2016, http://www.unaids.org/sites/default/files/media_asset/2016-prevention-gap-report_en.pdf (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[271] Kamisheni ya Dunia ya VVU na Sheria, HIV and the Law: Risks, Rights & Health, Julai 2012, https://hivlawcommission.org/report (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[272] Kwa mfano, utafiti uliofanya nchini Nigeria uligundua kwamba kupitishwa kwa Sheria ya mwaka 2014 ya Kuzuia Ndoa za Jinsia Moja katika nchi hiyo kuliendana mara moja na kushuka kwa mwamko wa kutafuta huduma za VVU miongoni mwa wanaume wanaofanya mapenzi na wanaume. Dr. Sheree R. Schwartz et al., “The Immediate Effect of the Same-Sex Marriage Prohibition Act on Stigma, Discrimination, and Engagement on HIV Prevention and Treatment Services in Men Who Have Sex With Men in Nigeria: Analysis of Prospective Data from the TRUST Cohort,” The Lancet 2 (2015) , imepitiwa Disemba 17, 2019, doi:10.1016/S2352-3018(15)00078-8.

[273] Makataba wa Afrika (Banjul) wa Haki za Binadamu na Watu, umepitishwa Juni 27, 1981, OAU Doc. CAB/LEG/67/3 rev. 5, 21I.L.M. 58 (1982), ukaanza kufanya kazi Oktoba 21, 1986, ukakubaliwa na Tanzania Februari 18, 1984, ibara. 11.

[274] Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa (ICCPR), umepitishwa Disemba 16, 1966, G.A. Res. 2200A (XXI), 21 U.N. GAOR Supp. (No. 16) at 52, U.N. Doc. A/6316 (1966), 999 U.N.T.S. 171, ukaanza kufanya kazi Machi 23, 1976, Ukakubaliwa na Tanzania Juni 11, 1986, ibara. 2, 22.

[275] Kamisheni ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, HIV, the Law and Human Rights in the African Human Rights System: Key Challenges and Opportunities for Rights-Based Responses, https://www.unaids.org/sites/default/files/media_asset/HIV_Law_AfricanHumanRightsSystem_en.pdf, aya. 87.

[276] Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa (ICCPR), umekubalika Disemba 16, 1966, G.A. Res. 2200A (XXI), 21 U.N. GAOR Supp. (No. 16) at 52, U.N. Doc. A/6316 (1966), 999 U.N.T.S. 171, ukaanza kutumika Machi 23, 1976, ukakubaliwa na Tanzania Juni 11, 1986. ibara ya 2 na 26 ya ICCPR inahakikisha usawa wa watu wote mbele ya sheria na haki ya kutokubaguliwa. Ibara ya 17 inalinda haki ya faragha. Angalia pia Toonen v. Australia, 50th Sess., Mawasiliano No. 488/1992, U.N. Doc CCPR/C/50/D/488/1992, Aprili 14, 1994, sec. 8.7.

[277] François Ayissi et al. v. Cameroon, Working Group on Arbitrary Detention, Opinion No. 22/2006, U.N. Doc. A/HRC/4/40/Add.1 at 91 (2006), aya. 20, ipo pia kwenye faili la Human Rights Watch.

[278] Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ibara. 16.

[279] Angalia Kamisheni ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, Zimbabwe Human Rights NGO Forum v. Zimbabwe, sec. 169, AHRLR 128 (ACHPR 2006); Makataba wa Afrika (Banjul) wa Haki za Binadamu na Watu, umepitishwa Juni 27, 1981, OAU Doc. CAB/LEG/67/3 rev. 5, 21I.L.M. 58 (1982), ukaanza kutumika Oktoba 21, 1986, ukakubaliwa na Tanzania Februari 18, 1984, ibara. 2.

[280] Kamisheni ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu, Azimio la 275, “Resolution on Protection against Violence and other Human Rights Violations against Persons on the basis of their real or imputed Sexual Orientation or Gender Identity,” limepitishwa mwaka 2014, https://www.achpr.org/sessions/resolutions?id=322 (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[281] Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ibara ya. 9. Matumizi ya herufi kubwa yamefuata andiko halisi.

[282] Ibid., ibara ya. 13.

[283] Tanzania ni kati ya nchi chache ambazo hazijaingiza katika sheria zake Mkataba dhidi ya mateso na udharirishaji wa namna nyingin,. Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa (ICCPR), umepitishwa Disemba 16, 1966, G.A. Res. 2200A (XXI), 21 U.N. GAOR Supp. (No. 16) at 52, U.N. Doc. A/6316 (1966), 999 U.N.T.S. 171, ukaanza kutumika Machi 23, 1976, ukapokelewa Tanzania tarehe Juni 11, 1976, ibara ya . 7; Mkataba wa Afrika wa haki za Binadamu na Watu unakataza pia mateso au udharirishaji wa aina nyingine yoyote. Makataba wa Afrika (Banjul) wa Haki za Binadamu na Watu, umepitishwa Juni 27, 1981, OAU Doc. CAB/LEG/67/3 rev. 5, 21 I.L.M. 58 (1982), ukaanza kutumika Oktoba 21, 1986, ukakubaliwa na Tanzania Februari 11, 1984, ibara ya. 5.

[284] Kamati dhidi ya Mateso, “Consideration of Reports Submitted by States Parties Under Article 19 of the Convention: Conclusions and recommendations of the Committee against Torture, Egypt,” CAT/C/CR/29/4, Disemba 23, 2002, http://www.refworld.org/docid/4f213bf92.html (imepitiwa Disemba 16, 2019, aya. 6(k).

[285] Kikundi Kazi cha Umoja wa Mataifa cha Ukamataji Holela , Ripoti ya Kikundi kazi cha Ukamataji Holela,

 A/HRC/16/47/Add.1, opinion no. 25/2009 (Misri), Machi 2, 2011, uk. 20, aya. 24, 28-29, http://www2.ohchr.org/english/bodies/hrcouncil/docs/16session/A.HRC.16.47.Add.1_AEV.pdf (imepitiwa Disemba 16, 2019).

[286] Ofisi ya Kamishna Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Binadamu, “Discrimination and Violence Against Individuals Based on Their Sexual Orientation and Gender Identity,” A/HRC/29/23, Mei 4, 2015, http://www.ohchr.org/EN/HRBodies/HRC/RegularSessions/Session29/Documents/A_HRC_29_23_en.doc (imepitiwa Disemba 16, 2019).

[287] ILO, OHCHR, UNDP, UNESCO, UNFPA, UNHCR, UNICEF, UNODC, UNWOMEN, WFP, WHO, and UNAIDS, “Ending Violence and Discrimination against Lesbian, Gay, Bisexual, Transgender and Intersex People,” Septemba 2015, http://www.ohchr.org/Documents/Issues/Discrimination/Joint_LGBTI_Statement_ENG.PDF (imepitiwa Disemba 18, 2019).

[288] Mkutano Mkuu wa Umoja wa Mataifa, “Report of the Special Rapporteur on the Question of Torture and Other Cruel, Inhuman or Degrading Treatment or Punishment,” A/56/156, Julai 3, 2001, https://digitallibrary.un.org/record/446206?ln=en (imepitiwa Disemba 19, 2019), aya. 24.

[289] Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa, “Report of the Special Rapporteur on torture and other cruel, inhuman or degrading treatment or punishment,” A/HRC/31/57, Januari 5, 2016, http://www.refworld.org/docid/56c435714.html (imepitiwa Disemba 16, 2019), aya. 36.

[290] Kamisheni ya Afrika ya Haki za BInadamu na Watu, Maoni ya Jumla No. 4 juu ya Mkataba wa Afrika wa Haki za Binadamu na Watu: The Right to Redress for Victims of Torture and Other Cruel, Inhuman or Degrading Punishment or Treatment (ibara 5), (imepitishwa na Mkutano Mkuu wa Kamisheni wa 21, uliofanyika kwanzia Februari 23 hadi Machi 4 2017), https://www.achpr.org/legalinstruments/detail?id=60 (imepitiwa Disemba 17, 2019).

[291] Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Kupinga Mateso, ulitiwa sahihi Disemba 10, 1984, G.A. res. 39/46, annex, 39 U.N. GAOR Supp. (No. 51) at 197, U.N. Doc. A/39/51 (1984), ukaanza kutumika Juni 26, 1987, ibara ya. 1; Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa, ibara ya. 4(2).